Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia Mbunge wa Jimbo la Mwibara, Kangi Lugola
akizungumza katika mkutano wa hadhara na wananchi wa Kijiji cha Ragati, Jimbo la Mwibara,
Wilayani ya Bunda, mkoani Mara, jana. Katika hotuba yake, Lugola aliwaonya Polisi nchini
ambao wanatumiwa na mafisadi kuwanyanyasa wananchi maskini kwa kupora ardhi zao na
kukimbilia kufungua kesi vituoni wakilazimisha ardhi hiyo kuwa ni mali yao.
Na Felix Mwagara, MOHA
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewaonya Polisi nchini ambao
wanatumiwa na mafisadi kuwanyanyasa wananchi maskini kwa kupora ardhi zao na kukimbilia
kufungua kesi vituoni wakilazimisha ardhi hiyo iwe mali yao.
Akizungumza na mamia ya wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Ragati,
Kata ya Kasuguti, Jimbo la Mwibara, wilayani Bunda, Mkoa wa Mara, Lugola alisema amepata
malalamiko mengi kutoka sehemu mbalimbali nchini, kuwa mafisadi uonea wananchi maskini
kwa kupora kwa nguvu ardhi wakidai wanamiliki wao na wanatumia badhi ya polisi wasiokua
waaminifu ili kuwakandamiza wananchi hao.
Kutokana na hatua hiyo, Lugola amepiga marufuku kwa mwananchi yeyote ambaye
anakurupuka kukimbilia kituo cha polisi kufungua kesi za ardhi ambazo hazina uthibitisho wa
jinai yoyote, badala yake kesi au malalamiko yake kwanza ayapeleke katika mabaraza ya ardhi
katika eneo husika ili ziweze kutatuliwa.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia Mbunge wa Jimbo la Mwibara, Kangi Lugola akiliangalia panga alilopewa na Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Bunda, ikiwa ni kiashiria cha kupewa ushujaa katika jamii ya Kabila la Wagita, mara baada ya Waziri huyo kumaliza kuzungumza na wananchi wa Kijiji cha Kibara, Mkoani Mara, jana. Katika hotuba yake, Lugola aliwaonya Polisi nchini ambao wanatumiwa na mafisadi kuwanyanyasa wananchi maskini kwa kupora ardhi zao na kukimbilia kufungua kesi vituoni wakilazimisha ardhi hiyo kuwa ni mali yao.
Lugola ameongeza kuwa, mafisadi hao ambao wanafedha baada ya kuona mmiliki halali wa
ardhi hiyo anagoma kuondoka katika sehemu husika, basi utumia fedha zake kwa kukimbilia
polisi kufungua kesi bila ya kuwa na uthitisho wowote huku baadhi ya polisi wasiokua
waaminifu wakitumiwa katika kufanikisha ardhi hiyo ananyang’anywa mwananchi huyo.
“Kuanzia leo mwananchi yeyote atakaeenda kufungua kesi kituo cha polisi inayohusu masuala
ya ardhi na endapo kiwanja hicho kimepimwa lazima awe na hati inayoonyesha yeye ni mmiliki
halali, ili iwasaidie polisi wajue wewe ndio mmiliki halali, na kwa upande wa ardhi ambayo
haijapimwa lazima mwananchi huyo aende polisi akiwa na uthibitisho kutoka kijijini au katika
mtaa unaosema kwamba eneo hilo ni la kwako na polisi wathibitishe hilo,” alisema Lugola.
Lugola aliongeza kuwa, na endapo kesi ya mlalamikaji yeyote ipo mahakamani anapaswa
kuheshimu makahama na si kuendeleza kufanya usumbufu katika jamii pamoja na kwenda polisi
na kuanza kutafuta njia ya kumsumbua mwananchi ambaye ni maskini katika eneo hilo.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia Mbunge wa Jimbo la Mwibara, Kangi Lugola (kushoto), akimkabidhi zawadi ya shilingi 250,000, mshindi wa kwanza wa Bonanza la Kangi la mpira wa miguu lililofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Ragati, Jimbo la Mwibara, Wilayani ya Bunda, mkoani Mara. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Katika hilo, Lugola alifafanua kuwa, endapo mwananchi ana hukumu ya mahakamani
inayoonyesha ameshinda kesi hiyo, mwananchi huyo anapaswa kwenda polisi na nakala ya
hukumu yake ili polisi waweze kushuhudia kwamba pande zote mbili ziliwahi kugombana
kuhusu ardhi na kufikishana mahakamani lakini mmojawapo alishinda.
“Rais Magufuli alianzisha Mahakama ya mafisadi hapa nchini, kwa taarifa niliokua nayo,
mahakama hii ina uhaba wa mafisadi, sasa mimi nitaitafutia wateja kwa kuhakikisha wale
mafisadi ambao uonea wananchi, utesa wananchi, uiba fedha za serikali au taasisi yoyote
nitawafikisha katika mahakama hiyo, hatutakubaliana na manyanyaso ya aina yoyote katika
Serikali hii ya awamu ya tano” alisema Lugola.
Lugola aliongeza kua, hataki kusikia mwananchi anaonewa, na pia aliapa hatacheka na mafisadi,
atapambana nao sehemu yoyote nchini na pia yupo tayari kwalolote na ameanza kupambana na
mafisadi ndani ya wizara yake na tayari wameanza kurudisha fedha za Serikali.
Aidha, Lugola katika hotuba yake alipiga marufuku kwa waendesha bodaboda wenye tabia ya
kubeba abiria zaidi ya mmoja kuiacha tabia hiyo ili kuepusha ajali, lakini aliwataka polisi
kutorudi nyuma, wahakikishe wanawakamata waendesha bodaboda wasiofuata sheria za usalama
barabarani.
Waziri Lugola yupo katika ziara jimboni kwake kwa kutembelea miradi mbalimbali ya
maendeleo pamoja na kuwaunganisha wananchi kupitia Bonanza lake la michezo ya mpira wa
miguu ambalo linashirikisha kila kata wakitoa washindi mbalimbali ambao anawapa zawadi
pamoja na kuingia moja kwa moja katika mashindano ya kugombea Kombe la Kangi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...