NGORO ni aina ya kilimo
kinachohifadhi mazingira kwa njia ya asili ambacho kinaaminika kilianza
kutumika na wakulima wa kabila la wamatengo Wilaya ya Mbinga Mkoa wa Ruvuma
zaidi ya miaka 300 iliyopita.
Kilimo cha ngoro
kilianzishwa na wazee maarufu wa kabila la wamatengo waliotokea nchini Malawi
katika karne ya 17 ambapo tayari vizazi zaidi ya 10 vimepita hivi sasa tangu
kilimo cha ngoro kilipoanzishwa katika wilaya ya Mbinga.
Ngwatura Ndunguru
Mbunge Mstaafu wa Mbinga anataja moja ya madhumuni ya kuanzisha kilimo hiki ni
kuudhibiti udongo wa juu wa ardhi ambao
kwa kawaida huondolewa na maji au upepo
kutokana na mmomonyoko wa ardhi ya juu ambayo ina rutuba nyingi ya kuifanya
mimea iweze kustawi vizuri na hatimaye kutoa mavuno mengi na bora.
‘‘Tunajua kuwa udongo
ulio chini ya tabaka la juu hauna rutuba ya kutosha ya kuwezesha mazao kustawi
vizuri, Kutoweka kwa udongo wa juu toka shambani au bustani kwa njia ya
mmomonyoko ni hasara kubwa ,kwa vile kunasababisha upungufu wa
mavuno’’,anasisitiza Ndunguru ambaye ni
Mkurugenzi Mstaafu wa Wizara ya Maliasili na Utalii.
Anazitaja njia za
kuhifadhi ardhi zinaweza kutumiwa kwa kutegemea hali ya hewa, mazingira ya eneo
kama ni maeneo ya mwinuko au tambarare.
Hata hivyo zinaweza
kutumika njia mbili au tatu katika shamba moja.Ziko njia kuu mbili za kuhifadhi
ardhi ambazo ni njia za asili au za kienyeji na njia ya kisasa ambazo
zimefanyiwa utafiti wa kina na wataalam.
Wataalam wakongwe kama
akina Bike mwaka 1938, Stenhouse mwaka 1994,
Temu na Bisanda mwaka 1966
wanaeleza kuwa Wamatengo walilazimika kutumia kilimo cha ngoro ili kuhifadhi udongo mzuri uliopo katika
miteremko hiyo.
Katika mashimo ya ngoro
hupandwa mazao kama maharage,mahindi na ngano kwenye kingo za mashimo hayo.
Mkulima hufyeka shamba lake na kuzipanga nyasi zilizokatwa kwenye mashimo
ya ngoro.
Mkulima akipindua
udongo wa chini kuwa juu hukata nyasi na kwamba udongo wenye rutuba hugeuka
kuwa mboji na rutuba huongezeka.Maji ya mvua yakisimama katika mashimo ya
ngoro hulinda unyevu wa ardhi na kukinga mmomonyoko
wa ardhi.
Inaaminika kuwa kilimo
cha ngoro ambacho tunaweza kukiita draft agriculture kinahusishwa na shughuli
za kuwepo kwa mapango ya kuishi.Historia ya Wilaya ya Mbinga inaonesha kuwa,hapo
zamani wananchi wa Wilaya ya Mbinga walikuwa na tabia ya kufanya kilimo cha
kuhamahama.
Wakulima wakati huo
walilima sehemu moja na wanapogundua sehemu hiyo rutuba imemalizika walikuwa
wanahamia sehemu nyingine yenye rutuba na kuendesha kilimo bila kujali athari
za kimazingira ambazo zilikuwa zinajitokeza kutokana na aina hiyo ya kilimo.
Kutokana na kuwepo kwa
mapango, wazee hao wa kabila la wamatengo waliamua kuanzisha kilimo cha kulima
na kufukia majani ili kupata mbolea ya
asili hivyo kuendesha kilimo walichokiita ngoro katika sehemu moja bila kuhama
huku wakirutubisha ardhi na kuzuia mmomonyoko wa udongo kutokana na ardhi ya
Mbinga kuwa na milima yenye miteremko
mikali.
Mbunge mstaafu wa
Mbinga Ngwatura Ndunguru anasisitiza
kuwa wamatengo tangu wameanza kutumia kilimo cha ngoro miaka 300 iliyopita hadi
sasa wamekuwa wanazalisha vyakula kwa wingi na kuhifadhi mazingira kwa njia ya
asili kwa kuzuia mmomonyoko wa udongo kutokea kwenye miteremko ya milima ya
umatengo wilayani humo.
Anabainisha zaidi kuwa
katika kilimo cha ngoro mvua zinaponyesha
maji huingia kwenye mmea na majani
yaliyowekwa chini yanaoza ambapo katika msimu mwingine majani yaliota kwenye
shimo yatafyekwa,mazao yaliosalia yanavunwa
na kutandazwa kwenye shimo na kufukuliwa majani ya mwaka jana ambayo tayari
yanakuwa mboji.
John Mbunda (80) mkazi
wa kijiji cha Kilanga Juu wilayani Mbinga anasema wamatengo walianzisha
mfumo maalum wa kilimo cha ngoro
uliyowasaidia uliyojulikana kwa kabila la wamatengo kwa jina la Ingoro.
Anasema mfumo huo uliwawezesha
kuendelea kulima kwenye maporomoko ya milima bila ya kusababisha mmomonyoko wa
udongo au kuathiri vibaya rutuba kwenye mashamba yao.
Alex Ndunguru mkazi wa
Kijiji cha Ilela anasema wenyeji wa Mbinga
walilazimika kubuni kilimo cha ‘ngoro ili kuhifadhi udongo mzuri ulio
katika miteremko ya Umatengo na kwamba ngoro ndiyo mkombozi katika kilimo kwa
kuwa kilimo kimekuwa endelevu badala ya mfumo wa zamani ambao wamatengo
walifanya kilimo cha kuhamahama.
Utafiti umeonesha wazi
kwamba teknolojia ya ngoro ni bora zaidi
katika kilimo,ambapo wakulima kutoka
maeneo mbalimbali nchini wamekuwa wakifika katika Wilaya ya Mbinga
kujionea wenyewe na kujifunza teknolojia hiyo inayohifadhi ardhi na kutunza
mazingira kwa muda mrefu.
Moja ya faida ya kilimo
cha ngoro ni kwamba hata kama mvua hazitanyesha,bado shamba litaendelea kuwa na
unyevunyevu kutokana na maji yaliyomo ndani ya mashimo hayo.
Kulingana na Mbunge Mstaafu wa Mbinga Ndunguru tayari wameanza
kukitangaza kilimo hicho na kukiingiza kuwa ni miongoni mwa vivutio vya utalii
ambavyo vinapatikana katika wilaya ya Mbinga pekee.
Baadhi ya wageni ambao wamekuwa wakitembea kwenye magari
kupitia barabara ya Mbinga hadi Mbambabay Wilaya ya Nyasa pamoja na maeneo
mengine ya milima ya umatengo wamekuwa wakisimama mara kwa mara kwenye milima
hiyo na kuchukua picha za kawaida na video.
Ndunguru anasisitiza
kuwa kilimo cha ngoro kimeonekana kuwavutia
watu wengi wa ndani na nje ya
nchi hasa mimea inayochomoza na
kuonekana mfano wa mapambo yaliopambwa
juu ya milima ya Umatengo.
Wizara ya Kilimo
imeanzisha Mradi wa kufufua Mifumo muhimu ya asili ya kilimo duniani (Global
Importance Agricutural Heritage System- GIAHS) ili kuendeleza Kilimo cha asili
na kumpunguzia mkulima gharama za uzalishaji.
Taarifa kutoka Idara ya
Matumizi Bora ya Ardhi Katika Wizara hiyo inaeleza kuwa mradi huo unatekelezwa
na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) ambao unalenga kutambua mifumo ya
asili na endelevu ya kilimo na ufugaji ili kumsaidia mkulima.
Kwa mujibu wa taarifa
hiyo katika Afrika Mashariki nchi ya Tanzania na Kenya ilichaguliwa kufufua
mifumo hiyo kwa kuwa na sehemu muhimu za kilimo na kwamba baada ya kuchaguliwa
nchi ya Tanzania ilipendekeza mifumo mitatu ya kilimo asili ukiwemo mfumo wa
Ngoro ambao unatumiwa na kabila la wamatengo.
Mifumo ya asili ya
kilimo ilianza kupendekezwa duniani tangu mwaka 2002.Baadhi ya nchi ambazo
zimeanza kutumia mifumo hii ya asili katika kilimo ni Japan, UPhilipino,China na Ujerumani.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...