Na Mwandishi Wetu, Arusha
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Aprili 30, 2026, “amewapiga msasa” waongoza watalii zaidi ya 230 wa kozi ya sita katika mfululizo wa mafunzo kwa wataalamu hao kuwaongezea uwezo zaidi wa kuhudumia wageni katika semina inayoendelea jijini Arusha katika Ukumbi wa AIM Mall.
Dkt. Abbasi ametoa mada kuhusiana na Majukumu ya Waongoza Watalii katika Kulinda Chapa (Branding) ya Nchi iliyobeba anuani ya: “ National/ Destination Branding and the Role of Tour Guides.”
Katibu Mkuu huyo ambaye pia ni mtaalam wa masuala ya mawasiliano kwa umma, ametoa mfano wa mafanikio ya filamu ya “Tanzania: The Royal Tour” kuwa moja ya ushuhuda wa umuhimu wa nchi kuwekeza katika mikakati mikubwa ya kuiweka chapa yake katika ramani ya dunia.
“Sote hapa tutakiri kuwa Royal Tour ilifanikiwa sana na inabaki kuwa moja ya miradi yetu mikubwa kama Taifa ya kuitangaza Tanzania uliolipa sana. Nawahakikishieni tunakuja na mipango zaidi ya kuipeleka chapa ya Tanzania kimataifa zaidi,” alisema.
Amewapa mifano mbalimbali waongoza watalii hao jinsi nchi nyingi duniani zinavyowekeza katika kusambaza habari nzuri na vivutio vyao vya utalii zaidi badala ya kulalamika au kuainisha changamoto zaidi.
“Kuna nadharia (theory) katika mawasiliano kwa umma inasema mtu akilitangaza jambo sana na kulirudiarudia (agenda setting) hata kama ni la uongo litaanza kuaminika.
Sisi ni mabalozi wa utalii basi tukayaoneshe na kuyasema mazuri ya vivutio vyetu badala ya kuposti vitu vidogo vidogo vyenye changamoto,” alisema akionesha mifano ya baadhi ya nchi zinavyotumia nguvu kubwa kutangaza vivutio vyao japo ni vichache na haviizidi Tanzania.
Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Chama cha Wamiliki wa Kampuni za Utalii Tanzania(TATO) na yanafanyika kwa awamu (batches) kadhaa zenye washiriki zaidi ya 250 kila moja na lengo ni kuwafikia waongoza watalii zaidi ya 2,500 ikiwa ni maandalizi ya msimu mpya wa utalii lakini na matukio makubwa kama Afcon 2027.
Kwa mujibu wa takwimu za Benki Kuu ya Tanzania, watalii wa kimataifa nchini wameongezeka kutoka 922,000 mwaka 2021 kabla ya Royal Tour na kufikia 2,294,000 mwaka jana huku mapato ya jumla ya sekta ya utalii yakifikia Dola Bilioni 4.4 kutoka Bilioni 1.3 mwaka 2021 kabla ya Royal Tour.




.jpeg)

.jpeg)


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...