Na Amiri Kilagalila,Njombe
Vifaa vitumikavyo kwenye ibada,vilivyokuwa vimechukuliwa na watu wasiojulikana Parokiani Wanging'ombe mkoani Njombe, vimepatikana vyote siku ya jana 15.03.2021majira ya asubuhi vikiwa vimewekwa ndani ya mfuko mmoja (shangazi kaja) na kutelekezwa nje ya nyumba ya mkuu wa sekondari ya Wanging'ombe.
Kwa mujibu wa taarifa ya kupatikana kwa vifaa hivyo Katibu wa Askofu na Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano Jimbo la Njombe,Pd. Innocent Chaula amesema
"Tumsifu Yesu Kristo!
Wapendwa, napenda kuwajulisha kuwa vyombo vitakatifu vilivyochukuliwa na
watu wasiojulikana kule Parokiani Wanging'ombe/Njombe vimepatikana
vyote leo 15.03.2021 asubuhi na mapema vikiwa vimewekwa ndani ya mfuko
mmoja (shangazi kaja) na kutelekezwa nje ya nyumba ya mkuu wa sekondari
ya Wanging'ombe"
Aidha amesema taratibu nyingine za kuvitakatifuza na kuvibariki upya zitafanyika kwa kuzingatia kanuni na sheria za Mama Kanisa.
Akizungumza na mwandishi wetu ili kuthibitisha tukio hilo amesema taarifa za awali waliweza kupokea kutoka kwa mkuu wa shule mara baada ya kufika nyumbani kwake na kuona mfuko huo.
"Vimepatikana nje ya nyumba ya mkuu wa shule wale wezi wamevitelekeza nje wakati mkuu wa shule hakuwepo na aliporudi ndipo akakutana na hilo fuko akatoa taarifa kwa walimu wenzake pamoja na polisi" Pd. Innocent Chaula amemweleza mwandishi wetu
Ikumbukwe vifaa hivyo viliibwa na watu wasiojulikana kwa kupitia dirishani (kwa kulivunja) na kuiba vitu mbali mbali vinavyotumika kwa ajili ya maadhimisho ya misa takatifu.
Taarifa iliyokuwa imetolewa na katibu huyo ilieleza kuwa tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Jumanne 09 Machi 202.
Alisema vifaa vilivyokuwa vimeibwa ni pamoja na.
1. Custodium yenye Ekaristi ya Mwonyesho ndani.
2. Monstrance
3. Kalisi (4)
4. Ciboria (3)
5. Patena (1)
6. Chombo cha kuwekea ubani (1)
7. Surplice (1)
Ambapo vyombo hivyo hutumika kwa ajili ya maadhimisho ya Misa Takatifu na Ibada za Kuabudu Ekaristi Takatifu.
Aliongeza kuwa wezi hao walichagua vitu vyenye rangi ya dhahabu tu, vile vilivyokuwa na rangi ya shaba vimeachwa.
Alisema walifungua Tabernakulo na kuchukua ciborium yenye Ekaristi Takatifu. Ekaristi Takatifu waliimwaga kwenye meza ya sakrastia na wao wakaondoka na Ciborium.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...