Na WMJJWM- Dodoma

Wataalamu wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii na Kada nyingine kutoka ngazi ya Mikoa, Halmashauri na kata nchini wametakiwa kuhamasisha Jamii kuwa wazalendo, kujitolea na kuchangia katika shughuli za maendeleo katika maeneo yao ili kutatua changamoto zinazowakabili.

Hayo yamesemwa Mei 22, 2024 jijini Dodoma na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Patrick Golwike wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo Wataalam kutoka ngazi ya Mikoa na Halmashauri kuhusu utekelezaji wa Mpango wa kuhamasisha na kusimamia Maendeleo Ngazi ya Msingi wa mwaka 2022/23-2025/26.

Golwike amesema Serikali inatambua mchango wa Timu ya Wataalamu ngazi ya mkoa, wilaya na kata katika kutoa huduma kwenye nyanja mbalimbali kwa jamii kwa kuandaa mafunzo hayo yatakayowezesha Mpango huo kuwafikia wataalamu waliopo kwenye maeneo yao kwa haraka.

"Natoa rai, kuwa ujuzi mtakaoupata mkautoe kwa Wataalamu wa ngazi ya kata ambao ndiyo kiungo muhimu baina ya Wananchi na Serikali" amesema Golwike

Aidha, Golwike amewaagiza wataalamu hao kwa kila mkoa uandae na kuwasilisha mpango kazi wa utekelezaji wa Mpango kwa kuanza kutoa mafunzo ya Mpango kwa Wataalamu ngazi ya msingi kwani bila ya kuwa na mpango kazi wa utekelezaji ni upotezaji wa rasilimali fedha na muda, kuweka mpango wa utaratibu wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi Ngazi ya msingi badala ya kusubiri viongozi wa ngazi za juu na kujenga mazoea ya kufanya kazi kwa timu na kuwajibika ili kuwa na kazi zenye matokeo na tija.

Pia ameagiza timu za Wataalamu ngazi ya Wilaya na kata kuwezeshwa ili kuhakikisha wanafanya vikao vya kufuatilia utekelezaji wa Mpango na kufanya maboresho kwenye maeneo yanayohitaji marekebisho na kuandaa na kuwasilisha taarifa za utekelezaji.

Vilevile amesema matokeo ya kuhamasisha uzalendo kwa jamii yatafanya kuwa na Taifa linalopenda yao, jamii inayofanya kwa bidii na jamii inayojitolea katika shughuli za maendeleo katika maeneo yao.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Idara za Serikali za Mitaa kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Jeremiah Mwambange amesema muamko wa wananchi kujitokeza katika shughuli za maendeleo kwa takwimu zilizopo ni asilimia 5 tu hivyo jitahada zaidi zinahitajika katika kuhamasisha wananchi kujitolea na kushiriki katika shughuli za maendeleo.

"Suala la Mpango wa Taifa wa Kuhamasisha na Kusimamia Maendeleo Ngazi ya Msingi wa Mwaka 2022/23 - 2025/26 ni la muhimu sana katika maendeleo ya nchi yetu kwani litasaisia kuamsha arinya wananchi kujitolea katika shughuli mbalimbali za maendeleo katika maeneo yao" amesema Mwambange

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Jamii kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Neema Ndoboka amesema lengo la mafunzo hayo ni kutoa elimu kwa Maafisa wa Serikali waliopo katika ngazi za Halmashauri na Mikoa ili waweze kuhakikisha Mpango huo unatekelezwa kikamilifu katika maeneo yao.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...