Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV

Klabu ya Soka ya Yanga imetangaza kuwakosa Wachezaji wake wapya na muhimu, Khalid Aucho, Fiston Mayele na Djuma Shabani katika mchezo wa hatua za awali wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Rivers United FC ya Nigeria mchezo utakaopigwa kwenye dimba la Benjamin Mkapa, Dar es Salaam Jumapili ya Septemba 12, 2021.

Yanga SC imetangaza kuwakosa Wachezaji hao kupitia kwa Afisa Habari wake, Haji Sunday Manara, amesema kuwakosa Wachezaji hao halikuwa kosa la Yanga kutokana na kupeleka maombi ya Hati za Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa wakati uliopangwa.

“Kuwakosa Wachezaji hawa hayakuwa makosa yetu sisi Yanga, mfano Mayele, Djuma mikataba yao ilikuwa mwisho tarehe 31, sisi tulipeleka DR Congo maombi ya ITC na tulipoingia nao mikataba wakasema tusubiri hadi tarehe 31 wakati dirisha lilikuwa linafungwa”, amesema Haji Manara.

Manara amedai kuwa Yanga SC ilipeleka maombi hayo ya ITC kwa wakati uliopangwa lakini pia imeshindikana kupatikana kwa Hati hizo kwa wakati uliopangwa na Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF).

Kwa upande wa Mchezaji Khalid Aucho, Manara ameeleza kuwa Aucho alikuwa na mgogoro wa maslahi na Klabu yake ya zamani ya Makkasa SC ya Misri, baadae Mchezaji huyo alikuwa huru na kusajiliwa na Yanga SC kwa wakati sahihi wa usajili.

Manara amesema, “Aucho alikuwa anacheza Misri hivyo kutokana na mgogoro uliopo kati yake na timu yake ya zamani, ndio maana wamezuia ITC yake, hivyo imeshindikana kupatikana ITC hiyo kwa mujibu muda uliopangwa na CAF wakazuia ITC ya Mchezaji huyo wa Kimataifa kutoka Uganda”.

“Tumefanya jitihada kuwasiliana na CAF lakini hawajatoa majibu yoyote kwa Wachezaji hao kucheza, tumewaandikia barua Shirikisho la Soka Ulimwenguni (FIFA) kupitia TFF kuomba kupata ITC za Wachezaji wote kwa muda kabla ya mchezo huo dhidi ya Rivers United”, ameeleza Manara.

Amesema ikitokea FIFA kushindwa kutoa majibu kuhusu ITC za Wachezaji hao, Yanga SC itacheza mchezo huo kutumia Wachezaji wake waliopo sasa. Pia amewataka Wanayanga kutoa hofu kuhusu Kikosi chao ambacho kimefanya maandalizi ya kutosha chini ya Kocha Mkuu, Nassredine Nabi kwa ajili ya mchezo huo.

Hata hivyo, CAF hawajatoa majibu kupitia TFF kuhusu idadi ya Watazamaji watakaoruhusiwa kuingia kutazama mchezo huo. Ndani ya masaa 24 kuanzia sasa CAF watatoa majibu ya kiwango cha Mashabiki wanaoruhusiwa kuingia Uwanjani kushuhudia mchezo huo kabla ya Klabu hiyo kutangaza viingilio vya mchezo husika.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...