Na. Majid Abdulkarim, Mbarali


Wananchi wa Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwasogezea huduma za upasuaji wa mtoto wa jicho karibu na kuwaondolea tatizo la upofu.

Hayo yamebainishwa na mmoja wa wagonjwa ambaye amefanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho Bi. Sabina Sent (65) kupitia kambi ya siku saba ya Madaktari Bingwa wa upasuaji wa macho Wilayani humo chini ya ufadhili wa Shirika la Kimataifa la Helen Killer.

“Namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia matibabu ya macho bila malipo, nimekuja nikiwa sioni lakini sasa naweza kuona vizuri macho yangu yote”, ameeleza Bi. Sabina.

Bi. Sabina amesema kuwa amekuwa haoni kwa muda wa miaka miwili lakini baada ya kufika katika Hospitali ya Wilaya ya Mbarali na kufanyiwa uchunguzi kisha upasuaji anarudi kwake akiwa na tabasamu la kuona.

Kwa upande wake Mzee Richard Enock (59) amesema ameishi na tatizo la kutokuona kwa miaka 18 lakini leo baada ya kufanyiwa upasuaji na madaktari bingwa wa macho bila malipo anaweza kuona vizuri.

Mzee Enock ameeleza kuwa tatizo la kutokuona lilimuanza toka mwaka 2005 ambapo lilianza jicho moja na kila siku nguvu ya kuona ikawa inapungua mpaka macho yote yakawa hayaoni tena.

“Namshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kutujali sisi wananchi kwa kutusogezea huduma za macho karibu na sisi maana sikuwa na uwezo wa kusafiri kufata huduma hizi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya”, amesema Mzee Enock

Naye Mtoto wa mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho, Nassoro Atupele amesema kuwa amefarijika sana kuona baba yake anaona kwani amekuwa haoni tangu mwaka 2014 ndo alipata tatizo la mtoto wa jicho na kuacha kuona kabisa.

“Nitoe wito kwa shukrani zangu za dhati kwa Serikali yetu, pia naomba huduma hizi ziwe ni endelevu kwani sio kila Mtanzania ataweza kusafiri kufika Hospitali zinazotoa huduma hizi za upasuaji kama zilivyotufata hapa Mbarali”, amesisitiza Atupele

Aidha, kambi hiyo ya Madaktari Bingwa wa Macho mpaka sasa imefanya upasuaji wa mtoto wa jicho kwa watu 150 na ilianza Jumatatu ya Agosti 14 na inatarajia kumalizika Agosti 20 mwaka huu.






 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...