ZIKIWA zimesalia siku nne kufikia mpambano wa nani mtani jembe kati ya watani wa jadi Simba na Yanga, Kocha wa zamani wa kikosi cha Wanamsimbazi Abdallah Kibadeni, amemshauri kocha mkuu wa timu ya Simba Patrick Phiri kuimarisha safu ya ushambuliaji na ulinzi.
Kibadeni alisema Simba wana nafasi kubwa ya kutetea ushindi wao, lakini wanachotakiwa kuzingatia ni kwenye safu hizo mbili ili waweze kuzuia mashambulizi ya wapinzani wao, vinginevyo itawawia ngumu.
"Mechi hiyo itakuwa ngumu kwa sababu timu hizo daima zinaushindani wa hali ya juu, lakini maombi yangu ni kuhakikisha Simba inafanikiwa kutwaa ubingwa wa nani mtani jembe, kwa sababu ina uwezo huo," alisema.

Kibadeni alisema mabeki waliopo Simba pamoja na washambuliaji ni wazuri, ila angalizo wanatakiwa kujituma na kuwa makali zaidi kila wanapopata mipira kwa sababu kosa moja tu linaweza kuwaletea matokeo mengine .
"Watulize presha ili wacheze mpira pia waache kucheza na jukwaa kwani kinachotakiwa pale ni ushindi na sivinginevyo, lakini uwezo wanao wafanye kazi iliyowapeleka uwanjani.
Aliongeza kuwa " Dany Sserunkuma waliyemsajili katika dirisha dogo ataongeza nguvu ya ushindani katika kikosi hicho kwani ana uwezo wa kuleta madhara katika lango la wapinzani wao, kikubwa ni kujipanga vema pia kujiamini," alisema Kibadeni
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...