Rais wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa, father Miguel d' Escoto Brockama akimwonyesha Mama Maria Nyerere, medali ya dhahabu ambayo rais huyo ameitengeneza maalum na kumtuza Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere. Mama Maria Nyerere alipokea Tuzo hiyo ya 'World Hero of Social Justice' kwa niaba ya Baba wa Taifa katika hafla iliyofanyika mwisho mwa wiki jijini New York, Marekani na kuhudhuriwa na mabalozi mbalimbali wa Afrika na mabara mengine wanaoziwakilisha nchi zao katika umoja wa mataifa, watoto wawili wa Baba wa taifa Bw. Andrew Nyerere na Bi. RoseMary Nyerere walihudhuria hafla hiyo, kushoto ni balozi wa tanzania katika umoja wa mataifa, Augustine Mahiga na kulia ni mwenyekiti wa kundi la nchi za Afrika balozi Mourad Benmehidi kutoka Algeria
Rais wa baraza kuu la 63 la Umoja wa mataifa, father Miguel d' Escoto Brockman, akitoa maelezo kwa Mama Maria Nyerere kuhutu tuzo ya 'World Hero of Social Justice' ambayo rais huyo ametunuku Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere katika hafla iliyofanyika jijini New York, Marekani na kuhudhuriwa na mabalozi mbalimal mbalimbali kutoka nchi za Afrika na mabara mengine wanaoziwakilisha nchi zao katika umoja wa mataifa

Mama Maria Nyerere akivishwa na Rais wa Baraza Kuu la 63 la Umoja wa Mataifa, Father Miguel d' Escoto Brockman kwa niaba ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere tuzo maalum ya ' World Hero of Social Justice' ambayo Rais huyo amemtunuku Baba wa Taifa kwa kutambua mchango wake katika kutetea na kupigania haki na usawa kwa watu wanyonge, hafla ya utoaji wa tuzo hiyo ilifanyika mwishoni mwa wiki Jiji New York, Marekani na kuhudhuriwa na mabalozi mbalimbali kutoka nchi za Afrika na mabara mengine wanaoziwakilisha nchi zao katika Umoja wa Mataifa. kushoto ni balozi wa tanzania katika umoja wa mataifa, Augustine Mahiga.
Baadhi ya wageni waalikwa wakiangalia picha zilizokuwa zikionyesha historia na matukio mbalimbali ya Baba wa Taifa enzi za uhai wake, picha hizo zilikuwa zimeandaliwa na Ubalozi wa Tanzania Umoja wa mataifa kwa kushirikiana na Maktaba ya Idara ya Habari Maelezo. Chini
Mama Maria hapa akiwa na watoto wake waliomsindikiza katika hafla hiyo, Andrew Nyerere na RoseMary Nyerere wengine katika picha hiyo ni Balozi Augustine Mahiga, Rais wa 63 wa Baraza kuu la Umoja wa mataifa Miguel d' Escoto Brockman na mwenyekiti wa Kundi la nchi za Afrika katika Umoja wa Mataifa Balozi wa Algeria
Mama Maria akiwa na baadhi ya Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao katika Umoja wa Mataifa walioshiriki hafla ya kukabidhiwa Tuzo kwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambayo ilipopekelewa na Mama Maria Nyerere tuzo hiyo ya ' World Hero of Socia Justice' imetolewa na Rais wa Baraza Kuu la 63 la Umoja wa Mataifa, Miguel d' Escoto Brockman
Mabalozi wa wanaoiwakilisha Tanzania nchini Marekani, Brazil na Umoja wa mataifa nao walikuwapo kumpa Tafu Mama katika hafla hiyo kutoka kulia Joram Biswalo (Brazil) Omben Sefue ( Washngton ) Tuvako Manongi ( ofisi ya Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa) na mwenyeji wao Augustine Mahiga (Umoja wa Mataifa) katika picha ya pamoja na Mama Maria Nyerere
Mama Maria Nyerere katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa. aliyekaa mbele na Mama Maria ni Balozi Augustine Mahiga
Mama Maria atoa somo Umoja wa Mataifa
 
Habari na picha kwa hisani ya
ubalozi wa Tanzania Umoja wa Mataifa

Ushauri umetolewa kwa Umoja wa Mataifa kuyatumia mawazo, ushauri na mapendekezo ambao umewahi kutolewa na viongozi mbalimbali duniani akiwamo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazoikabili dunia hivi sasa .
Mjane wa Baba wa Taifa Mama Maria Nyerere ametoa ushauri huo wakati akitosha shukrani zake baada ya kupokea Tuzo maalum ya Baba wa Taifa ijulikanayo kama ‘ World Hero of Justice’ pamoja na Medal ya dhahabu iliyotolewa na Rais wa Baraza kuu la 63 la Umoja wa Mataifa, Bw. Miguel d’ Escoto Brockman.
Hafla hiyo ilifanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano wa Umoja wa Afrika jijini New York na kuhudhuriwa na mabalozi mbalimbali wanaoziwakilisha nchi zao katika Umoja wa mataifa.
Kwa upande wa Tanzania, Mabalozi Augustine Mahiga (Umoja wa Mataifa) Ombeni Sefue ( Washangton) Joram Biswalo (Brazili ) na Tuvako Manongi kutoka Ofisi ya Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa walihudhiria hafla hiyo.
“ombi langu kwenu wageni waalikwa mliohudhuria hafla hii na Umoja wa Mataifa kwa ujumla ni kwamba mujaribu kuangalia ni kwa namna mnaweza kutumia ushauri mawazo na mapendekezo yaliyotolewa na viongozi waliotangulia na kuyatumia katika kuzikabili changamoto za dunia ya leo. Ninayo imani kubwa kwamba kama tukijaribu kuzingatia ushauri wao tunaweza kufanikiwa “ akasema Mama Maria.
Aidha Mjane huyo wa Baba wa Taifa, akabainisha zaidi katika hotuba yake hiyo iliyosomwa kwa niaba yake na mmoja wa watoto wake walioambatana naye katika hafla hiyo, Bi RoseMary Nyerere, kwamba Baba wa Taifa alikuwa miongoni mwa viongozi waliotoa kipaumbele kwa Umoja wa Mataifa.
Anasema Mama Maria “ Mwalimu Nyerere hakusita kuutumia umoja wa mataifa katika kusukuma ajenda mbalimbali alizoamini kwamba ni muhimu katika maendeleo na ustawi wa mwanadamu. Aliutumia umoja wa mataifa kupigania na kutetea haki za watu maskini na wanyonge, kupigania amani na usalama na kupinga ubeberu na ubaguzi”.
Akaongeza kwa kusema kwamba Baba wa Taifa aliamini kwamba umoja wa mataifa ulikuwa ndio jukwaa pekee linalowakutanisha kwa pamoja na kutoa fursa sawa kwa mataifa ya kujenga na kuwasilisha hoja na upigaji wa kura katika mambo mbalimbali bila ya kujali ikiwa taifa hilo ni dogo, kubwa, tajiri, maskini au lina nguvu kubwa kiasi gani.
“ pamoja na mwalimu kuamini katika usawa huo, kwa upande mwingine aliamini kwamba mataifa hayo hayakuwa sawa na hasa linapokuja suala la maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Ni kwa sababu hiyo hakusita kutamka bayana na kuyataka mataifa yaliyoendelea kuyasaidia mataifa maskini ili nayo yaweze kukabiliana na changomo mbalimbali” akasema Mama Maria.
Katika hotuba yake hiyo iliyowasisimua wageni waalikwa, Mama Maria ameeleza kuwa umoja na ushirikiano miongoni mwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa ni jambo la muhimu sana na hasa katika kipindi hiki.
Akizungumzia kuhusu mitizamo mbalimbali ya Baba wa Taifa kuhusu Bara la Afrika na hasa baada ya kumalizika kwa ukoloni na ubaguzi wa rangi. Mama Maria anasema, Mwalimu alihimiza waafrika kuungana ili kutafuta na kujipatia nguvu za kisiasa, nguvu za kiuchumi ili kujiletea maendeleo endelevu, amani na usalama.
Anaeleza kuwa Mwalimu aliamini kwamba Umoja wa Afrika ulikuwa na unabaki kuwa chombo pekee ambacho kitaziwezesha nchi za Afrika kuzikabilia changamamoto zinazolikabili bara hilo ambazo ni umaskini, magonjwa, ujinga na migogoro ya kisiasa.
“Miaka kumi baada ya kifo cha Mwalimu Nyerere, waafrika tunaendela na jitihada za kujenga msingi wa umoja na mshikamano ndani ya bara letu. Najua wako watakaokuja kutusaidia, lakini lazima tukumbuke kwamba maendeleo katika kila nchi moja moja yatatokana na jitihada za wananchi wenyewe na kama kila mmoja wetu atatimiza wajibu wake, kama alivyokuwa akisisitiza Baba wa Taifa kwamba inawezekana timiza wajibu wako”.
Akizungumzia Tuzo aliyopewa Baba wa Taifa, Mama Maria anasema Tuzo hiyo imetolewa katika wakati muafaka na ikiwa zimebaki wiki chache za maadhimisho ya miaka 10 tangu alipofariki Baba wa Taifa Octoba 14,1999.
Akasema kwa tuzo hiyo ni kielelezo kilichodhahiri cha kutambulikwa kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya Baba wa Taifa ya kupigania na kutetea haki, usawa na maendeleo ya mwanadamu. Na kwamba anashukuru kuwa bado wapo viongozi wanaozienzi na kuziendelea fikra za Baba wa taifa.
“Kwa niaba ya Baba wa Taifa, kwa niaba yangu mwenyewe , familia yangu, serikali yangu na watanzania wote, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa heshima hii kubwa uliyompatia Baba wa Taifa, Tanzania na Afrika kwa ujumla” akasisitiza Mama Maria.
Akatumia fursa hiyo kuishukuru serikali kwa kuendelea kumuenzi Baba wa Taifa na kwa kumuwezesha yeye na watoto wake Bw. Andrew Nyerere na Bi RoseMary Nyerere kuweza kuhudhuria hafla hiyo.
Rais huyo wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa, mmoja wa viongozi waliokuwa karibu sana na Baba wa taifa, akitoa tuzo hiyo anasema ameamua na baada ya kushauriana na viongozi mbalimbali kutoa tuzo hiyo kwa Baba wa Taifa kwa kuwa alikuwa kati ya viongozi wachache ambao sio tu walisimama kidete kutetea wanyonge na haki za binadamu bali pia walimvutia hata yeye kufuata nyayo zao za kupigania na kuwatetea wanyonge.
Akabainisha kwamba viongozi waliokuwa na fikra, misimamo na mitizamo kama ya Baba wa Taifa kwa sasa ni wachache sana na kwamba dunia inahitaji viongozi kama wa aina hiyo ya Baba wa Taifa.
Wasifu wa Baba wa Taifa ulisomwa na Padre Art Wille kutoka Shirika la Marknoll Order. Padre Wille aliyeishi Tanzania alimfahamu vema na kwa karibu sana Baba wa Taifa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 5 mpaka sasa

  1. hongera sana wanaoona umuhimu wa kuwasaidia wanyonge ili nao wajione kama sehemu ya mchakato wa dunia yetu. Katika azimio la Arusha ukiondoa neno Ujamaa misingi yake inatekelezeka hata sasa lakini wajanja wengi wao waliokuwa wanamzunguka Nyerere wakachomeka Azimio jingine la Zanzibar ambalo ndio linatusumbua leo na vita isiyopiganika ya Ufisadi!!katika azimio la Arusha ilisemwa wazi viongozi wasijilimbikie mali bali wawe watumishi wa umma leo watu ni mawaziri na wana makampuni yao sasa atajizuia vipi kupachika kampuni yake kwenye mlolongo wake wa shughuli za umma!!!?China imefanikiwa leo kuendesha ubepari pale Hongkong katikati ya Ujamaa(one country two systems) kwa vile bado ina-embrace MIIKO ya uongozi ukikosea tu unakula shaba.tuna mengi ya kujifunza kutoka huko kama tunataka kusimamia mgawanyo wa mali zetu chache kwa usawa..

    ReplyDelete
  2. hongera sana baraza kuu la umoja wa mataifa kwa kumuenzi mwalimu jk nyerere kwani mwalimu ni mmoja kati ya viongozi bora kabisa kuwahi kutokea barani afrika

    ReplyDelete
  3. Kuna siku mbeba box mwenzangu aliuliza kwanini serikali inabana hotuba za baba wa Taifa? Jibu halikupatikana.
    MAMA AMESISITIZA KUTUMIA MAWAZO,MAPENDEKEZO NA USHAURI WA WAZEE WA ZAMANI KWENYE KUENDELEZA DUNIA YA LEO, KWA MIMI HASA NCHI YETU YA TANZANIA ILIYOJAA UWOZO KWENYE KILA SEKTA YA SERIKALI MPAKA PCB YENYEWE MATOPE MATUPU.
    AU ZILE HOTUBA ZINAWAGUSA NDIYO MAANA WANABANA?
    KAKA MICHU TUNAOMBA UTUTAFUTIE UTATUZI WA HILI JAMBO MAANA HAWA JAMAA UNAKUTANA NAO SANA KWENYE KONA ZAKO EMBU TUULIZIE SIKU MOJA NDUGU YETU TUPATE JIBU ROHO ZETU ZITULIE TAFADHALI.

    MBEBA BOX UK

    ReplyDelete
  4. WAKATI HUO UKIUMWA MOJAKWAMOJA HOSIPITALI SIO SASA UNAJIKAZA KWA KUWA HUN A MIA 5 YA KUMUONA MGANGA, WAKATI HUO UNAINGIA MAKTABA BURE SIO SASA MPAKA ULIPIE UACHAMA. SHULE BURE VYUO VIKUU BURE.WAZUNGU WAKATUONEA GERE WAKA SEMA BURE MWISHO , SASA SHULE NI KUWA NAZO NA SIO KUCHARGE KWA AKILI ZAKO.NA WALIONAZO NI WALE WALE UTASIKIA MAJINA YALE YALE WATOTTO MPAKA VITUKUU WAKIJIVUNIA HIMAYA YAO. WAO NDIO WATAPATA AJIRA KIRAISI WENGINE KALAGA BAO. LAKINI HIKI KIZAZI CHA NYERERE KIKO KAMA CHA WALALAHOI WENGINE WAWAJIVUNII HILO JINA ILI WAPATE ULAJI WANAZIDISHA MAADILI YA BABA YAO.

    ReplyDelete
  5. Hii inadhirisha kwamba Mwl Nyerere alikuwa lulu ya Afrika na kwamba ni wachache wanauwezo kama wake,ni vizuri na sisi tukamuenzi kwa busara na fikra zake na ukweli utabaki palepale kwamba NYERERE WAS THE GREATEST.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...