*Imo ujenzi wa miundombinu ya barabara, bandari na ndege ya mizigo

Na Said Mwishehe, Michuzi TV

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan ametaja hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kutafuta masoko ya uhakika kwa ajili ya mazao ya wakulima nchini.

Ametaja hatua hizo leo Septemba 7,2023 wakati wa mkutano wa Jukwaa la Mfumo wa Chakula Afrika (AGRF) ambapo ametumia nafasi hiyo kuelezea hatua ambazo Serikali inachukua kuondoa changamoto ya masoko.

“Kuhusu masoko kuna shida katika kupatikana masoko lakini katika tafiti ambazo tumefanya tumegundua kuna mambo mawili ambayo yana utata na tunayafanyia kazi

“Jambo la kwanza ni Connection kwanza kujua mahitaji na balansi , balansi gani inatakiwa wapi ndani na nje ya nchi ,tukijua hilo tutakuwa na usahihi wa kinachozalishwa upande mmoja kiende upande mwingine,”amesema.

Ameongeza jambo la pili ni Connectio ya mkulima na soko lenyewe na kwamba eneo hilo hawajafanya  vizuri bado huku akifafanua wameanza katika baadhi ya mazao kwa mfano korosho.

“Tumeshuhudia mara kadhaa bei ya korosho ikipanda kwasababu kuna ushirika wa mkulima na mnunuaji moja kwa moja, hivyo tumemuondoa mtu wa kati amba walikuwa wanakwenda moja kwa moja kununua mazao shambani na wananunua kwa bei ndogo.

“Tulivyounganisha mkulima na mnunuzi pamoja na soko wanunuaji wananunua kwenye vyama vya ushirika vya wakulima na kwa maana hiyo wanapata muda wa kushindana bei na bei zinapanda.

“Tumeshuhudia hivi karibuni zao la ufuta kwasababu tumeingiza kwenye ushirika na tumetumia mfumo wa stakabadhi ghalani, wakulima wanapeleka mazao yao huko kwenye ushirika , wanunuaji wanashindanishwa bei inapanda,”amesema Rais Samia.

Ameongeza la kufurahisha zaidi ni katika zao la mbaazi ambalo miaka miwili, mitatu nyuma walihamasisha wakulima walime sana na wakalima lakini kwasababu hawakuwaunganisha na soko na hawakuwa na mipango mizuri mbaazi zilianguka bei sana na kuwavunja moyo wakulima

“Mwaka jana (2022) mbaazi iliuzwa kwa Sh.300 kwa kilo lakini mwaka huu(2023) wakulima wameuza kwa zaidi ya Sh.2000 kwa kilo. Sasa huu ndio mtindo tutakaokwenda nao kwenye mazao mengine pia ili kumuunganisha mkulima na soko,”amesema.

Pia amesema hatua nyingine wanayochukua amesema soko linahusu usafiri na usafiri ndio unaleta soko , hivyo Serikali imejidhatiti kujenga barabara kwa kuunganisha mikoa na mikoa , mikoa na wilaya zake lakini barabara kubwa na nchi jirani ili kufanikisha masoko ya nchi hizo.

 “Katika  barabara mwaka jana na mwaka huu tumetoa fedha nyingi sana kutengeneza barabara za ndani ya wilaya ili mazao yasikwame kwa wakulima yaende kwenye masoko

“Sio barabara peke yake tunatengeneza bandari zetu Tanzania , bandari ya Dar es Saalam, Zanzibar ,Tanga na Mtwara , zote ziweze kupokea meli zinazoweza kushusha na kuchukua mazao yetu yanayozalishwa kwenda nje na tumefanikiwa vizuri

“Pia kama mnavyoelewa tumenunua ndege ya mizigo ili isafirishe mazao hasa mazao ya matunda ambayo yanakaa kwa muda ambapo kwa ndege ile sasa tunaweza kuchukua mizigo yetu wenyewe na kuipeleka kwenye soko kuliko kutegemea kwa jirani apakie apeleke.

“Kwani hatujui wakati wa kupakia pengine mazao yale yale yameandikwa yametoka kwa jirani wakati yametoka Tanzania.Kwahiyo sasa ndege yetu itaweza kutusafirisha mazao yetu,”amesema.

Aidha amesema katika bandari wanajenga sehemu itakayoweza kuhifadhi mazao yanayoharibika kwa haraka yaweze kuhifadhiwa wakati yanasubiri usafiri.“Kwa hiyo tunachukua hatua zote hizi ili kumfikisha mkulima, kufikisha mazao kwenye soko.”

Pia amesema jambo lingine kubwa ambalo wanafanya hasa katika mpango wa  BBT ni kutafuta na kufanya ushirika na watu ambao watakuwa wakiongeza thamani mazao ya vijana.

“Kwa maana vijana wakilima na wakivuna kuwe na mtu anayechukua mazao yote na kuyapeleka kuyaongeza thamani kwenye viwanda vyetu yakiwa yamechakatwa. Kwahiyo hizo ndizo hatua ambazo serikali inazichukua kuimarisha soko.”









Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...