MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Mhe. Profesa Ibrahim Lipumba amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) huku makamu wake akiwa ni mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, Mhe. Haji Ambar Khamis.
Uchaguzi huo umefanyika leo Julai 3, 2023 katika mkutano mkuu wa TCD uliokuwa na ajenda mbalimbali ikiwemo ya uchaguzi wa mwenyekiti mpya ambapo wajumbe kutoka vyama vya Chadema, ACT Wazalendo, CUF, CCM, NCCR Mageuzi na CHAUMMA wakishiriki.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji - TCD, Bernadetha Kafuko imesema kuwa Profesa Lipumba amepokea kijiti kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) – Tanzania Bara, Mhe. Abdulrahman Kinana. Viongozi hao watatumikia uongozi wa TCD kwa kipindi cha mwaka mmoja, kwa mujibu wa Katiba ya TCD.
Akizungumza baada ya kuchaguliwa, Mhe. Profesa Lipumba amesema vipaumbele vyake katika mwaka mmoja wa uenyekiti wake ni kuongeza ushirikiano na maridhiano ndani ya vyama vya siasa na pia kujenga asasi za kidemokrasia. Pia, mchakato wa kupata katiba uendelee.
“Matumaini yetu ni kwamba kazi nzuri ambayo Mheshimiwa Kinana ameifanya, sisi tutaiendeleza na tuweze kuwa na kongamano zuri ambalo tunatarajia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan atakuwa mgeni rasmi. Kongamano hilo ni jambo ambalo tunaendelea kuwasiliana.” Amesema.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...