Raisa Said, Lushoto
MKUU wa Wilaya ya Lushoto Mkoa wa Tanga Kalisti Lazaro amewashauri Wakazi wa Wilaya hiyo kujitokeza kwa wingi kuhesabiwa wakati mchakato wa Sensa ya Watu na Makazi utakapoanza mwaka 2022.
Akizungumza Wakati wa ziara yake ya kata kwa kata ambayo ameambatana na Mbunge wa Jimbo la Lushoto Shaban Shekelindi maarufu Bosnia ,Lazaro amesema suala la kuhesabiwa ni muhimu sababu Serikali haiwezi kutengeneza mipango ya maendeleo kwa wananchi wake bila kuwa na takwimu sahihi za wakazi wa eneo husika.
Amefafanua lengo la sensa hiyo ni kuisadia Serikali kupata taarifa za msingi zitakazosaidia mchakato wa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025, mageuzi ya masuala ya afya na jamii, pamoja na ufuatiliaji wa ajenda za maendeleo za kimataifa.
Amesisitiza kuwa taarifa za idadi ya watu husaidia katika mamlaka za wilaya katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ambayo huakisi matakwa ya watu katika ngazi husika na kusaidia kwenye uwiano wa mgawanyo wa rasilimali
"Takwimu sahihi za Sensa zinahitajika kwa ajili ya ugawaji wa majimbo ya uchaguzi kwa ufanisi, kurekebisha mipaka ya kiutawala katika serikali za mitaa," ameeleza Lazaro
Katika hatua nyingine Mkuu wa Wilaya huyo amesema kama wilaya wamejipanga kuendelea kuihamasisha jamii kwenye mikutano ya hadhara na Vikao kwenye ngazi ya Wilaya, Kata, Vijiji na Vitongoji ambapo ajenda ya Sensa inatakiwa kuwa ya Kudumu.
Amesema kuwa wilaya itatumia vipeperushi na mabango pamoja na kutumia taasisi zilizopo kama shule na vyuo kutoa elimu kwa wanafunzi.Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepanga kufanya Sensa ya Watu na Makazi ifikapo mwezi Agosti 2022.
Amefafanua Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar (OCGS), ipo kwenye maandalizi ya kufanya Sensa hiyo.
Sensa ya Watu na Makazi ni zoezi la kitaifa linalofanyika kila baada ya miaka 10 ambapo Sensa ya mwisho kufanyika nchini ni ile ya mwaka 2012.
Hivyo Sensa ya mwaka 2022 itakuwa ni sensa ya Sita kufanyika nchini baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964. Sensa nyingine zilifanyika mwaka 1967, 1978, 1988, 2002 na 20.
Kwa Upande wake Mbunge wa Jimbo hilo , Shaban Shekelindi ameahidi kushirikiana na Mkuu wa Wilaya huyo lengo kuhakikisha wanahamasisha suala zima la sensa ili muda utakapofika wananchi wajitokeze kwa wingi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...