Serikali imetoa mwezi mmoja kwa Mamlaka
zinazohusika na masuala ya usalama barabarani kuhakikisha zinakamilisha
uboreshaji wa mfumo wa kielektroniki wa uwekaji wa vifaa vya kufuatilia
udhibiti mwendo barabarani ikiwa lengo ni kushughulikia matatizo ya kiusalama
barabarani kupitia vyombo vya usafiri.
Akizungumza hayo jijini Dar es Salaam,
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani amesema
kuwa mfumo huo uendane na utengenezaji wa mpango wa Taifa wa kufuatilia masuala
ya kiusalama barabarani utakaohusisha wataalam kutoka Jeshi la Polisi Kitengo
cha Usalama Barabarani, Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu
(SUMATRA) na Wataalam wa Idara ya Usalama na Mazingira (Sekta ya Ujenzi).
"Shirikianeni kutengeneza mfumo
ambao utasaidia kutambua matatizo mbalimbali yanayoweza kujitokeza barabarani
ili kubaini mwenendo wa mabasi na malori mwanzo hadi mwisho wa safari
zake", amesema Naibu Waziri
Ngonyani.
Amesisitiza kuwa mfumo ambao utaandaliwa
na wataalam hao unatakiwa kukidhi mahitaji ya kila mmoja ili kuleta matokeo
chanya kwa manufaa ya nchi yatakayosaidia kupunguza ajali za barabarani
zinazotokana na mwendo kasi, kupambana na uhalifu na kulinda usalama wa abiria.
Aidha, Eng. Ngonyani amefafanua kuwa katika
juhudi za kuhakikisha serikali inapunguza ajali za barabarani wizara yake
kupitia Idara ya Usalama na Mazingira tayari imesaini mkataba wa kufunga
kamera za udhibiti mwendo kasi katika barabara kuu ya TANZAM (Dar es Salaam -
Tunduma), ambapo sehemu ya majaribio ya mradi huo imefanyika katika maeneo ya
Dar es Salaam - Chalinze - Morogoro.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya
Ndani ya Nchi, Eng. Hamad Masauni, amesema kuwa taratibu za kutengeneza mfumo
huo zinatakiwa kukamilika haraka ili kusaidia Jeshi la Polisi kutumia mfumo huo
kuweza kupambana na uhalifu katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Ametanabaisha kuwa Serikali itamchukulia
hatua kali za kisheria mtu yeyote atakaejaribu kuhujumu mfumo huo kwani
serikali itatumia fedha nyingi kuutekeleza kwa lengo la kuhakikisha usalama wa
raia unalindwa ipasavyo.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa SUMATRA, Gilliard
Ngewe, ameeleza manufaa ya mfumo huo kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri wa
magari ya abiria na mizigo kuwa ni itasaidia kupunguza matumizi ya mafuta,
uharibifu wa matairi ya magari mara kwa mara na kupunguza gharama za
matengenezo ya magari.
Mfumo huo wa kieletroniki wa usalama
barabarani ni moja ya mbinu zinazotumiwa na Serikali katika kuhakikisha
matumizi ya usalama barabarani yanazingatiwa kwa mujibu wa Sheria, Taratibu na
Kanuni.
Makamu
Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani ambaye pia ni Naibu Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, akizungumza na wataalam
wa mfumo wa kieletroniki wa usalama barabarani katika kikao kazi kilichofanyika
jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Naibu
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Eng. Hamad Masauni.
Mwenyekiti wa
Baraza la Taifa la Usalama barabarani ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mambo ya
Ndani ya Nchi, Eng. Hamad Masauni, akichangia mada katika kikao kazi na
wataalam wa mfumo wa kieletroniki wa usalama barabarani, jijini Dar es Salaam.
Kushoto ni Makamu Mweyekiti wa Baraza hilo ambaye ni Naibu Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani.
Kamanda wa
Usalama Barabarani, Jeshi la Polisi Tanzania Fortunatus Muslim, akifafanua
jambo kwa watalaam wa mfumo wa kieletroniki wa usalama barabarani katika kikao
kazi kilichofanyika, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa
Idara ya Usalama na Mazingira kutoka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
(Sekta ya Ujenzi), Eng. Julius Chambo akisisitiza jambo wakati wa kikao kazi
cha watalaam wa mfumo wa kieletroniki wa usalama barabarani kilichofanyika,
jijini Dar es Salaam.
Meneja wa
Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa
usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA), Godfrey Nsato, akifafanua jambo kwa
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani na Naibu
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Eng. Hamad Masauni (hawapo pichani), namna
mfumo wa kieletroniki wa kudhibiti mwenendo wa magari ya abiria na mizigo
inavyofanya kazi, jijini Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...