Na Pamela Mollel,Arusha 

Arusha inatarajia kuandika historia mpya kupitia Tamasha kubwa la Sanaa na Kazi za Ufundi litakalofanyika Oktoba 2026, tukio linalolenga kuipa nguvu sekta ya utalii na sanaa pamoja na kukuza uchumi na ubunifu nchini Tanzania

Tamasha hilo linaandaliwa na Tanzania International Tourism Festival (TITF) kwa kushirikiana na Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TASFA), likiwa limebeba dhamira ya kuwaunganisha wasanii, wabunifu na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha, Mkurugenzi wa TITF, Ibrahim Jamal, amesema lengo kuu la tamasha hilo ni kuinua thamani ya kazi za ubunifu na kuzifanya ziwe na ushindani katika masoko ya kimataifa kupitia sekta ya utalii

Amefafanua kuwa tamasha hilo litakuwa jukwaa muhimu litakalowakutanisha wachongaji, wachoraji, wabunifu wa mavazi, watengenezaji wa vito, wafinyanzi na wasanii wa kazi za mikono kutoka maeneo mbalimbali nchini Tanzania

Mbali na maonesho ya sanaa, washiriki watapata fursa ya mafunzo maalum yatakayojikita katika uongezaji thamani wa bidhaa, ulinzi wa haki miliki za kazi za ubunifu pamoja na mbinu za kufikia masoko ya ndani na nje ya nchi

Aidha, kutakuwa na maonyesho ya moja kwa moja ya utengenezaji wa kazi za sanaa (live demonstrations) pamoja na mikutano ya kibiashara (B2B) itakayowaunganisha wasanii na wanunuzi wakubwa pamoja na wawekezaji wa kimataifa

Kwa upande wake, Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TAFCA), Rukia Walele, amesema tamasha hilo linafungua ukurasa mpya kwa sekta ya sanaa za ufundi ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikichangia uchumi na kuhifadhi utamaduni wa Kitanzania

Ameongeza kuwa kupitia vyama zaidi ya 20 vinavyounda shirikisho hilo, maelfu ya wasanii nchini watapata nafasi ya kutambulika, kujifunza mbinu za kisasa za biashara na kujenga mitandao itakayowaingiza katika masoko ya kikanda na kimataifa

Aidha, amesema sanaa za ufundi ni nguzo muhimu ya uchumi wa ubunifu, hivyo tamasha hilo litasaidia kuongeza kipato kwa wasanii na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha sanaa na utalii barani Afrika

 Waandaaji wamesisitiza kuwa Arusha itakuwa kitovu cha ubunifu na utalii wakati wa tamasha hilo, ambalo linatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki na wageni kutoka mataifa mbalimbali, ikiwa ni chachu ya mageuzi ya kiuchumi kupitia sanaa na utamaduni.







Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...