Na Amiri Kilagalila,Njombe
Ujenzi wa barabara ya zege kilomita hamsini ya Lusitu- Mawengi wilayani Ludewa mkoani Njombe umefikia 86% kwa kukamilisha zaidi ya KM 45 ambapo mradi huo unatarajiwa kukabidhiwa mwezi agosti mwaka huu.
Wakazi wa wilaya hiyo wamesema barabara hiyo imewarahisishia kusafiri na kusafirisha mazao yao kwani kwa msimu wa mvua kama huu walikuwa wakitumia zaidi ya siku moja kutoka wilayani ludewa hadi mjini Njombe tofauti na sasa ambapo wanatumia saa tatu hadi nne tu na kuipongeza serikali pamoja na wakala wa barabara Tanzania TANROADS
Lenato Wila ni mwenyekiti wa kijiji cha Mawengi na Aneth Paulo mkazi wa kijiji hicho ambao wanaeleza namna walivyovumilia kwa miaka mingi hadi sasa wamepata barabara hiyo.
“Barabara hii ilikuwa haipitiki kabisa,tangu tulipopata uhuru na nauli ilikuwa kubwa sana kwenye vyombo vya usafiri lakini kwa kilomita ambazo imefikia sasa hivi kweli wananchi wameanza kupata matunda ya uhuru”alisema Lenato Wila
Aneth Paulo alisema “Kuna wakati mwingine utakuta mnakwama huko milimani na kuweza kulala pale pale lakini kwa sasa tunafika Njombe siku moja kwa kweli tunaishukuru serikali na TANROADS kwa kusimamia ujenzi wa barabara hii
Kwa mujibu wa Antony Mtewele ambaye ni dereva wa mabasi kutoka Ludewa kuelekea mjini Njombe na Elizai Nage ambao ni wakazi wa Ludewa wanasema ujenzi wa barabara hiyo umechukua zaidi ya miaka miwili hali ambayo ilichelewesha huduma lakini wanayofuraha kubwa kwa sasa kuona ujenzi unakamilika.
Wasimamizi wa mradi huu ni wakala wa barabara TANROADS mkoa wa Njombe ambao meneja wake Lucy Shalua anasema zimebaki kimomita tano pekee ili mradi ukamilike, huku wakitarajia kukabidhiwa mwezi agosti mwaka huu.
“Mpaka katika mradi huu mkandarasi ameshajenga jumla ya KM za zege kwa hiyo ina maana mradi huu umefikia asilimia themanini na sita”alisema Lucy Shalua
Mhandisi mshauri wa mradi amesema atahakikisha mkandarasi Cheon Kwang atakamilisha mradi kwa wakati.
“Tutahakikisha tunasukuma mradi huu ili uweze kukamilika mwishoni mwa mwezi wa nane”
Hali iliyopo sasa ni kuhakikisha mradi huu unakamika mwisho wa mwezi agosti ambapo mbunge wa jimbo la Ludewa Joseph Kamonga ameishukuru serikali kwa kuwahisha malipo ya mkandarasi hali inayoongeza kasi ya ujenzi.
“Na tunaomba serikali pia iendelee kumlipa mkandarasi kwa wakati ili asiwe na visingizio kwa kuwa mpaka sasa kwa kweli kasi ya ulipaji ni nzuri”alisema Kamonga.
Lucy Shalua meneja wa TANROADS mkoa wa Njombe akieleza maendeleo ya mradi wa barabara huku akibainisha kuwa wataendelea kuongeza nguvu za usimamizi ili kukamilisha bara bara hiyo kwa wakati.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...