Abiria wakishuka kutoka kwenye kivuko cha MV. Kitunda baada
ya kuwasili kutokea Lindi mjini wakati kivuko hicho kikifanyiwa majaribio.
Kivuko hicho cha tani 50 kina uwezo wa kubeba abiria 100 na magari 6 na ni mojawapo ya utekelezaji wa ahadi ya
Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli aliyoitoa kwa wakazi wa maeneo hayo
wakati alipofanya ziara mkoani humo.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Dkt. Mussa Mgwatu akiingia kwenye chumba cha mabaharia Kivuko cha MV Kitunda kukagua.
Na Alfred Mgweno -TEMESA LINDI
Wananchi wa Lindi na Kitunda mkoani Lindi leo wameshuhudia kuwasili kwa kivuko cha MV. Kitunda ambacho kitatoa huduma katika eneo hilo na kurahisisha usafiri wa abiria na mizigo kati ya Lindi mjini na eneo la Kitunda ambalo kwa muda mrefu limekuwa likifikika kwa njia ya mzunguko umbali wa kilometa 80 kwa kutumia barabara.
Kuwasili kwa kivuko hicho ni ahadi aliyoitoa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli wakati akiwahutubia wakazi wa maeneo hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Ilulu mjini Lindi mapema mwezi Machi mwaka jana akiwa ziarani mkoani humo.
Kuwasili kwa kivuko hicho ni ahadi aliyoitoa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli wakati akiwahutubia wakazi wa maeneo hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Ilulu mjini Lindi mapema mwezi Machi mwaka jana akiwa ziarani mkoani humo.
Akizungumza mara baada ya kuwasili kwa kivuko hicho Katibu wa CCM wilaya ya Lindi Bw. Stanley Mkandawile amesema hii ni faraja kubwa kwa wakazi wa maeneo ya Lindi na Kitunda ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakipata adha kubwa ya usafiri unaounganisha maeneo hayo na amewataka kuhakikisha wanakitunza na kukithamini kivuko hicho. Bw. Mkandawile alisema serikali ya awamu ya tano imeendelea kutekeleza sera yake ya kutoa huduma bora kwa wananchi.
Nae Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Dkt. Mussa Mgwatu alisema ujenzi wa maegesho ya kivuko cha Lindi/Kitunda umekamilika kwa asilimia 98 na ujenzi wa vyumba vya abiria unaanza mara moja.
Aliongeza kusema “Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa aliwaahidi juzi (Jumatatu) kwamba kivuko hiki kitafika hapa Lindi (Jumatano) hivyo kazi yangu ilikuwa ni kuhakikisha ninatekeleza ahadi hiyo, ninayo furaha kubwa kuwaeleza wananchi hususani wa Lindi kwamba kivuko kimefika na kipo tayari kutoa huduma kwa ajili ya kuwasaidia wananchi kusafiri kutoka Lindi kwenda Kitunda na vile vile kutoka Kitunda kwenda Lindi.”
Aidha, Dkt. Mgwatu alibainisha kuwa kivuko hicho kina uwezo wa kubeba abiria 100 na magari 6 kwa pamoja sawa na uzito wa tani 50. Ujenzi wa maegesho ya kivuko upande wa Lindi na Kitunda umegharimu Shilingi za kitanzania Bilioni 1.97 na umefanywa na kampuni ya kizalendo ya Hematek Investment Limited.
Kivuko cha MV Kitunda kimewasili jana jioni na kitaanza kutoa huduma haraka iwezekanavyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...