Na Said Mwishehe, Zanzibar

KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Shaka Hamdu Shaka amesema Chama hicho hakijawahi kuogopa mfumo wowote wa kimageuzi iwe katika siasa, kiuchumi au kijamii.

Ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza kwenye Kituo cha Redio cha Zenj FM Mjini Zanzibar ambapo alifika kwenye kituo hicho ikiwa sehemu ya kutembelea vyombo mbalimbali vya habari vilivyopo visiwani hapa baada ya kufanya ziara kama hizo Tanzania Bara.

Akiwa katika kituo hicho cha redio pamoja na kuelezea sababu za kufanya ziara hiyo, mmoja ya watangazaji alitaka kufahamu iwapo CCM ina hofu yoyote wa kimageuzi iwapo mchakato wa Katiba mpya utafanyika na kupatikana.

Akijibu swali hilo, Shaka ameeleza Chama Cha Mapinduzi hakijawahi kuogopa mfumo wowote wa kimageuzi na hawaogopi kwasababu wanajiamiani kwani mpaka leo bado wamekubaki kuwa ndio tegemeo la Watanzania.

“Na hivyo vya ambavyo mnavizungumza sisi ndio ambao tunafanya kazi ya kuvilea na tunafanya kazi hiyo ili viweze kutukurupusha kidogo na viweze kuishi na kama isingekuwa malezi mazuri ya CCM basi leo kwenye ramani ya vyama vya siasa visingekuwepo.

“Kikubwa ambacho nataka kuhimiza hapa ni uvumilivu wa kisiasa , umoja na mshikamano. Nilitegemea mngeuliza kuhusu maridhiano ambayo tunakwenda nayo,”amesema Shaka.

Akielezea kuhusu maridhiano amesema wanakwenda vizuri na tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano na Mwenyekiti wa CCM Taifa Samia Suluhu Hassan baada ya kuingia madarakani alikutana na makundi mbalimbali.

Shaka amesema miongoni mwa makundi ambayo amekutana nayo ni pamoja na kundi la wanasiasa ambalo ndilo limekuja kuibua maridhiano ya kisiasa , hivyo alikutana na a na viongozi wa Chadema , ACT Wazalendo, CUF.

“Na atakutana na viongozi wa vyama vingine vyote ili kuleta ustawi wa maendeleo tukiwa tumeridhiana na tukiwa tunavumiliana kuweza kufanya siasa zetu, kwa hiyo tulikotoka ni kuzuri tuliko ni kuzuri zaidi na tunakokwenda ni kuzuri na muelekeo ni mzuri sana,”amesema Shaka.

Kuhusu ziara yake kwenye kituo hicho cha redio Shaka amesema Chama Cha Mapinduzi kimeona kina kila sababu ya kuhakikisha kinaendelea kuimarisha mahusiano mazuri kati yake na vyombo vya habari nchini, na ili kujenga mahusiano hayo ameamua kufanya ziara hiyo.

Ametumia nafasi hiyo kutoa shukrani zake za dhati kwa uongozi wa Zenji FM kwa mchango wake mkubwa kwa CCM lakini kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Redio yenu imekuwa ikizungumza na kuhamasisha masuala ya maendeleo katika serikali zote mbili, na kwa CCM tunatambua mchango wa redio hii na tutaendelea kuuenzi na kuuheshimu, tumekuja hapa kuwahakikisha kwamba Chama kipo pamoja nanyi na kwenye changamoto tushirikishane kutafuta ufumbuzi,”amesema Shaka.

Pamoja na mambo mengine Shaka aliomba wafanyakazi wa redio hiyo pamoja na msafara wake kusimama kwa dakika moja kwa ajili ya kumuombea dua aliyekuwa Mkurugenzi na Mwanzilishi wa kituo hicho Mohamed Seif Hatibu ambaye kwa sasa ni marehemu.

Shaka amesema sababu za kufanya kumuombea ni kutokana na kuenzi na kukumbuka mchango wake katika harakati za mapinduzi ya kuanzisha redio binafsi katika visiwa vya Zanzibar.

 








Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...