Wadau wa Haki Jinai Mkoani Katavi wamehimizwa kushirikiana katika kuhakikisha mifumo ya upatikanaji wa haki inaimarishwa ili kuwasaidia wananchi hasa wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

 

Hayo yamebainika wakati wa ziara ya Makatibu Wakuu wa Wizara za Afya- Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu na Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome mkoani Katavi  yenye lengo la kushirikiana kuhakikisha mifumo ya utoaji haki katika mashauri ya makosa ya jinai inaimarishwa.

 

Makatibu Wakuu hao wakizungumza kwa nyakati tofauti na watendaji wa Polisi na Mahakama Mkoani Katavi wamesema mifumo hiyo ikiwemo madawati ya jinsia, upatanishi, adhabu mbadala na huduma ya mkono kwa mkono (One Stop Center) ikiimarishwa zitasaidia kuharakisha utoaji wa haki kwa wakati.

 

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara za Afya- Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu amesisitiza kuimarishwa kwa madawati ya jinsia ya polisi kwani yanasaida sana watu wanaofanyiwa ukatili wa kijinsia na kuwa na mifumo imara ya kuwashughulikia wanaotenda makosa hayo, hasa ukatili dhidi ya watoto kwa sababu ndiyo waathirika wakubwa

 

 "Haya madawati yanabidi yaimarishwe ni muhumu sana katika kuhakikisha wanaotendewa vitendo vya ukatili wanapata huduma stahiki na watuhumiwa kuchukuliwa hatua za Kisheria” alisema Dkt. Jingu.

 

Aidha Dkt. Jingu ameendelea kusisitiza Maafisa Ustawi wa Jamii kuwepo katika kesi zinazohusisha watoto ili kuwalinda na kuhakikisha haki zao zinapatikana kwa kukosekana kwao kunasababisha watoto wengi kukosa haki zao katika kesi za Ukatili wa kijinsia.

 

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria  Profesa Sifuni Mchome mesisitiza kuwa kesi za Ukatili wa hasa dhidi ya watoto na wanawake zifuatiliwe kwa umakini kwa kuzingatia kuwa vitendo hivyo vina madhara makubwa katika jamii.

 

Aidha amewataka watendaji kutumia adhabu mbadala kama za kupatanisha kulingana na kesi husika katika kijamii ili kusaidia kupunguza msongamano wa kesi na mahabusu magerezani.

 

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa Janeth Musaroche akieleza mafanikio ya mifumo ya utoaji Haki Mkoa wa Katavi amesema kuwa mojawapo ya mafanikio waliyoyapata ni kuanzishwa kwa Sheria ya kutoa adhabu mbadala inayosaidia kuwapunguzia mzigo wa kuwa na mahabusu wengi katika magereza.

 

Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi ACP Benjamin Kuzaga amewaleza Makatibu Wakuu hao namna wanavyoboresha mifumo ya utoaji haki ikiwemo kujenga zahanati itakayotumika kwa huduma za mkono kwa mkono inayosaidia kutoa huduma kwa wahanga wanafanyiwa vitendo vya ukatili.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu (kushoto) akifafanua jambo kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi ACP Benjamini Kuzaga kuhusu zahanati iliyojengwa na Polisi pamoja na wadau wengine ili kurahisisha huduma za mkono kwa mkono (One Stop Center). Katikati ni Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome.

 

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora Dkt. Laurence Ndumbaro akizungumza katika kikao na baadhi ya watumishi wa Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi (hawapo pichani) katika ziara ya pamoja ya Makatibu Wakuu waWizara ya Katiba na Sheria  Prof. Sifuni Mchome( kulia) na Katibu Mkuu wa Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu.

 

Makatibu Wakuu wa Wizara ya Afya- Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu (kulia) na Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome wakiwasili na kupokelewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mhe. Janeth Musaroche katika Mahakama ya Mkoa Katavi katika ziara yao yenye lengo la kushirikiana kuhakikisha mifumo ya utoaji haki katika mashauri ya makosa ya jinai inaimarishwa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...