Timu ya Ushirombo Warriors FC imetwaa ubingwa wa Wilaya ya Bukombe katika mashindano ya KNK CUP 2026, baada ya kuichapa Katome FC mabao 2-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa tarehe 7 Septemba 2026 katika Uwanja wa Bukombe Stadium uliopo Mtaa wa Kilimahewa, Kata ya Katente, Tarafa ya Ushirombo, Wilaya ya Bukombe mkoani Geita.

Ushirombo Warriors walionyesha kiwango kizuri na kutumia vyema nafasi walizopata. Bao la kwanza lilifungwa dakika ya 43 na mshambuliaji wao Hames Kigwangala kabla ya mapumziko.

Kama mabingwa, Ushirombo Warriors FC walikabidhiwa kombe, seti tatu za jezi, mipira mitatu pamoja na kitita cha shilingi milioni 5. Katome FC ambao walimaliza nafasi ya pili walikabidhiwa seti mbili za jezi, mipira miwili pamoja na shilingi milioni 3. Nafasi ya tatu ilichukuliwa na Msasa FC ambao walikabidhiwa seti moja ya jezi, mpira mmoja pamoja na shilingi milioni 1.

Zawadi hizo zilikabidhiwa na Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Paskasi Muragili, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita. Mashindano hayo yanafadhiliwa na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko.

Mratibu wa Kamati ya Mashindano ya KNK CUP 2026 Wilaya ya Bukombe, Bosco Mwidad, alisema mashindano hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwaibua vijana wenye vipaji vya soka. Alisema tangu mashindano hayo yalipoanza mwezi Julai mwaka huu, jumla ya timu 248 zilishiriki, huku zawadi zikitolewa kuanzia ngazi ya kata hadi tarafa.

Nahodha wa Ushirombo Warriors FC, Damas Buyenze, alieleza furaha yake baada ya timu hiyo kutwaa ubingwa wa Wilaya kwa mara ya kwanza. Alisema “Nina furaha sana pamoja na wachezaji wenzangu kwa kutwaa ubingwa wa Wilaya, kwani si jambo dogo. Tulijipa moyo, tukajituma na kumsikiliza mwalimu wa timu, na leo tumetwaa ubingwa. Pia namshukuru Mungu kwa kunisaidia kuwa golikipa bora”.

Wananchi wa Bukombe pamoja na wapenda michezo kwa ujumla wamemshukuru Dkt. Doto Mashaka Biteko kwa kuendelea kugharamia mashindano hayo ambayo yamekuwa chachu kubwa ya kukuza na kuibua vipaji vya watoto na vijana katika Wilaya hiyo.










Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...