Mwanamuziki wa Hip Hop nchini Farid Kubanda Fid Q (wa pili kulia)akizungumza na waandishi wa habari kuhusu tamatasha la muziki Hip Hop Asili ambalo litafanyika Juni mwaka huu jijini Dar es Salaam.Wa pili kushoto ni Mkuu wa Idara Ushirikiano na Utamaduni kutoka Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania Cecile Frobert.
Mussa Sango(wa kwanza kulia) ambaye ni mmoja ya waandaaji wa tamasha hilo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Boresha Redio akifafanua jambo kuhusu kuelekea tamasha hilo.



Mkuu wa Idara Ushirikiano na Utamaduni kutoka Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania Cecile Frobert(wa pili kushoto) akizungumza namna ambavyo Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania ambavyo umeamua kusaidia kufanikisha tamasha hilo la muziki wa Hip Hop Asili.

 

Said Mwishehe, Michuzi TV

TAMASHA la muziki wa Hip Hop asili linatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Juni 25 hadi Juni 27 mwaka huu ikiwa ni mkakati wa kuibua wasanii wasiosikia katika muziki huo.

Katika kuelekea tamasha hilo waandaaji wa tamasha hilo wamesema kutakuwa na ratiba ya kwenda mikoani kusaka vipaji vya wasanii wa muziki huo na baada ya hapo watakuja kushiriki kwenye tamasha kubwa ambalo litafanyika katika tarehe hizo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza leo Februari 1,2021 katika Kituo cha Udamaduni cha Alliance de France, Mwanamuziki wa muziki wa Hip Hop Farid Kubanda a.k.a Fid Q amesema tamasha hilo litafanyika chini ya ufadhili wa Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania kwa kushirikiana na wadau wengine wa muziki huo wakiwemo Art Space ambao wametoa eneo ambalo tamasha hilo litafanyika.

"Tumekutana hapa leo kuzungumzia tamasha ambalo liko mbele yetu, tunatarajia kulifanya Juni mwaka huu na kabla ya hapo kutakuwa na shughuli ndogo ndogo ambazo zitaendelea na miongoni mwa shughuli hizo ni kwenda mikoani kusaka vipaji vya muziki wa hip hop asili.

"Hivyo Februari 5 mwaka huu tutakuwa Mjini Dodoma pale katika Klabu ya  T Squre ambayo ina hadhi, ina steji nzuri ambapo wasanii watakuwa huru kuonesha vipaji vyao. Baada ya hapo tutakwenda Zanzibar.

"Ni matumaini yetu kupitia tamasha hilo tunakwenda kuibua vipaji vya muziki huo ambavyo havijapata nafasi ya kusikika.Tunawashukuru Ubalozi wa Ufaransa kwa kutusaidia katika hili na tunatamani kuona tunalifanya kila mwaka kama wataendelea kutufadhili,"amesema Fid Q.

Amefafanua baada ya kufanya Dodoma na Zanzibar pia watatoa ratiba ya mikoa mingine ambayo watakwenda kuibua vipaji ambavyo mwisho wa siku vitakutanishwa katika Jiji la Dar es Salaam kuanzia hiyo Juni 25 hadi Juni 27 mwaka huu ambapo itakuwa siku ya Ijumaa, Jumamosi na Jumapili.

Fid Q ameongeza kupitia tamasha hilo mbali ya kuibua vipaji, litakwenda kuutangaza zaidi muziki hu na kwamba Hip Hop ni maisha ya kila siku ya mwanadamu, hivyo katika muziki huo kuna kitu zaidi ya kimoja ambacho msanii anakifanya.

"Wakati tunaelekea katika tamasha hilo tutakuwa na matukio mengi, tutawajengea uwezo wasanii ambao watapatikana, tutawapa mafundisho ya kuutumia muziki huo katika fikra chanya zaidi kuliko kuwaza fikra hasi,"amesema na kuongeza tamasha hilo mbali ya kuwa na wasanii wa Tanzania litahusisha na wasanii kutoka mataifa mengine ili kuongeza ladha ya burudani.

Kuhusu kiingilio amesema watavitangaza lakini kwa wale ambao watakata tiketi ya siku zote tatu kwa wakati mmoja kutakuwa na punguzo ukilinganisha na yule ambaye atakata tiketi ya siku moja moja ambayo itakuwa juu kidogo.

Kwa upande wake Mkuu wa Idara Ushirikiano na Utamaduni kutoka Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania Cecile Frobert ameeleza wazi Ubalozi wa Ufaransa umekuwa na mkakati wa kuhakikisha wasanii wanapata nafasi ya kuonesha vipaji vyao, hivyo wameamua kusaidia kufanikisha tamasha hilo la kuibua vipaji vya Hip hop asili.

Amesema ni tamasha kubwa ambalo litakuwakutanisha wasanii kutoka mataifa megine yakiwemo ya Kenya na Uganda , hivyo amesisitiza wataendelea kusaidia katika kuhakikisha wasanii wanasaidia katika kufanya kazi yao ya sanaa huku akiweka wazi katika tamasha hilo ni matarajio yao kuona kuna ushiriki wa wasanii wa kike.

Kuhusu tamasha hilo iwapo watakuwa wakilifadhili kila mwaka, amesema ni mapema kwa sasa kutoa majibu lakini ni matumaini yao huko mbele ya safari watajua ni jinsi gani wanaweza kusaidia kwani wamekuwa wakifanya hivyo mara kwa mara kufanikisha matamsha mbalimbali ya wasanii wa aina tofauti tofauti.

Wakati huo huo Mussa Sango ambaye ni moja ya washiriki katika kuandaa tamasha hilo, amesema wanayo redio ambayo imekuwa ikisaidia kuibua vipaji vya wasanii, hivyo kupitia tamasha hilo watakuwa na jukumu la kusaidiana na Fid Q na wadau wengine kusaka vipaji vipya vya muziki huo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...