Na. Damian Kunambi, Njombe


Mkuu wa Wilaya ya Ludewa Andrea Tsere amewaagiza Viongozi wote wa ngazi ya kata na vijiji kutoa elimu kwa wafugaji wa ng'ombe juu ya zoezi la uvishaji hereni kwa mifugo hiyo ili kuweza kutambua idadi yao katika wilaya hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mkuu huyo ameongeza kuwa hereni hizo zitasaidia kujua afya ya mifugo,uhitaji wa maeneo ya malisho na kupunguza migogoro ya wakulima na wafugaji hivyo amewataka wafugaji kuonyesha ushirikiano wao ili kufanikisha zoezi hilo.

Amesema katika zoezi hilo kwa asilimia kubwa limegharamiwa na serikali hivyo kwa upande wa wafugaji watapaswa kugharamia hereni ambayo gharama yake haipungui shilingi 1500.

"Wafugaji mnapaswa kuunga mkono zoezi hili kwakuwa lina faida kubwa sana kwenu, kwani changamoto nyingi zinazohusiana na mifugo zitakwenda kumalizika", Amesema Tsere.

Ameongeza kuwa endapo ng'ombe atavaa hereni atakuwa ameunganishwa katika mfumo wa computer ambao utawezesha kujua afya yake, eneo alilopo na hata ikitokea anaibiwa inakuwa rahisi kupatikana.

Sanjari na hilo pia amewataka wafugaji wa ng'ombe kufugia mifugo yao kwenye mazizi badala ya kuwaacha milimani wakijichunga wenyewe kitu ambacho huleta uharibifu wa miundombinu ya barabara, maji na mfugaji hupoteza mavuno mengi yanayotokana na ng'ombe.

Amesema mifugo hiyo inapokuwa peke yake porini inakosa uangalizi wa karibu hasa wanapokuwa na watoto (Ndama) kwani ndama hao hupoteza maisha kwa kutumbukia katika mitaro na magonjwa mbalimbali.

"Kuacha ng'ombe porini tunapoteza mazao ya mifugo yetu, mbolea na hata maziwa ambayo tungeweza kuyatumia kwa afya ya binadamu tunayaacha yananyonywa na sungura huko maporini", Amesema Tsere.


 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...