Na Issa Mwadangala.

Waumini wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Konde Jimbo la Magharibi Usharika wa Mpemba Mjini Tunduma wametakiwa kuachana na fikra hasi ambazo hupelekea kuongezeka kwa uhalifu katika jamii.

Akizungumza Februari 25, 2024 na waumini wa Kanisa hilo wakati wa ibada ya Jumapili, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi SACP THEOPISTA MALLYA amesema waumini wanapaswa kuwa na fikra na mitazamo chanya yenye kujenga jamii.

“Kitendo cha baadhi ya waumini kutofikiri kwa makini na kuwashirikisha watu wengine pindi wapatapo changamoto mbalimbali katika maisha hupelekea kufanya maamuzi mabaya yenye kuleta madhara katika jamii kama kujiua, kuiba, kudhulumu mali za wajane na yatima, na kufanya watoto wa mtaani kuongezeka katika jamii kitendo kinachopelekea watoto hao kufanyiwa ukatili wakiwa mitaani” alisema Kamanda Mallya

Sambamba na hayo Kamanda Mallya amewataka waumini kuwashirikisha viongozi wa dini pindi wanapopata changamoto mbalimbali ili wapatiwe ushauri wa kiroho ambao ni muhimu kwa kila muumini anapopitia nyakati hizo.

Nae Mchungaji wa Kanisa hilo NSUBHILEN NDENGAWA aliwataka waumini hao kujitokeza kwenye maeneo yao pindi waonapo au wafanyiwapo vitendo vya kihalifu na kikatili ambapo aliwasisitiza wakemee bila woga kwani kwa kufanya hivyo kutapunguza uhalifu na kuiacha jamii ikiwa salama.

Aidha alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuendelea kuyafikia makundi mbalimbali kwa kutoa elimu ili jamii iachane na ukatili pamoja na matendo ya kihalifu ambayo hayampendezi Mungu na kuzingatia mafundisho yaliyoandikwa katika Kitabu kitakatifu (Biblia) hasa makatazo kama Walawi 18:22, Warumi 1:24-29, Zaburi 15:5, Kutoka 23:8, Kumbukumbu la Torati 16:19 na Waefeso 4:26.

Pamoja na kushiriki katika ibada, SACP. Mallya hutumia nyumba za ibada kama sehemu ya kutoa elimu ambayo waumini huwajengea imani ya kiroho ili kutoshiriki na kuchukia aina yeyote ya uhalifu katika jamii.







 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...