TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Katika siku chache zilizopita, Mkurugenzi wa Shule ya Chekechea ya Moses Nursery ya Yombo Vituka, Dar es Salaam, Bwana Moses Kabambara amekuwa anasambaza kadi kwa watu binafsi, makampuni, mashirika na ofisi za ubalozi zilizoko nchini akisaka michango kwa ajili ya ununuzi wa madawati na ujenzi wa madarasa na uzio wa shule yake.
Katika kadi yake ya kuomba michango na kwenye taarifa anazozisambaza kwenye vyombo vya habari, Bwana Kabambara anatumia jina la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mke wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Nembo ya Taifa kuonyesha kuwa Mheshimiwa Mama Kikwete ndiye mchangishaji na Mgeni Rasmi kwenye matembezi ya shughuli ya kuchangia maendeleo ya shule yake.
Aidha, amekuwa anadai kuwa Mama Kikwete ndiye atakuwa Mgeni Rasmi kwenye shughuli hiyo.
Tunapenda kuchukua nafasi hii kuuarifu umma wa Tanzania kama ifuatavyo kuhusu suala hili:
(a) Kwamba Mama Salma Kikwete kamwe hajapata kuridhia kuwa Mgeni Rasmi katika matembelezi hayo
(b) Kwamba Mama Salma Kikwete hajapata kukubali kuwa mchagishaji ama hata mshiriki wa aina yoyote katika uchangishaji fedha kwa ajili ya shule hiyo.
(c) Kwamba Bwana Kabambara anaufanyia udanganyifu umma ili uweze kuamini kuwa Mama Salma Kikwete amekubali kushiriki katika shughuli za uchangiaji fedha shule yake.
Tunapenda kupitia taarifa hii kuutahadharisha umma kuwa macho na vitendo vya baadhi ya watu wanaotumia majina ya Viongozi wa Kitaifa kuchangisha ama kukusanya fedha ama hata kufanya mambo mengine yenye kulenga manufaa au maslahi binafsi.
Hili ni kosa la jinai mbali na kwamba vitendo vya namna hii husababisha usumbufu kwa jamii na kwa viongozi husika.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
18 Mei, 2012
kwa ushahidi ambao upo tayari kwa serikali wanasubiri nini kumshtaki?
ReplyDeletemimi nilifikiri tungekuwa tunapewa taarifa za mhusika kuwa mikononi mwa polisi na kupandishwa kizimbani.
SERIKALI KUWENI SERIOUS.
Sheria ichukue mkondo wake. Na taarifa itolewe kama ilivyotolewa kupinga uchangishaji huo. Itakuwa fundisho kwa wengine. Serikali inapaswa kuwa seious na kumshitaki mtu huyo mara moja.
ReplyDeleteSasa mnasubiri nini?mimi nilidhani tayari yupo ukonga kumbe mnatoa angalizo asiendelee kuchangisha kiupole tu,hii ndio Tanzania mambo yake tambarareeeeeeeee,kutowajibika kumkamata ni aina fulani ya ufisadi,au kama kawaida yetu UPELELEZI bado
ReplyDeleteInashangaza kuona kuwa serikali inakanusha tu kuwa Mama Kiwete siye mgeni rasmi katika uchangishaji huo. Huyo mtu wanamjua lakini cha ajabu hakuna hatua zilizochukuliwa. Serikali kuweni makini msifanye mzaha. Kukanusha bila mhusika kumpeleka mahakamani ni kukejeli wananchi. Mdau Beijing.
ReplyDeletemna tupa taarifa ya nini wakati jamaa ni tapeli kwa nini asikamatwe...angekuwa jambazi ikulu ingetupa taarifa...mnatuchanganya wananchi
ReplyDeleteKama ni kosa na jinai kama ilivyoandikwa, kwanini mtuhumiwa hajakamatwa na kufikishwa kwenye mkono wa sheria???
ReplyDelete