Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeipongeza Serikali kwa kupitia Mamlaka ya Viwanja vya ndege Tanzanai (TAA), kwa kukamilisha mradi wa ujenzi wa uzio katika kiwanja cha ndege cha Mwanza ili kuongeza usalama wa kiwanja hicho.

Akizungumza jijini Mwanza mara baada ya kukagua mradi huo ambao umejengwa na Kampuni ya M/s Mumangi Trans & Construction, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ,Mhe. Selemani Kakoso, amesema kukamilika kwa hatua hiyo kutapunguza matukio ya ajali ambazo zimekuwa zikiripotiwa kiwanjani hapo.

“Niipongeze sana Serikali kwa kutoa fedha na kukamilisha mradi huu, maana kulikuwa na matukio ya ajali za wanyama na binadamu na nina imani kwa sasa hatutasikia tena matukio ya ajali", amesema Mwenyekiti Kakoso.

Mwenyekiti Kakoso ameitaka TAA kuhakikisha inaweka mipaka katika maeneo ya viwanja vyao vyote nchini na kuvitafutia mapema hati miliki ili kuepuka uvamizi na kupunguza migogoro kwa wananchi kwenye maeneo ya viwanja vya ndege.

“TAA mna maeneo makubwa sana kwenye viwanja lakini havina hati miliki mfano Sumbawanga, Mtwara, Songea na maeneo mengine na wananchi wanasogea taratibu msipokaa sawa mtajikuta mnapelekwa mahakamani na kiwanja ni cha kwenu", amefafanua Mwenyekiti Kakoso.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi), Atupele Mwakibete, amesema Serikali imejipanga kutekeleza miradi ya maboresho kwa kiwanja cha ndege cha Mwanza ili kuupa hadhi uwanja huo kulingana na taratibu za usafiri wa anga.

Naye, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Hamisi Amiri, amesema ujenzi wa uzio kwa sasa umekamilika kwa asilimia mia moja na umegharimu takribani bilioni mbili.

Mkurugenzi Amiri ameongeza kuwa ujenzi wa uzio umezingatia viwango vya sasa vya Shirika la Usafiri wa Anga Duniani (ICAO), ili kuendana na hadhi na kiwanja hicho.

(Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi)



Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Seleman Kakoso akitoa maelekezo kwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Uchukuzi), Atupele Mwakibete (mwenye koti la mistari) na Mamlaka ya Viwanja vha Ndege Tanzania (TAA), wakati kamati hiyo ilipotembelea mradi wa Ujenzi wa Uzio katika Kiwanja cha Ndege cha Mwanza.



Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Uchukuzi), Atupele Mwakibete akitoa ufafanuzi kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Seleman Kakoso pamoja na wajumbe, kuhusu mipango ya Serikali kwa Kiwanja cha Ndege cha Mwanza, wakati kamati hiyo ilipotembelea mradi wa Ujenzi wa Uzio katika Kiwanja cha Ndege cha Mwanza.



Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Seleman Kakoso akiangalia uzio uliowekwa katika Kiwanja cha Ndege cha Mwanza, wakati yeye na Kamati yake walipotembelea kiwanja hicho jijini.



Muonekano wa sehemu ya uzio wa kiwanja cha Ndege Mwanza ukiwa umekamilika kwa asilimia mia moja. Mradi huo umegharimu takribani bilioni mbili na kukamilika kwake kutapunguza matukio ya ajali kiwajani hapo.




Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Seleman Kakoso akitoa maelekezo kwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Uchukuzi), Atupele Mwakibete (kulia) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Hamisi Amiri (kulia kwa Mwenyekiti) wakati kamati hiyo ilipotembelea mradi wa Ujenzi wa Uzio katika Kiwanja cha Ndege cha Mwanza.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...