Na Khadija Kalili, Michuzi TV
MKUU wa Mkoa wa Pwani Alhaji Abubakari Kunenge amesema kuwa maandalizi ya uzinduzi wa bandari kavu ,Kwala iliyopo Wilaya ya Kibaha utakaofanyika tarehe 31 ,2025 (kesho) umekamilika.

Akizungumza katika mkutano na Waandishi wa Habari leo tarehe 30 2025 uliofanyika Bandari Kavu Kwala Mkoani hapa amesema kuwa maandalizi yamekamilika kwa 95.

"Mgeni rasmi atakua Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan hivyo natoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Pwani pamoja na Mikoa jirani wajitokeze kwa wingi kwa sababu jambo hilo ni la kihistoria ndani na nje ya nchi" amesema RC Kunenge.

Kunenge ameongeza kwa kusema kuwa sambamba na uzinduzi wa bandari kavu pia Rais Dkt. Samia atazindua Kongani ya viwanda ya Kwala ambayo ona uwezo wa kuwa na viwanda 250.

"Eneo la Kwala ni sehemu ambayo serikali imefanya uwekezaji mkubwa ikiwa pamoja na ujenzi wa viwanda vikubwa 250 ambapo hadi sasa tayari viwanja saba tayari vimejengwa na vinafanya kazi.

"Bandari Kavu ya Kwala ina uwezo wa kuhudumia makasha 823 kwa siku na Makasha 30,000 kwa mwaka.

Kunenge amesema bandari kavu ya Kwala itaongeza ufanisi wa bandari ya Dar es Salaam ambapo kimsingi bandari imelenga kusaidia na kupunguza msongamano wa makasha katika bandari ya Dar es Salaam kwa asilimia 30.

RC Kunenge amesema kuwa Dkt. Rais Samia siku hiyo atazindua maeneo ya ujenzi wa bandari kavu kwa ajili ya nchi za DRC Kongo, Zambia, Burundi, Malawi, Zimbabwe na Uganda ambapo pia amesema kuwa nchi za Sudan na Somalia nao wameonesha nia ya kujenga bandari kavu katika eneo hilo.

Wakati huohuo Rais Dkt. Samia atapokea mabehewa 160 ya reli ya kati ambapo kati ya hayo mabehewa 20 yamekarabatiwa na mabehewa 100 yamenunuliwa mapya na serikali na mengine 40 yamekarabatiwa na Shirika la Chakula Duniani pamoja na Wakala wa Ushoroba wa Kati.

RC Kunenge amesema kuwa Rais Dkt.Samia ataweka jiwe la msingi kwenye Kongani ya Viwanda ya Kwala yenye viwanda 250 Kongani ambayo ni kubwa katika nchi yaKuhusu Bandari Kavu ya Kwala, Kunenge amesema mradi huo ,utaongeza ufanisi mkubwa kwa kuhudumia wastani wa makasha 823 kwa siku sawa na zaidi ya makasha 300,000 kwa mwaka hatua itakayopunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam kwa zaidi ya asilimia 30.

Aidha RC Kunenge amesema kuwa Rais Samia anatarajiwa kupokea jumla ya mabehewa 160 ambapo mabehewa 100 ni mapya yaliyonunuliwa na serikali kwa ajili ya reli ya SGR ,mabehewa 20 yamefanyiwa ukarabati na mabehewa 40 yametolewa na WFP.
Na Mwandishi Wetu, Mwanza
VIONGOZI wa klabu mbalimbali zinazoshiriki michezo ya Shirikisho la michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa Tanzania (SHIMIWI), wamepata mafunzo ya kuwajengea uwezo kuhusu afya michezoni yaliyotolewa na Daktari bingwa kutoka taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Rocky City Mall, Jijini Mwanza.

Dkt. Eva Wakuganda, ambaye pia yupo kitengo kinachohusiana na masuala ya afya za wachezaji kwa upande wa ugonjwa wa moyo, amesema ni muhimu kupima afya kabla ya kufanya mazoezi na michezo ya aina yeyote kwa watu wazima hata kwa wanafunzi mashuleni, ili kutambua matatizo waliyonayo.

“Tunafanya hivi kwa sababu sasa kumekuwa na matatizo ya watu wazima au Watoto kuanguka wakati wakiwa kwenye michezo au mazoezi ya muda mrefu kutokana na kutokujua hitilafu ya umeme wa mioyo yao au presha za mapafu yake ni kubwa au matundu yake kupitisha hewa ni madogo na labda ni tatizo alilozaliwa nalo na kukua nalo bila kujua, na hata kunakuwa na hitilafu hata kwenye misuli na mwanamichezo anaweza kuanguka ghafla na kuzimia au kufa bila kujua ana matatizo ya moyo wakati akiwa anafanya mazoezi kwa muda mrefu, hivyo ni muhimu kupima afya zao mara kwa mara, ili kujua afya zetu mapema, ” amesema Dkt. Wakuganda.

Dkt. Wakuganda amesema matatizo ya moyo yanaongoza Duniani kwa vifo takribani milioni 20 ya watu wa rika mbalimbali, ambapo kwa takwimu za utafiti wa Shirika la Afya Duniani (WHO) ya mwaka 2021 inaonesha takribani ugonjwa huu unashika nafasi ya juu katika 10 bora za magonjwa yasiyoambukiza, lakini huweza kuepukika kwa kufanya mazoezi kiasi, kuacha kuvuta sigara, kuacha unywaji wa pombe na kula mlo kamili.

Ametoa angalizo kwa watu wazima kufanya mazoezi angalau kwa dakika 30 hadi saa moja kwa siku, kwani zaidi ya hapo unaweza kusababisha kuongezeka kwa uzito, kumea kwa sukari mwilini, mafuta kuongezeka hadi kuziba mishipa ya damu kwenye moyo, ambapo mtu akifuata masharti ya mazoezi kunasaidia kuepuka madhara hayo na magonjwa mengine, ikiwemo hatari ya kuanguka na kupoteza maisha, ambapo takwimu za Waafrika kwa mujibu wa WHO zinaonesha kati ya wanamichezo 3,000 mmojawapo anahatari ya kuanguka, tofauti na Ulaya ni kati ya 25 mmojawapo anaathari hiyo.

Amesema mbali na mafunzo haya, pia Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete itatoa mafunzo zaidi kwa wanamichezo takribani 2000 watakaoshiriki kwenye michezo ya SHIMIWI inayotarajia kuanza tarehe 1-16, Septemba, 2025 kwenye viwanja mbalimbali Jijini Mwanza.

Mbali na SHIMIWI pia amesema taasisi hiyo sasa inatoa elimu ya afya kwa wanamichezo mbalimbali kwenye viwanja na maeneo yanayotumika kwa mazoezi, hususan viwanjani na gym.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa SHIMIWI, Bw. Alex Temba ameishukuru taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete kwa kutoa mafunzo haya kwa kuwa yatawasaidia watumishi wa umma wanapoanza mazoezi kuhakikisha wanapima afya zao, ili kuepusha madhara mbalimbali.

“Tunawakaribisha taasisi nyingine kipindi cha michezo yetu waje kutoa elimu kwa watumishi na wananchi wa Mwanza, ili ujumbe wao uweze kutufikia kwa wingi wetu, hii inasaidia serikali kwa kuwa huduma zinakuwa zimewafikia wananchi kwa haraka, hivyo rai yangu ni vyema kutambua athari za matatizo ya moyo mapema,” amesema Bw. Temba.

Naye Dkt. Richard Yomba ambaye anahusika na tiba ya michezo anayetokea Polisi amesema itambulike wazi kuwa kabla ya kufanya mazoezi au mashindano ya aina yeyote lazima mhusika akapime afya ili kutambua afya yake, kuanzia moyo na sehemu nyingine za mwili.

Dkt. Yomba ametoa ushauri kwa kuiomba taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete wawekeze elimu hii hususan kwa wanamichezo, ambao wengi wao ndio wanaoshiriki kwenye michezo mbalimbali nchini, vikiwemo vikundi vya mbio za jogging na marathoni.

“Hata mazoezi tunayofanya kwa kuangalia mikanda majumbani mwetu, au tukila chakula kwa masaa kadhaa kabla ya kwenda kwenye michezo au mazoezi au tukinywa vinywaji vya kuongeza nguvu navyo vyote vinaleta madhara kwenye moyo, hivyo tujitahidi kuhakikisha tunaepuka hayo,” amesema Dkt. Yomba.

Kwa upande wake Bi. Anna Zebedayo, mjumbe kutoka klabu ya Michezo ya mkoa wa Mwanza, amesema mafunzo hayo yawamewapa elimu itakayowasaidia wakati wanapokuwa michezoni na wachezaji wao, ambapo ameahidi kupeleka elimu hii kwa klabu yake.

“Tunaomba hawa madaktari wa taasisi ya Jakaya Kikwete waje mara kwa mara ili tuweze kupata elimu hii itayotusaidia kutambua namna mtu atakapoanguka akiwa michezoni au mazoezini anapewa huduma gani, na kujua madhara mengine mbalimbali,” amesema Bi. Anna.






KATIKA hali ya kuonyesha moyo wa kizalendo na kugusa maisha ya Watanzania wa kawaida, kampuni ya Meridianbet imeendelea kuthibitisha kuwa mafanikio ya kweli hayapimwi tu kwa faida ya kibiashara, bali pia kwa namna taasisi inavyorudisha thamani kwa jamii inayoiwezesha. Meridianbet imefanya tukio maalum lililoacha alama kubwa katika mioyo ya wasafishaji wa barabara ndani ya Manispaa ya Kinondoni kwa kuwapatia msaada wa vifaa muhimu vya kujikinga wakati wa kazi.

Tukio hilo lililofanyikia katika ofisi za Manispaa ya Kinondoni, limeambatana na utoaji wa vifaa kama vile glovu, barakoa, viatu maalum vya kazi (buti), pamoja na makoti yenye reflector kwa ajili ya kuongeza ulinzi na usalama wakati wa kazi za usafi. Wasafishaji hao, ambao mara nyingi huonekana kama kundi linalopuuzwa licha ya mchango wao mkubwa kwa jamii, wamepokea msaada huo kwa shukrani na furaha isiyoelezeka.

Akizungumza kwa niaba ya Meridianbet, muwakilishi wa kampuni hiyo ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya dhamira yao ya kuwa karibu na jamii, hasa kwa wale wanaohusika moja kwa moja na kuboresha mazingira ya mijini. “Kila siku wanahakikisha jiji letu linapendeza na linabaki salama kiafya, lakini mara nyingi hawapewi vifaa vya kutosha kujikinga. Leo tumeamua kuchukua hatua ndogo lakini yenye maana kubwa kwao.”

Kwa upande wake, mwakilishi kutoka Manispaa ya Kinondoni ameonesha kufurahishwa na msaada huo, akieleza kuwa ni nadra kuona kampuni binafsi zikielekeza macho yao kwa makundi kama haya. Amesema, “Kuna utofauti mkubwa kati ya kusema unajali jamii na kuonyesha kwa vitendo. Tunawapongeza Meridianbet kwa kuchukua jukumu hili kwa uzito unaostahili.”

Meridianbet imekuwa ikijijengea sifa ya kuwa kampuni inayojali zaidi ya michezo ya kubahatisha. Kupitia miradi yao ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), wamekuwa wakitekeleza misaada mbalimbali ikiwemo ya kielimu, huduma za afya, pamoja na kuwezesha vijana kupitia michezo na ajira mbadala. Hii ni sehemu ya dira yao ya kuhakikisha jamii zinazowazunguka zinakuwa na maendeleo endelevu.

Kwa mara nyingine, Meridianbet imeonyesha kuwa mafanikio yana maana zaidi pale yanaporudishwa kwa jamii. Kwa hatua kama hizi, si tu kwamba kampuni inajijengea jina la kuaminika, bali pia inazidi kuimarisha mshikamano wa kijamii, jambo ambalo lina thamani kubwa kuliko pesa.

Kwa hakika, Meridianbet si tu kinara wa michezo ya kubahatisha, bali pia ni chombo kinachoweka utu mbele na kuonyesha kuwa maendeleo ya kweli huanzia chini.

Tanzania ni miongoni mwa nchi barani Afrika zenye matumizi makubwa zaidi ya pombe haramu, hali inayoleta hatari kubwa kwa afya ya umma, wataalamu wameonya.

Haya yalibainishwa leo katika mkutano uliowakutanisha wadau kutoka Serikalini na Sekta Binafsi kujadili namna ya kukabiliana na tatizo hili linalotishia maisha na kudhoofisha ukusanyaji wa mapato kutoka sekta halali ya pombe.

Mkutano huo, wenye kaulimbiu ya "Kuungana Kupambana na Pombe Haramu Nchini Tanzania," ulisisitiza kuwa Tanzania inahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali, wasimamizi wa sheria, wazalishaji, na vyombo vya sheria ili kukabili changamoto ya pombe haramu, ambayo inakadiriwa kuwa asilimia 55 ya jumla ya pombe inayozalishwa, kusambazwa na kutumiwa nchini.

"Pombe haramu bado ni suala tete nchini Tanzania. Inaleta hatari kubwa kwa afya ya umma kutokana na uzalishaji wake usiosimamiwa, ukosefu wa udhibiti wa ubora, na mara nyingi huwa na mchanganyiko hatari. Zaidi ya hayo, biashara haramu ya pombe inadhoofisha biashara halali, inanyima Serikali mapato makubwa ya kodi, na inachochea mzunguko wa uchumi usio rasmi ambao ni vigumu kuufuatilia au kuusimamia," alibainisha Hussein Sufian, Mwenyekiti wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI).

Jukwaa hilo liliashiria uzinduzi rasmi wa utafiti wa kitaifa kuhusu pombe haramu unaolenga kubainisha ukubwa halisi na sababu za kuenea kwa pombe haramu nchini Tanzania. Aina za pombe zinazowekwa katika kundi la pombe haramu ni pamoja na bandia, pombe za kienyeji zilizotengenezwa nyumbani, pombe za magendo, pamoja na pombe zinazouzwa bila kulipa kodi za Serikali.

Utafiti huo wa pamoja kati ya Serikali na sekta binafsi unatokana na mazungumzo ya awali kati ya pande hizo mbili, ambayo yalitambua umuhimu wa kuwa na ushahidi unaoungwa mkono na takwimu katika kuunda sera, kanuni na sheria za kupambana na pombe haramu nchini.

Akizungumza kwa niaba ya wazalishaji wakuu wa pombe waliohudhuria mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Serengeti Breweries Limited (SBL), Obinna Anyalebechi, alisema sekta hiyo ilikuwa na shauku ya kutumia matokeo ya utafiti huo kubuni bidhaa maalum zitakazowavutia watumiaji kutoka kundi la pombe haramu kujiunga na pombe halali.

Kwa upande wa Serikali, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alisema lengo la juhudi hizi za pamoja ni kuhakikisha kuwa sera za kitaifa na hatua za udhibiti za baadaye zinatokana na ushahidi wa kuaminika unaotokana na takwimu, na kwamba watafanya kazi kwa pamoja kutafuta suluhisho endelevu na lenye manufaa kwa Watanzania na kwa sekta rasmi.

"Mkutano huu ni hatua muhimu katika kuratibu juhudi zetu za kupambana na biashara ya pombe haramu, tatizo linalohatarisha afya ya umma, kudhoofisha biashara halali, na kupunguza mapato ya Serikali," alisema Chalamila.

Meneja wa Mradi wa Euromonitor, Benjamin Rideout, akizungumza kwenye mkutano wa wadau uliofanyika 30 Julai 2025 jijini Dar es Salaam, kujadili changamoto ya pombe haramu, inayoaminika kuchangia asilimia 55 ya matumizi ya pombe nchini. Mkutano huo uliandaliwa na CTI na kuhudhuriwa na wadau kutoka sekta binafsi na serikali. Pichani kutoka kushoto ni Prof. Lilian Kahale (UDSM), DC wa Kinondoni Mhe. Saad Mtambule, na Mkurugenzi Mtendaji wa Serengeti Breweries, Dr. Obinna Anyalebechi.










Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizindua Kiwanda cha Majaribio cha Kuchenjua Urani cha Mantra Tanzania Limited kilichopo katika Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, tarehe 30 Julai, 2025.
















ASKARI watano na raia watatu wa Jiji la Dar es Salaam wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashitaka 16, yakiwemo ya kughushi vibali vya umiliki wa silaha na kuwasilisha nyaraka za uongo.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo na Wakili wa Serikali, Frank Rimoy, washtakiwa wametajwa kuwa ni PF Inspekta Fredrick Malekela (45), E 4627 Sajenti Kalemwa Kaunga (54), E 7855 Sajenti Edger Mlogo (54), F 1129 Sajenti Robert Titus (47), na F 5092 Sajenti John Kaponswe (46).

Washtakiwa wengine ni Damson Minyilenga (46), Simon Aloyce (60) ambaye ni mfanyabiashara, na Verand Liberio (29).

Katika kesi hiyo, washtakiwa wanakabiliwa na shtaka moja la kuwasilisha nyaraka ya uongo na mashtaka 15 ya kughushi.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Geofrey Mhini, ilidaiwa kuwa mwaka 2024 ndani ya Mkoa wa Dar es Salaam, washtakiwa kwa pamoja walitengeneza nyaraka ya uongo kwa nia ya udanganyifu, ikionyesha kibali cha kumiliki silaha chenye jina la Ahmed Abdallah Ally, huku wakijua kuwa taarifa hizo si za kweli.

Imeelezwa kuwa washtakiwa hao pia waliwasilisha nyaraka ya uongo iliyodai kuwa ni kibali cha kumiliki silaha chenye jina la Ahmed Sandrudin, wakiwa na nia ovu ya kulaghai mamlaka husika.

Katika mashtaka ya kughushi, kwa mujibu wa upande wa mashtaka, inadaiwa kuwa katika kipindi hicho cha mwaka 2024, washtakiwa wote, wakiwa na nia ovu ya kulaghai, walitengeneza vibali vya umiliki wa silaha kwa kutumia majina na namba mbalimbali za watu tofauti tofauti, huku wakijua kuwa nyaraka hizo ni za kughushi.

Hata hivyo, washtakiwa wote wamekana kutenda makosa hayo na wamerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana, ambapo mahakama ilimtaka kila mshtakiwa kuwa na mdhamini mmoja atakayesaini bondi ya Sh. Milioni nne, awe na kitambulisho cha NIDA na barua ya utambulisho kutoka serikali za mitaa.

Kesi hiyo imepangwa kutajwa tena Agosti 12, mwaka huu.







“Serikali kupitia Mradi wa BOOST imeleta mapinduzi makubwa ya elimu kwetu. Tunashukuru kwa kutujengea madarasa, matundu ya vyoo na kuweka mazingira bora ya kujifunza,” alisema Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mzizima ya Mchepuo wa Kiingereza, Maua Rashid Kibendu, akifungua ziara ya waandishi wa habari shuleni hapo jijini Dar es Salaam.

Katika ziara hiyo, wanafunzi wa darasa la sita waliwaonyesha wageni umahiri wao wa kuelewa na kueleza masomo ya sayansi kwa Kiingereza. Mwanafunzi Abiero Odwar aliwaelekeza wenzake kwa ufasaha kuhusu mfumo wa hewa na chakula mwilini, huku Subra Saad Kumbata akieleza kwa umahiri njia za uzalishaji wa umeme kwa kutumia vifaa mbalimbali.

Uwezo huo wa wanafunzi unatokana na uwekezaji wa Serikali kupitia Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi (BOOST), ambao mwaka 2024 ulitoa zaidi ya shilingi milioni 306 kwa ajili ya uanzishwaji wa shule hiyo.

Kupitia fedha hizo, shule imepata madarasa tisa, matundu 16 ya vyoo, na miundombinu mingine muhimu, hali iliyoongeza hamasa ya walimu kufundisha na wanafunzi kujifunza. Shule hiyo sasa ina wanafunzi 647 — wavulana 313 na wasichana 334 — na imekuwa kivutio cha wanafunzi kutoka shule nyingine kutokana na ufaulu wa juu katika mitihani ya kitaifa.













Top News