Na Janeth Raphael- Michuzitv Dodoma

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imefanikisha kukamilika kwa Mradi wa UVIKO 19 katika kijiji cha Ibihwa, Lamaiti vilivyopo kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Bahi na Mradi kufikisha umeme kwenye Kituo cha afya ulipo katika kijiji cha Makolongo, Halmashauri ya wilaya ya Chemba, Miradi yote ina thamani ya zaidi ya shilingi milioni 900.

Mkurugenzi wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA); Mhandisi, Francis Songela amesema Serikali kupitia REA imewezesha na kufanikisha kukamilika kwa Mradi wa Kupeleka Umeme kwenye pampu za maji na Vituo vya Afya kwa lengo la kukabiliana na magonjwa ya milipuko, ugonjwa wa UVIKO 19 ukiwa ni mmoja wapo.

Mhandisi, Songela ameyasema hayo wakati wa ziara ya Wajumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) walipotembelea na kukagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa UVIKO 19 katika wilaya ya Bahi na Chemba, leo Tarehe 9 Septemba, 2023 ambaye aliambatana na Mkurugenzi wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Bwana Oswald Urassa pamoja na Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi, Mhandisi Jones Olotu.

Mhandisi Songela amesema, utekelezaji wa Mradi wa UVIKO 19 kwa mkoa wa Dodoma, unataraji kukamilika mwisho wa Mwezi Septemba, 2023 na kupongeza namna Mkandarasi (Kampuni ya DIEYNEM Ltd) ilivyofanikisha ujenzi wa miundombinu ya umeme kwenda kwenye visima vya maji katika kijiji cha Ibihwa, Lamaiti (Wilaya ya Bahi) na miundombinu ya umeme kwenda kwenye Kituo cha Afya katika kijiji cha Makolongo (Wilaya ya Chemba).

Mhandisi Songela amesema upatikanaji wa huduma ya maji na afya ni vitu vya muhimu na ndiyo maana Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) iliona ipo haja ya kuja na Miradi ambayo italenga kwenye kurahisisha upatikanaji wa nishati ya uhakika ili kuchochea upatikanaji wa maji ya uhakika pamoja na huduma ya afya.

“Mradi wa UVIKO 19 uliandaliwa mahsusi kwa ajili ya kuboresha afya ya Mwanamchi, kwa maana ya apata maji ya uhakika lakini pia zahanati ziwe na huduma nzuri ili kuchangia katika kupunguza magonjwa mbali mbali ya milipuko, ukiwemo UVIKO 19” alisema, Mhandisi Songela.


Mhandisi, Songera ameongeza kuwa Mradi wa UVIKO 19 unaenda kuleta mabadiliko makubwa katika maisha ya watu kwa kuwa zaidi ya vitongoji 26 katika vijiji viwili vya (Ibihwa na Lamaiti) Wananchi wake wanaenda kunufaika na huduma ya maji ya uhakika.

Wakati huo huo; Mhandisi Songela ametoa wito kwa Viongozi wa Serikali za vijijini vya Ibihwa, Lamaiti na Makolongo kuwahamasisha Wananchi ili wachangamkie fursa ya uwepo wa umeme wa uhakika ili kuunganishwa na huduma hiyo ya umeme kabla Mkandarasi hajaondoka kwenye eneo la Mradi.












Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...