Chanzo cha Mto Ruvuma kilichopo katika Milima Matogoro



 

Na Albano Midelo

MTO Ruvuma ni miongoni mwa vivutio vitano vya utalii vinavyoubeba Mkoa wa Ruvuma.Vivutio vingine ni ziwa Nyasa,Makumbusho ya Taifa ya Majimaji,ushoroba wa Selous-Niassa,Hifadhi ya Taifa ya Nyerere na utalii wa kiutamaduni na kihistoria.

Mratibu wa Utalii Kanda ya Kusini Deborah Mwakanosya anasema Mto Ruvuma umeubeba Mkoa wa Ruvuma kwa kuwa umepita katika wilaya zote tano ambazo ni Songea,Mbinga,Nyasa,Namtumbo na Tunduru.

Mwakanosya anasema Mto Ruvuma ndiyo Mto mrefu kuliko yote katika nchi za Afrika Mashariki na miongoni mwa mito maarufu barani Afrika ukiwa umeanzia kwenye misitu ya milima ya Matogoro Manispaa ya Songea na kumwaga maji yake Bahari ya Hindi.

“Mto Ruvuma umedhihirisha maajabu ya Mungu ambayo hayawezi kusimuliwa katika mikoa mingine nchini,ispokuwa Mkoa wa Ruvuma,katika milima ya Matogoro Manispaa ya Songea tunakutana na chanzo cha mto Ruvuma,ukiona chanzo hicho,ni mfano wa kisima kidogo sana ambacho kimetoa mfereji mdogo,lakini kazi yake huko mbele huwezi kuongelea katika hali ya kawaida na kueleweka kwa jamii’’,anasisitiza Mwakanosya.

Anasema kisima hicho kidogo chenye mfereji mdogo kwenye milima ya Matogoro kipo meta 1500 toka usawa wa bahari kimekwenda kuunda mto maarufu duniani unaoitwa Ruvuma ukiwa na urefu za kilometa zaidi ya 800 na upana wa kati ya meta 300 hadi 500 kutegemea na eneo lililopo kwa sababu kuna baadhi ya maeneo mto huo una upana mkubwa zaidi.

Kwa mujibu wa mhifadhi huyo,Mto Ruvuma  umebeba fukwe mbalimbali zinazovutia wageni wengi ambapo anazitaja fukwe nyingi za kuvutia zinapatikana kwa wingi katika hifadhi ya Taifa ya mazingira asilia ya Mwambesi iliyopo wilayani Tunduru.

Anasema katika hifadhi hiyo ,Mto Ruvuma umetengeneza visiwa na fukwe nzuri za kuvutia ambazo zinamwezesha mtalii kuogelea na kuona wanyama wengi ambao wapo katika hifadhi hiyo kando kando ya Mto Ruvuma wakiwemo tembo,mamba,simba,jamii ya swala na samaki wa aina mbalimbali.

Hata hivyo Mratibu huyo wa Utalii Kanda ya Kusini anasema ili mto huo uweze kufika katika Bahari ya Hindi na kumwaga maji yake,unaanzia wilaya ya Songea milima ya Matogoro,unapita katika shamba maarufu la AVIV ambalo wanaendesha kilimo cha umwagiliaji wa zao la kahawa kupitia mto Ruvuma ambapo wameajiriwa watumishi zaidi ya 3000.

Kutokea hapo mto huo umepita hadi katika eneo la Tulila wilayani Mbinga ambako Shirika la watawa wa katoliki wa mtakatifu Agnes wameweka mradi mkubwa wa umeme wa maji kwenye maporomoko ya Mto Ruvuma Chanzo hicho kinamilikiwa na watawa wabenediktine wa Mtakatifu Agnes Chipole Jimbo Kuu Katoliki la Songea.

Akizungumza kwa niaba ya Mama Mkuu wa Shirika hilo,Sr.Richards Chiwinga(OSB) anasema wana mashine mbili ambazo zina uwezo wa kuzalisha megawatts tano.

Analitaja bwawa la Tulila kuwa lina ukubwa wa meta za ujazo milioni 1.14,likiwa na urefu wa meta 750 toka usawa wa bahari na usawa wa maji(level) ni meta 748 na kwamba maji yakizidi kiwango hicho yanamwagika.

Maporomoko ya Mto Ruvuma katika eneo la Tulila yana  mandhari nzuri ya kuvutia unaweza kufanya utalii wa kupiga picha, kuogelea, kuendesha mtumbwi, pia kuna fukwe nzuri kutoka katika mto Ruvuma ambao ni miongoni mwa mito maarufu barani Afrika ambao unamwaga maji yake Bahari ya Hindi.

Mto Ruvuma katika Wilaya ya Nyasa umepita kwenye Pori la Akiba la Liparamba ambako katika eneo la Nakatuta kuna maporomoko mazuri ya maji ya mto Ruvuma ambayo yanavutia wageni wengi pia katika eneo hilo mtalii anaweza kufanya utalii wa kuvua samaki na kupanda kwenye tabaka la jiwe kando kando yam to Ruvuma..

Safari ya mto Ruvuma kutoka Liparamba imeendelea hadi eneo la Mkenda mpakani mwa Tanzania na Msumbiji ambako kumejengwa daraja kubwa lenye urefu wa meta 98 linalogawa Tanzania na Msumbuji kupitia Mto Ruvuma.

Mwakanosya anabainisha zaidi kuwa Mto Ruvuma umeendelea hadi katika wilaya ya Namtumbo kwenye Jumuiya za uhifadhi wanyamapori vijijini ambazo ni Kimbanda,Kisungule na Chingoli na kwamba Mto Ruvuma unaendelea hadi katika msitu wa Hifadhi ya mazingira asilia Mwambesi wilayani Tunduru.

“Mto Ruvuma katika hifadhi ya mwambesi kuna vivutio vya aina zote ikiwemo michezo ya kuendesha mitumbwi ambayo kwa mara ya kwanza Tanzania mchezo wa kuendesha mitumbwi ulizinduliwa mwaka 2019 katika eneo la Wenje Mto Ruvuma na watalii 22 ambao walitoka nchi 16 duniani  walishiriki’’,anasisitiza Mwakanosya.

Anasema mto huo ukishapita katika wilaya zote za mkoa wa Ruvuma unaendelea na safari yake hadi katika daraja la umoja wilayani Nanyumbu mkoani Mtwara na kuendelea hadi mkoani Mtwara.

Mto Ruvuma unamwaga maji yake katika Bahari ya Hindi kwenye eneo la kati ya Mtwara nchini Tanzania na Rasi ya Delgado nchini Msumbiji.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...