Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umeendesha Kongamano la Tafakuri ya Siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu kwa ajili ya kujadili vipaumbele, mafanikio, changamoto na kutoa mapendekezo ya namna ya kusonga mbele katika kuwaletea maendeleo wananchi na kila kundi katika jamii linanufaika na rasilimali za taifa.
Kongamano hilo lililoandaliwa na TGNP limefanyika leo Jumatano Juni 30,2021 katika
ukumbi wa TGNP Mabibo jijini Dar es salaam na kukutanisha pamoja wawakilishi wa
asasi za kiraia, taasisi za elimu ya juu,wadau wa maendeleo, wanachama wa TGNP,
vituo vya taarifa na maarifa na wanaharakati wa masuala ya jinsia, demokrasia
na maendeleo.
Akifungua Kongamano hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP,
Lilian Liundi amesema linalenga kutafakari kwa pamoja katika muktadha wa
vipaumbele vya serikali ya awamu ya sita, utekelezaji wake na mwelekeo wake na
kupendekeza maeneo yanayotakiwa kutiliwa mkazo zaidi.
“Juni 26,2021 Rais Samia ametimiza siku 100 akiongoza taifa
la Tanzania akiwa ni Rais wa Kwanza mwanamke. Imekuwa ni ada ya TGNP na wadau
kufakanya tafakari pindi serikali mpya inapofikisha siku 100. Tulianza na
Hayati Mhe. Benjamin Mkapa, tukaja kwa Mhe. Jakaya Kikwete,kasha Hayati Dkt.
John Pombe Magufuli na sasa ni Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan, hakika kila zama
na kitabu chake”,amesema Liundi.
“Mwaka 2021 ni mwaka wa kipekee pia kwani ni mwaka wa
kwanza wa utekelezaji wa mpango wa tatu wa maendeleo ya nchi yetu ambao ni
mpango wa mwisho katika kutekeleza Dira yetu ya Maendeleo ambayo inaisha 2025.
Lakini pia serikali imeanza kupitisha bajeti ya kwanza ya mpango huu ambapo
bajeti hiyo inaweka misingi ya utekelezaji wa mpango wa miaka mitano wa tatu”,ameongeza.
“Kipekee tumefurahishwa na Mhe. Rais Samia kwa kuonesha
bayana tunu za kuongoza taifa ambazo zimejumuisha masuala ya haki, demokrasia
na usawa. Tumeona juhudi kubwa za
kuongeza kasi katika kuleta usawa wa kijinsia kwa kuongeza wanawake katika
nafasi za uongozi kwa kuzingatia vigezo na sifa stahiki. Tumpe ushirikiano ili kuudhihirisha ulimwengu kuwa mwanamke ana kitu cha ziada katika masuala ya uongozi",ameeleza Liundi.
"Tumeona juhudi kubwa za kuongeza kasi katika kuleta usawa wa kijinsia kwa kuongeza wanawake katika nafasi za uongozi na kuongeza tija katika kuingiza masuala ya kijinsia katika sera,bajeti,mipango na michakato yote ya maendeleo. Hii itasaidia kuongeza kasi ya maendeleo jumuishi na endelevu nchini",amesema.
Aidha amesema TGNP pamoja na wadau wataendelea kufanya kazi na serikali ya awamu ya sita kwa njia mbalimbali na kufuatilia na kutoa chambuzi na ushauri mbalimbali.
"Mama yetu Mpendwa Mhe. Samia Suluhu katika siku hizi 100 ametupa mwanga, sisi tuwe kama
jicho lake la tatu katika kumsaidia, amefanya mambo makubwa katika siku hizi
siku 100, zimegusa vipaumbele vyetu muhimu.
Miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa na wadau kwenye kongamano hilo ni pamoja na masuala ya kijinsia yapewe kipaumbele, Rasilimali zilizotengwa na serikali na zifuatiliwe, kuwe na bajeti zenye mrengo wa kijinsia ili bajeti ifaidishe makundi mbalimbali, serikali ifanye utafiti kuhusu hasara gani taifa linapata kutokana na ukatili wa kijinsia.
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi akizungumza wakati akifungua Kongamano la Tafakuri ya Siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu kwa ajili ya kujadili vipaumbele, mafanikio, changamoto na kutoa mapendekezo ya namna ya kusonga mbele leo Jumatano Juni 30,2021 katika ukumbi wa TGNP Mabibo jijini Dar es salaam
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...