Mtalaam wa viwango kutoka Shirika la Viwango nchini (TBS) Bi. Fatuma Mauniko akitoa mafunzo kwa wasindikaji kutoka wilaya 5 za Mkoa wa Morogoro
**************************
Na Mwandishi wetu,Ifakara
Mtalaam wa viwango kutoka Shirika la Viwango nchini (TBS) Bi. Fatuma Mauniko amewashauri Wasindikaji wa zao la mpungo Mkoani Morogoro.
Akitoa elimu kuhusu maswala ya viwango vya mchele nchini yaliyoandaliwa na Baraza la Mchele kwa kushirikiana na REPOA, mtalaamu huyo alisema kwamba mashine za kukoborea mchele pamoja na magala yanoyotumika katika kuhifadhia mchele hayakidhi viwango ili kutoa mchele ulio bora.
“Ni vema Wasindikaji wetu wakaboresha nyenzo zao iwapo wanataka kufikia katika bei shindani ambayo itawawezesha kupata kipato cha juu zaidi katika masoko makubwa ya ndani na nje ya nchi”, alisema.
Bi. Mauniko alisema kwamba Wasindikaji wengi wana elimu ndogo inayohusu ubora na usalama wa mchele, hivyo kukosa masoko na bei shindani, jambo ambalo linawakosesha mapato makubwa.
Warsha hiyo ya siku tatu ilizinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mheshimiwa Loata Ole Sanare, na kuhudhuriwa na Wasindikaji kutoka wilaya ya Mvomero, Malinyi, Ulanga, Kilosa na Ifakara.
Katika ufunguzi wake, Mkuu huyo wa Mkoa alisema zao la mchele ni zao la Mkoa wa Morogoro, hivyo angependa kuona kwamba kero zote zinazowahusu wasindikaji wa zao la mchele ziweze kutatuliwa.
“Ziorodhosheni kero zote ili iwe rahisi kwangu kuweza kuzifuatilia. Kuna kero zinazowahusu wenzetu wa Shirika la Umeme Tanzania, nyingine Wakala wa Barabara za Vijijini na nyingine wakala wa Barabara nchini (TANROADS”, alisema na kuongeza kwamba ushirikiano wa pamoja na sekta binafsi utaharakisha katika kutatua changamoto zinazowakabiri wasindikaji wa mchele.
Mkuu huyo wa Mkoa alisema ataitisha kikao cha wadau wote ili wazijadili changamoto hizo kwa pamoja.
Akizungumza katika Warsha hiyo, Mtalaam wa Mawasiliano Mwandamizi kutoka REPOA, Bwana Godfrey Kalagho alisema mafunzo hayo ni sehemu ya programmu ya utafiti na kujenga uwezo wa watunga sera, wazalishaji, na wauzaji biadhaa nje ya nchi kutathimi sera na kusaidia kuboresha ushindani na kutanua wigo wa masoko.
Alisema mradi huo unafadhiliwa na Jumuiya ya Ulaya na kusimamiwa na Sekretiati ya Jumuiya ya nchi za Afrika, Caribbean, na Pacific (OACPS), na kutekelezwa na REPOA na taasisi ya mafunzo ya maendeleo ya Chuo Kikuu cha Erasmus Rotterdam (ISS).
Maeneo mahususi ya mradi huo ni bidhaa za mboga mboga, mchele, ngozi, mwani, na huduma za usafirishaji.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...