VUNJO.

MBUNGE wa Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, Enock Koola ameendelea na ziara yake ya kuhamasisha kilimo cha kahawa katika jimbo hilo ambapo mamia ya wakulima wakijitokeza kushiriki na kupata elimu kuhusu mbinu bora za uzalishaji wa zao hilo la kimkakati.

Katika mwendelezo wa ziara hiyo, Mbunge pamoja na timu yake ilitembelea kata za Mwika Kaskazini na Mamba Kaskazini, akiambatana na Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Catherine Joachim pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Godfrey Mnzava kuhamasisha wakulima wa zao la kahawa.

Akizungumza na wananchi, Koola alisisitiza umuhimu wa kufufua na kuimarisha kilimo cha kahawa kama nguzo kuu ya uchumi wa wananchi wa Vunjo.

Alibainisha kuwa juhudi za pamoja kati ya serikali, viongozi wa kisiasa na wakulima ni msingi wa kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa kahawa, na kuhakikisha wakulima wanapata masoko yenye tija.

Kwa upande wake, Dkt. Catherin Joachim aliwahimiza wakulima kuchangamkia fursa zilizopo katika sekta ya kahawa kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu wa kilimo na kutumia mbinu za kisasa ili kuongeza tija na kipato.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mnzava, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kupitia vyama vya ushirika pamoja na matumizi sahihi ya pembejeo ili kuongeza ushindani wa kahawa ya Vunjo katika soko la ndani na kimataifa.

Wakulima wamepongeza jitihada za Mbunge kwa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha zao la kahawa linakuza uchumi wa kaya na maendeleo ya jamii katika eneo hili.





Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...