Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeihakikishia Serikali ya Norway kuwa inaendelea kuelekeza nguvu zake kwenye kuweka mikakati sahihi ya kuvutia uwekezaji kutoka nje ya nchi, ikiwemo nchi ya Norway, ili kuleta maendeleo kwa wananchi wa Tanzania.

Hayo yamesemwa na Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania alipokutana na Bw. Jon Lamoy, Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo la Norway lijulikanalo kwa kifupi kama NORAD mwanzoni mwa ziara yake ya kikazi ya siku tatu Mjini Oslo, makao makuu ya Norway.

Katika mazungumzo yao, Mkurugenzi Lamoy alimueleza Waziri Mahiga kuwa shirika hilo limekuwa na uhusiano wa karibu na wa kindugu kwa zaidi ya miongo mitano na nchi ya Tanzania. Yeye binafsi na washirika wengi wa Tanzania nchini humo wanasifu utendaji kazi wa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli hususan kwenye mapambano dhidi ya rushwa. 

Rushwa inarudisha nyuma maendeleo kwa kuikosesha nchi mapato, hivyo jitihada za Tanzania za kupambana na rushwa, hususan kwenye ukusanyaji kodi, zitawawezesha wananchi wa Tanzania kunufaika na huduma za kijamii na hatimaye kupata maendeleo kwa haraka.

Hata hivyo mkurugenzi huyo alitoa angalizo kuwa nia nzuri ya Serikali ya Tanzania ya kuweka mifumo thabiti ya uwekezaji wenye faida  ukiwemo ule wa sekta ya madini, ni muhimu ikakamilika mapema ili kutoa fursa kwa wawekezaji wapya kuwekeza kwenye sekta hiyo kwa wakati.

Kwa upande wake, Mheshimiwa Mahiga alielezea kuwa suala hilo tayari linafanyiwa kazi ambapo pamoja na Serikali kuweka mazingira rafiki  kwa wawekezaji, uwekezaji huo ni lazima uwe na faida kwa Watanzania na kwa maendeleo ya nchi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...