Na Fredy Mgunda,Iringa.
NAIBU waziri wa viwanda na biashara Exaud Kigahe amevitaka viwanda vinavyozalisha nguzo za umeme kuhakikisha wanazalisha nguzo zenye ubora unaotakiwa ili kuiondolea serikali hasara ya kununua nguzo hizo mara kwa mara.
Akizungumza wakati wa ziara aliyoifanya kwenye kiwanda cha kuzalisha nguzo za umeme cha Sao Hill kilichopo wilayani Mufindi, Kigahe alisema kuwa kumekuwa na baadhi ya viwanda ambavyo vimekuwa havizalishi nguzo zenye ubora na kuipatia hasara serikali.
Alisema kwenye uzalishaji wa nguzo kumekuwa na baadhi ya wazalishaji wa nguzo ambao hawaweki vizuri dawa ya kutibia nguzo na kusababisha kuharibika kwa nguzo haraka sana tofauti na makadilio ya serikali ya nguzo moja kuishi kwa zaidi ya miaka hamsini.
“Unakuta nguzo imekaa miaka mitatu tu imeharibika na inaanguka kutokana na kuzalishwa chini ya kiwango kutoka katika kiwanda ambacho kimezalisha nguzo na hasara hiyo inaenda moja kwa moja kwa serikali na sio kwao”alisema Kigahe
Kigahe alisema kuwa TBS wanapaswa kuanza kufuatilia ubora wa nguzo zinazozalishwa kwenye viwanda ambavyo sio waadilifu katika kuzalisha nguzo hizo za umeme ambao zimekua zikiharibika mara kwa mara.
Aidha Kigae aliwataka wanunuzi wa nguzo kutoka kwa wakulima wa bidhaa hiyo kuhakikisha wananunua kwa bei inayotakiwa na kuacha mara moja tabia ya kuwanyonya wakulima wa nguzo hizo.
Alisisitiza kuwa serikali inapaswa kununua nguzo za umeme ambazo zinakidhi viwango vya TBS ili kuepukana na kupata harasa ambayo wamekuwa wanaipata pasipokuwa na sababu ya msingi.
Naibu waziri wa viwanda na biashara Exaud Kigahe aliwaponge viongozi wa kiwanda cha Sao Hill kwa kuzalisha nguzo zenye ubora unaotakiwa ambapo nguzo zao zinauwezo kwa kukaa ardhini kwa zaidi ya miaka hamsini.
Kwa upande wake mwenyekiti wa wazalishaji wa nguzo nyanda za juu kusini Negro Sanga alisema kuwa kumekuwa na unyonyaji kwa baadhi ya kampuni kwa kununua nguzo kwa gharama ndogo na kuiuzia serikali kwa gharama kubwa nguzo hizo.
Alisema kuwa kila kampuni imekuwa na bei yake inayojiamulia kiasi kwamba inakuwa inawanyonya wakulima wa nguzo hizo zinapoka shambani hadi kufika kiwandani.
Naye meneja wa kiwanda cha Sao Hill George Bottger alisema kuwa lengo la kiwanda hicho ni kuhakikisha wanazalisha nguzo zilizo bora na zenye viwango vinavyotakiwa kimataifa kwa lengo la kuiondolea hasra serikali ambayo imekuwa inaipata kutoka katika viwanda vingine.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...