RAMBIRAMBI MSIBA WA GRATIAN MATOVU.
 
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha mwamuzi wa zamani wa kimataifa Gratian Matovu kilichotokea jana saa 6 mchana (Februari 3 mwaka huu) nyumbani kwake Mbezi Beach Makonde, Dar es Salaam.
 
Licha ya kuwa mwamuzi, Matovu aliyezaliwa Novemba Mosi 1926 aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Muda ya Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (FAT), sasa TFF mwishoni mwa miaka ya 90. Pia aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi ya TFF.
 
Vilevile aliwahi kuwa mkufunzi wa waamuzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) na pia kamishna wa shirikisho hilo.
 
Msiba uko nyumbani kwake Mbezi Beach Makonde na shughuli za kumuaga marehemu zitafanyika hapo hapo siku ya Jumatatu (Februari 6 mwaka huu) kuanzia saa 5 asubuhi.
 
Kwa mujibu wa mtoto wa marehemu, Steven Matovu baadaye mwili utasafirishwa kwenda Karagwe mkoani Kagera kwa maziko ambayo yanatarajiwa kufanyika Februari 9 mwaka huu.
 
Msiba huo ni pigo kwa familia ya Matovu, TFF na familia ya mpira wa miguu kwa ujumla nchini kutokana na mchango alioutoa kwa Tanzania hasa wakati akiwa mwamuzi na mkufunzi wa waamuzi.
 
TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Matovu, Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) na kuwataka kuwa na uvumilivu katika kipindi hiki cha msiba huo mzito. Pia TFF itatoa ubani wa sh. 200,000 kwa familia ya marehemu kama rambirambi zake.
 
Mungu aiweke roho ya marehemu Gratian Matovu mahali pema peponi. Amina

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Pole sana Mrs Matovu kwa kufiwa na Baba yetu (Mume wako mpendwa tulikuwa tunamuona alivyokuwa anakuleta na ukurudisha pale Kisutu Secondary miaka ya 1977) pole sana mwalimu!
    mama G

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...