MBUNGE wa Kiteto mkoani Manyara, Edward Ole Lekaita Kisau ameishukuru serikali, kwa kuwapatia fedha nyingi na kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo.
Miradi iliyotembelewa na mwenge wa uhuru mwaka 2023 Kiteto, ni pamoja na kufungua madarasa mawili na ofisi Shule ya Msingi Esukuta na Daraja Orkine.
Pia mwenge huo ulifungua shule mpya ya msingi Azimio na kupanda miti 500 na kuzindua na utunzaji wa mazingira Shule ya Sekondari Nasa Matui na kuzindua klabu ya wapinga rushwa.
Vile vile ,uliweka jiwe la msingi ujenzi wa majengo matatu Hospital ya Wilaya ya Kiteto na kuzindua mradi wa maji wa RUWASA majengo mapya Kata ya Kaloleni.
Ole Lekaita aliyasema hayo jana wakati akizungumza kwenye mbio za mwenge wa uhuru wilayani Kiteto, wakati wa kukagua, kuzindua, kutembelea na kuweka jiwe la msingi, kwenye miradi ya maendeleo mbalimbali yenye thamani ya Sh.bilioni 2.4.
Ole Lekaita alisema kupitia miradi mbalimbali iliyotembelewa na mwenge Kiteto na mingine iliyopo wilayani humo, ambayo haijapitiwa na mwenge, wamepiga hatua kubwa ya maendeleo.
"Kwa niaba ya watu wa Jimbo la Kiteto tunaipongeza serikali kwa kutupatia fedha za maendeleo, zilizofanikisha miradi ya sekta ya elimu, afya, maji, miundombinu na mengine," alisema Ole Lekaita.
Hata hivyo, alisema wakazi wa Kiteto hawana cha kuilipa, ila wanaiombea ili izidi kushinda uchaguzi mkuu mwaka 2025.
Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru mwaka 2023, Abdalah Shaibu Kaim, alimpongeza mbunge wa Kiteto kwa kushiriki kwenye shughuli za mwenge ulipokuwa Kiteto.
"Mheshimiwa Mbunge Ole Lekaita nakupongeza sana kwa kushiriki ipasavyo kwenye mbio za mwenge kwa mwaka huu, wewe ni mzalendo mtu bingwa kabisa kwani umeonyesha ushirikiano mkubwa na viongozi wenzake wa Kiteto," alisema Kaim.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...