Na Mwandishi Wetu

TAASISI ya Social Action Trust Fund (SATF) iliyoanzishwa kwa udhamini wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Serikali ya Marekani (USAID) na kuratibiwa na Serikali ya Tanzania limekabidhi vifaa kwaajili ya ujasiriamali kwa vijana 13 katika Kijiji cha Picha ya Ndege wilayani Mkuranga mkoani Pwani.
Lengo la taasisi hiyo ni kusaidia juhudi za Serikali katika kutoa huduma kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu waweze kuzifikia ndoto zao na vijana hao 13 ni kati ya vijana 50 walioshiriki mafunzo ya ujasiriamali ikiwamo ushonaji na utengezaji wa mabegi kwa msaada wa SATF kwa kushirikiana na SIDO Pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga.

Akizungumza leo wakati wa kukabidhi vifaa hivyo kwa vijana hao,  Meneja Miradi wa SATF Nelson Rutabanzibwa amesema waliokabidhiwa vifaa ni pamoja na mhitimu mmoja wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Masasi aliyehitimu mafunzo ya upishi na usimamizi wa hoteli.

Amesema SATF ina mpango wa kuwasaidia vijana kwa kuwapatia masomo ya kukuza ujuzi wao kwa kushirikana na wadau mbalimbali.
 
Ameongeza kwamba mwaka jana waliwasaidia vijana 50 kutoka Mkuranga ambao walishiriki mafunzo ya ujasiliamali, ufundi wa ushonaji nguo na utengenezaji mabegi kwa miezi sita pale SIDO Dar es salaam kati yao waliofanikiwa kumaliza ni 45, ambapo miongoni mwao ni hao 13 waliokabidhiwa vifaa hivyo.

Kwa mujibu wa Rutabanzibwa, taasisi  hiyo imekabidhi cherehani za kisasa zinazotumia umeme na vifaa vingine kwaajili ya ujasiliamali wa upishi na kwamba wataendelea kuwakabidhi vifa wengine kadri wanavyopata maeneo ya kufanyia shughuli zao.

Amesema wao wanawawezesha kwa kuwapatia elimu ya kuwaongezea ujuzi, kwahiyo jamii pia inatakiwa kuunga mkono juhudi hizo kwa kuwapatia maeneo ya kufanyia shughuli zao.

"Ndio maana nikasema hao waliosalia wakipata maeneo pia tutawapa vifaa ili waweze kujiingizia kipato kama tulivyofanya leo kwa wenzao,"amesema Rutabanzibwa na kuongeza kuwa taasisi hiyo itaendelea na jitihada zake za kusadia jamii kupitia miradi yake mbalimbali ili kufikia malengo yake.

Wakizungunza kwa nyakati tofauti Zulfa Shabani na Abdallah Amad, miongoni mwa wafaidika wa msaada huo walisema kuwa wana kila sababu ya kutimiza ndoto zao kutokana na walichopewa na SATF kuanzia kuwaongezea ujuzi hadi kukabidhiwa nyenzo za kuwaingizia kipato. 

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Shirika la Jipe Moyo Women and Community Organisation (JIMOWACO), Asha Antony, aliwataka vijana hao kutumia vyema vifaa hivyo ili viwasaidie kujipatia kipato kwaajili yao na familia zao, kutoa ajira na kuwafundisha wengine.

Mbali na kujiingizia kipato vifaa hivi ambavyo ni vya kisasa pia vitasaidia kuongeza pato katika taifa letu kwasababu mtakuwa mkilipa kodi, kwahiyo ni muhimu kuvitunza, alisema  Asha.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Picha ya Ndege, Abbas Shabani aliishukuru SATF huku akiwataka vijana kuwa na nidhamu pale wanapopata fursa za kuongeza ujuzi kutoka kwa wafadhili wanaojitokeza.

Wakati huo huo Mratibu wa Mashirika yasiyo ya kiserikali, NGOs, Wilaya ya Mkuranga, Timothy Kudra alisema kuwa, vijana hao wana haki ya kutumia fursa hiyo kuanzisha vikundi vya kijamii kwa kufuata taratibu.

"Wakati mnafurahia msaada huu kutoka SATF, fikirieni sasa kuanzisha vikundi vya kijamii. Hii itawasaidia sana kufanikisha shughuli zenu za kujiingizia kipato kwasababu tayari mtakuwa na kikundi kinachotambulika kisheria kwahiyo mnaweza kupata wafadhili mbalimbali na hata tenda," amesema Kudra.

Aidha kiongozi huyo aliidhihirishia SATF kuwa, Serikali iko tayari kutoa ushirikiano wa aina yoyote, pale utakapohitajika msaada kwa taasisi yoyote katika Wilaya ya Mkuranga na milango iko wazi. 

"Hawa vijana mliowasaidia leo tumewapokea na tutawaboreshea mazingira ili wafaidike na walichokipata."

Msajili wa NGOs Wilaya ya Mkuranga Timothy Kudra (kulia) akikabidhi msaada huo kwa mmoja wa vijana ambao wamepatiwa vifaa hivyo



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...