JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU
TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA
OFISI YA WAZIRI MKUU
TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
KUTOKAMILIKA KWA ZAHANATI YA MBEKENYERA,
MRADI WA TASAF
Mnamo tarehe 28 Februari, 2011 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI alitembelea Wilaya ya Ruangwa Mkoa wa Lindi kukagua shughuli za maendeleo. Wakati anakwenda kutembelea Sekondari ya Mbekenyera, Raia mmoja wa Ruangwa alimtumia ujumbe mfupi wa simu kwamba fedha za Mradi wa Zahanati Kijijini hapo zimeliwa, maana malipo yote yamefanyika lakini jengo limepauliwa tu na wala kuezeka hakukukamilika. Waziri wa Nchi aliamua kutembelea Mradi huo na kukuta yaliyoelezwa ni ya kweli. Mratibu wa TASAF wa Wilaya alishindwa kueleza ni kwa nini alifanya malipo yote bila kukagua maendeleo ya ujenzi.
Waziri wa Nchi ameagiza yafuatayo:-
Mratibu wa TASAF Wilaya ya Ruangwa Bwana Leslie Chande asimamishwe kazi mara moja kutokana na kutowajibika kwake na ajieleze kwenye Kamati ya Fedha ni kwa nini Zahanati haikukamilika. Aidha, Madiwani kupitia Kamati ya Fedha wachukue hatua zaidi kwa jinsi watakavyoona inafaa kwa wale wote waliosababisha kutokamilika kwa Zahanati hiyo.
Bw. Solomon Mbonile Mhandisi wa Wilaya aliyeidhinisha malipo hayo pia asimamishwe kazi haraka sana na taarifa iletwe Wizarani. Kamati ya Fedha imjadili na kumpatia Waziri wa Nchi maoni na mapendekezo yao.
Bado Wananchi wa Mbekenyera wanahitaji kupata Zahanati ndiyo maana waliibua Mradi huu. Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa imeagizwa kuchukua hatua za haraka kuhakikisha Zahanati hii inakamilika na kutoa taarifa kwa Mhe. Waziri wa Nchi ndani ya miezi miwili (2) kuanzia tarehe ya leo.
IMETOLEWA NA OFISI YA WAZIRI MKUU
TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA
17/05/2011
Naona Matunda ya Semina Elekezi yameanza kuonekana.
ReplyDeleteHEKO
Mambo hayo !!!Huwa tunalaumu serikali haisaidii kuleta maendeleo mkoani Lindi na Mtwara,sasa tunagundua kuwa viongozi wenyewe huko Lindi wanakuwa mafisadi kula hata pesa ya kukarabati zahanati,jamani hali hii ni mbaya sana.Cha msingi viongozi hawa walipe hizo pesa na pia kuchukuliwa hatua za kisheria ikibidi wafikishwe mahakamani.Pasiwe na mzunguko mkubwa hapa mara iundwe tume mara blaa blaa,makosa yao yako wazi kabisa wachukuliwe hatua tu haraka bila kupoteza wakati ili liwe fundisho kwa viongozi wengine.
ReplyDeletemtoto wa Lindi,Atlanta,Ga,Usa
Najua kuna mapungufu mengi tu kwenye utekelezaji wa miradi mbalimbali kwenye Halmashauri zetu. Swali langu ni utaratibu gani wa kumfukuza mtu kazi?
ReplyDeleteYaani mgeni akipita, fukuza kazi fulani kwa kuwa kazi mbaya,, wakati upelelezi wa kujua kilichotokea haujafanyika nk.
Kwa kweli kati ya pesa iliyoliwa na wajanja wachache na kuliletea hasara kubwa Taifa ni pesa ya TASAF. Hii ni kwa nchi nzima na sio hiyo kidogo ambayo wameigundua huko Ruangwa. Ukizingatia hii hela ilitolewa na wahisani ni deni ambalo tunatakiwa kulilipa. Lakini hakuna cha maana kilichofanyika mbali na kula pesa na wachache kutajirika sana wakati wananchi walio wengi wanalia njaa na shida zao. Ndiyo maana hata wa-CHADEMA wanajikuta wanapata support kubwa toka kwa wananchi maana sasa wamechoka na kudanganywa na kutumiwa kama njia za wachache kutajirika. Kweli inatia simanzi na inaleta hasira. Kwa nini viongozi wetu kila kitu lazima wale 90% na 10% ndiyo itumike kwa shughuli za maendeleo ya wananchi???? Jamni tutafika lini????
ReplyDeleteMdau anayeumia na ufisadi
Hongera sana serikali.Kuwasimamisha kazi tu hakutoshi..wafikishwe kwenye vyombo vya sheria.wajibu hizo tuhuma.Kuna taasisi nyingi na maeneo mengi TZ yenye matatizo ya kufanana(similar) na haya.
ReplyDeleteDavid V
Hongera Waziri wa Nchi, kwa kuchukua hatua zinazoonyesha mfano wa kufuatwa na watumishi wote wa serikali. Nakupa hongera kwa kufanya uamuzi wa kusimamisha kazi wahusika wakuu wa ubadhirifu wa fedha za nchi ila naomba usiishie kutoa amri bali uhakikishe hiyo amri inatekelezwa na watuhumiwa wafikishwe kwenye vyombo vya sheria na uchunguzi yakini ufanyike ili kugundua yote yaliyojiri mpaka fedha zikatumika ovyo badala ya kutekelezea lengo. Hapo ndipo tutapata kutambua na kujifunza ili mambo kama hayo yasijirudie. Pia Muhimu kuliko yote Mheshimiwa waziri wa nchi usisubiri utumiwe ujumbe mfupi fanya uchunguzi kwenye miradi yote ya serikali kuhakikisha inatekelezwa ipaswavyo. Unda timu madhubuti ya kufuatilia miradi ya serikali ikupe taarifa zilizokamilika zenye uthibitisho tosha ili tujikwamue tuendelee badala ya kurudishwa nyuma na watu wachache wenye kuweka maslahi yao binafsi mbele badala ya majukumu waliyopewa na taifa.
ReplyDeleteNa wachukuliwe kweli sheria sio kutufumba macho tuu. Maendeleo yanaletwa na sisi wenyewe kijiji changu hakitaendelea kama mimi mwenyewe siwajibiki ipasavyo. Tutakufa masikini for good.
ReplyDeleteMama H