Na Amiri Kilagalila,Njombe

Mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Njombe Kuluthum Sadick amewaagiza wakuu wa shule za sekondari za serikali  kwenye halmashauri hiyo kuhakikisha wanajenga misingi bora ya elimu kwa wanafunzi wao tangu wanapoingia kidato cha kwanza ili wanapomaliza masomo yao wafaulu kiwango cha daraja la kwanza na la pili pekee.

Agizo hilo amelitoa wakati akikabidhi zawadi kwa walimu wa shule ya sekondari ya  Uwemba iliyopo katika halmashauri ya mji Njombe baada ya kufanikiwa kufuta alama sifuri katika mtihani wa taifa wa kidato cha nne uliofanyika mwaka jana nchini kote.

Amesema katika kipindi hiki ambacho yeye ni mkurugenzi wa halmashauri hiyo hataki kuona mwanafunzi anakosa ufaulu wa daraja la kwanza na la pili kwenye mitihani yao ya taifa katika shule zote za sekondari za halmashauri hiyo.

Amesema endapo wanafunzi wataelezwa na kujengewa uwezo tangu awali wanapojiunga na kidato cha kwanza basi wataweza kufanya vizuri kwenye mitihani yao.

"Mkiwaambia watoto toka mwanzo wanajiunga kidato cha kwanza mpaka kufikia kidato cha watakuwa wamezoea kuwa shule inayotakiwa ni ufaulu wa daraja la kwanza na la pili"alisema Kuluthum.

Aliwapongeza walimu wa shule hiyo kwa kuhakikisha wanafuta ufaulu wa alama sifuri katika mtihani wa kidato cha nne mwaka na kuwataka kuweka nguvu zaidi ili kufuta ufaulu wa daraja la nne na la tatu.

Afisa elimu taaluma sekondari wa halmashauri ya mji wa Njombe Huruma Chaula alisema shule ya sekondari Uwemba ni miongoni mwa shule mbili za serikali zilizopo kwenye halmashauri hiyo ambazo zimefanikiwa kufuta sifuri kwenye matokeo ya kidato cha nne katika mtihani wa mwaka jana.

Alisema shule nyingine iliyofanikiwa kufuta alama sifuri kwenye mtihani wa kidato cha nne katika halmashauri hiyo ni shule ya sekondari Matola ambayo pia ni serikali.

Alisema kuna mkakati uliowekwa na halmashauri hiyo wa kuhakikisha kila shule inakuwa na wanafunzi wasiopungua watano ambao wanafaulu kwa daraja la kwanza kwenye mtihani wa taifa wa kidato cha nne ambapo shule ya sekondari Uwemba imefanikiwa katika hilo.

"Matokeo haya na hafla hii imeandaliwa makusudi na sisi kama idara tumeipokea kwasababu imekidhi vigezo kwa isingekuwa hivyo hata sisi tusingekuja hapa" alisema Huruma.

Mkuu wa shule ya sekondari Uwemba Alex Chengula alisema wanafunzi wa kidato cha nne ambao walihitimu masomo yao hapo mwaka jana walikuwa 162 huku wavulana wakiwa 70 na wasichana 92.

Amesema matokeo ya wanafunzi hao kwenye mtihani huo daraja la kwanza walikuwa wanafunzi 5, daraja la pili wanafunzi 13, daraja la tatu 28 na daraja la nne wanafunzi 116.

Amesema katika matokeo ya kidato cha sita kwa mtihani wa taifa hapo mwaka jana daraja la kwanza walikuwa wanafunzi 43, daraja la pili 63, daraja la tatu 12 na hakukuwa na wanafunzi waliopata daraja la nne.

"Tumepanga mikakati mbalimbali ambayo itatufanya tuendelee kufanya vizuri zaidi ya matokeo haya ambayo tunapongezana leo na mikakati hiyo ni kutoa mitihani mingi iwezekanavyo katika madarasa ya mitihani ya taifa kwa kufuata muundo wa baraza la mitihani la taifa" alisema Chengula.

Diwani wa kata ya Uwemba Jactan Mtewele aliwashukuru walimu wa shule hiyo pamoja na wazazi wa wanafunzi kwa ushirikiano wao katika kuhakikisha wanatokomeza ufaulu wa daraja sifuri kwenye shule hiyo.

Aliwataka wanafunzi,wazazi na walimu kuendelea kujenga mahusiano mazuri ili shule hiyo iendelee fanya vizuri katika mitihani ya taifa.

" Tumejitahidi sana kuwa na mahusiano mazuri ndiyo maana leo tumefika hapa lakini pia jambo lingine ni uwepo wa  nidhamu baina yetu sote" alisema Mtewele


 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...