* TARURA, Madiwani wakutana kupitia rasimu ya bajeti
HALMASHAURI Ya Manispaa ya Kinondoni itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa barabara za Manispaa hiyo ambayo mtandao wake umefikilia Kilomita 1660 ambapo fedha hizo zitakabidhiwa kwa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) ambao ndio watekelezaji wakubwa wa miradi ya miundombinu ya barabara.
Hayo yameelezwa leo na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni Songoro Mnyonge wakati wa kikao maalumu cha kupitia rasimu ya bajeti ya matengenezo ya barabara 2022/2023 iliyowasilishwa na TARURA ili kuona mahitaji halisi katika maeneo wanayoyahudumia kwa kuhakikisha kila Kata inafikiwa na miundombinu ya barabara.
Songoro amesema Halmashauri hiyo kupitia baraza la Madiwani wataendelea kutenga fedha na kukabidhi kwa Wakala hiyo kwa utekelezaji zaidi na wataendelea kudumisha mahusiano katika utendaji kazi kwa manufaa ya wananchi.
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam Eng. Sylivester Chinengu amesema Wakala hiyo imewasilisha rasimu ya bajeti kwa Baraza la Madiwani la Manispaa hiyo kama walivyoelekezwa na TAMISEMI juu ya ushirikiano kupitia vikao ili kuwa na uelewa wa pamoja katika bajeti.
Ameeleza kuwa bajeti hiyo imejikita katika maeneo matatu ambayo ni bajeti ya kawaida ya matengenezo ambayo ina shilingi bilioni 5.6 kukarabati barabara, bajeti kutoka katika maendeleo shilingi bilioni 17 pamoja na miradi ya DMDP awamu ya tatu yenye shilingi bilioni 144 ambazo zitatumika kuboresha barabara katika Manispaa hiyo yenye mtandao wa barabara kilomita 1660.
Awali akifungua kikao hicho Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Godwin Gondwe amesema, TARURA wameleta mapendekezo hayo kwa baraza la madiwani ili waweze kuona kiasi kilichopo kwa kulinganishi na maeneo yaliyoelekezwa na madiwani kuangalia uwezekaano wa kuongeza bajeti hiyo katika vikao vyao.
Amesema kuwa Halmashauri hiyo imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya miundombinu ya barabara na kuikabidhi Wakala hiyo kwa utekelezaji zaidi.
''Baraza la Madiwani linafanya kazi kubwa hasa kwa kuzingatia kutenga kiasi cha fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara, tuwaombe TARURA watumie fedha hizo sawasawa pamoja na kutoa taarifa ya matumizi ya fedha hizo...Pia waite kikao kama hiki wakati wa makabidhiano ya ujenzi kwa wakandarasi ili irahisishe ufuatiliaje na kule wanakopelekwa wakatambulishwe kwa watendaji wa Kata.'' Amesema.
Aidha DC Gondwe amewataka wakandarasi wanaosimamia miradi hiyo kuitekeleza vyema kulingana na thamani ya fedha iliyotumika.
Mkutano huo uliwahusisha Madiwani wa Manispaa hiyo, vyombo vya ulinzi naa usalama na maafisa kutoka TARURA.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...