Na Mwandishi Wetu

Viongozi wa kiimani waliopo kanda ya ziwa katika mikoa ya Kagera, Mwanza na Mara wanaounda jukwaa la kiimani kanda ya ziwa wamependekeza sheria zinazohusika na kulisimamia baraza la kata zirekebishwe ili kuruhusu mabadiliko ikiwemo kuondolewa kwa jukumu la kufanya maamuzi badala yake liishie kuwa chombo cha usuluhishi.

Pendekezo hilo limesomwa na Mwenyekiti Mwenza wa Jukwaa hili Sheikh Haruna Kichwabuta ambaye ni shekh wa Mkoa wa Kagera alipokuwa anasoma taarifa iliyoandaliwa na Jukwaa hilo kwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe, William Lukuvi walipokutana nae na kufanya mazungumzo katika ofisi za Wizara ya Ardhi zilizopo Mtumba Jijini Dodoma tarehe 03 Novemba mwaka huu.

Jukwaa La Kiimani Kanda ya Ziwa baada ya kujadiliana limebainisha changamoto mbalimbali zinazosababishwa na mabaraza haya ya kata ambayo ni pamoja na miingiliano ya kimamlaka katika maamuzi, uelewa duni wa wajumbe juu ya masuala ya kisheria, upendeleo, ukata, rushwa, siasa, sintofahamu juu ya usimamizi na uwajibikaji pamoja na ukosefu wa ulinganifu wa kijinsia kwa wajumbe.

“Sheria ya mabaraza ya kata inataja wajumbe wasiwe wanasheria na pia wajumbe hawatakiwi kuwa watu wenye elimu kubwa wakati wanashughulikia maswala ya kisheria yenye kuhitajiwatu wenye ufahamu wa kutosha kuzitafsiri sheria hizo na hivyo kupelekea makosa yanayosababisha watu kupoeza haki zao” Alisema Shekh Kichwabuta.

Kwa upande wake Askofu Abednego Keshomshahara wa Kanisa la kiinjili la kilutheri Tanzania Jimbo la Kaskazini Magharibi Bukoba alisema wamelazimika kujadili changamoto hizi kwani hadi hivi sasa braza la kata linasimamiwa na mamlaka tofautitofauti na hivyo kupelekea hali ya kutoeleweka nani ni msimamizi na pia anayepaswa kuwajibika kwani katika maswala ya jinai baraza linasimamiwa na mahakama ya mwanzo ila kwenye migogoro ya ardhi mabaraza yamekuwa yakisimamiwa na mabaraza ya ardhi na nyumba ya wilaya.

Akipokea taarifa ya mapendekezo ya Jukwaa hilo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi amesema changamoto hiyo serikali inaitambua na tayari muundo unaandaliwa utakaowawezesha Wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya kuajiriwa kwa masharti ya kudumu mara baada ya kukamilika kwa miongozo na taratibu za Utumishi wa Umma.

Aidha Mhe. Lukuvi aliongeza kuwa hatua hiyo inatokana na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufanya marekebisho ya Sheria ambayo ilikuwa inaelekeza Wenyeviti hao kuajiriwa kwa mkataba wa miaka mitatu.

‘‘Marekebisho hayo yalifanyika ili kuondoa changamoto za mlundikano wa mashauri katika Mabaraza ya Ardhi wakati wa kusubiri Mwenyekiti mwingine ateuliwe, na hayo mambo ya rushwa yamejitokeza zaidi pale ambapo mwenyekiti hana uhakika wa kubaki katika nafasi yake mara muda wake unapokwisha’’ alisema Mhe. Lukuvi.

Akielezea katika mtazamo wa kisheria baada ya kupokea taarifa hiyo, Mkurugenzi wa Kitengo cha sheria Wizara ya Ardhi Michael Luena alisema ile dhana ya wajumbe kutokuwa wanasheria ilitokana na kwamba wale walikuwa wanashauri kutokana na mila na desturi za eneo husika, ila kutokana na kuendelea kukua kwa jamii, zimeibuka hoja ambazo zinahitaji utaalamu wa sheria ambazo ni muhimu kuingizwa katika maboresho ya kisheria kwani yapo upande wa kisheria.

Akiwashukuru wawakilishi wa Jukwaa la kiimani Kanda ya Ziwa waliofika wizarani, Msajili wa Mabaraza ya ardhi Stella Chaggi alisema baada ya kupata ujio wa jukwaa hili wizara ililazimika kuwaalika na wadau wengine kutoka Wizara Sheria ya Katiba na Tamisemi katika kuhakikisha makubaliano haya yanafanyiwa kazi katika sekta zote husika.

 Jukwaa hili limeundwa kwa ajili ya kuzishughulikia changamoto zilizopo kwenye jamii kwa kuzijadili pamoja na kutoa mapendekezo kwa Serikali. Kikao hiko kilihudhuriwa pia na wawakilishi kutoka TAMISEMI pamoja na Wizara ya Katiba na Sheria ambapo Viongozi hao wa Jukwaa la Kiimani Kanda ya Ziwa waliwakabidhi taarifa yao iliyoonyosha changamoto na mapendekezo, yote hayo ikiwa ni jitihada za kuboresha utendaji kazi hasa katika ngazi ya Mabaraza ya Kata

Mhe. William Lukuvi akipokea taarifa ya changamoto na mapendekezo katika Mabaraza ya Kata kutoka kwa Mwenyekiti Mwenza Jukwaa la Kiimani Kanda ya Ziwa Sheikh Haruna Kichwa

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Jukwaa la Kiimani Kanda ya Ziwa, baadhi ya viongozi wa Wizara Ardhi pamoja na wawakilishi kutoka TAMISEMI na Wizara ya Sheria na Katiba

Askofu Dkt. Abednego Keshomshahara wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Jimbo la Kaskazini – Magharibi Bukoba akiwasilisha mapendekezo ya Jukwaa la Kiimani Kanda ya Ziwa katika kuboresha utendaji kazi wa Mabaraza ya Kata mbele ya Mhe. William Lukuvi 

Mhe. William Lukuvi akimsikiliza kwa makini Mwenyekiti Mwenza Jukwaa la Kiimani Kanda ya Ziwa Sheikh Haruna Kichwa akitoa ufafanuzi juu ya utendaji kazi wa Jukwaa hilo 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...