Na Pamela Mollel,Arusha

Mama Martha Sangwa kutoka wilaya ya Simanjiro, Mkoani Manyara anakuwa mwanamke wa kwanza wa kimasai, kujifungua watoto, tena mapacha, kupitia njia ya upandikizaji mimba.

Martha (36)ambaye amejifungua watoto wawili katika hospitali ya Avinta Care ya jijini Arusha, anasema amekuwa akihangaika kutafuta mtoto kwa zaidi ya miaka kumi.

Mwanamke huyo aliwataka wanawake kujitokeza kwa wingi kuchangamkia fursa hiyo kwa kuwa haihusiani na imani za kishirikina bali ni huduma inayotolewa na wataalamu waliobobea katika masuala ya uzazi

Yeye ni miongoni mwa wanawake tisa wanaopata huduma hiyo ya kupandikiziwa watoto katika hospitali hiyo iliyopo mtaa wa Jacaranda, eneo la Uzunguni mjini Arusha.

“Kati ya wanawake hao tisa, tayari watano wamefanikiwa kupata watoto, baadhi yao wakijifungua mapacha hivyo kufanya idadi ya watoto wote waliozaliwa kwa njia hii kuwa nane,” alisema Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Akina Mama, Nicholaus Mazuguni.

Kwa mujibu wa Daktari Mazuguni, Kliniki ya Avinta Care hutoa huduma hiyo kwa kushirikiana na hospitali ya taifa ya Muhimbili, Dar-es-salaam

Aidha alipongeza serikali ya awamu ya siti chini ya Rais Mama Samia Suluhu kwa jitiada kubwa ya kuhakikisha afya nzuri ya akina mama na
hasa afya ya uzazi

"Katika hotuba yake mwaka jana mwezi wa 12 katika sherehe za Uhuru,Mh Rais alisema Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba siku za usoni huduma ya tiba ya upandikizaji mimba katika taasisi za serikali hasa Muhimbili inakuwepo"alisema Dkt Mazuguni

Aliongeza kuwa huduma hii inafanywa na watanzania wazawa lakini mwanzoni iliaminika kuwa wanaoweza kutoa tiba hii ni madaktari bigwa kutoka India,Afrika kusini na Narobi tena kwa gharama kubwa

Naye Mganga Mkuu wa mkoa, Dk Sylvia Mamkwe, aliyemuwakilisha Mkuu wa Mkoa, katika uzinduzi wa huduma hiyo maalum ya uzazi, amesema katika utoaji wa huduma bora za afya, serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi.

Dk Mamkwe amewashauri watanzania kutoogopa kutumia njia hizi mbadala za tiba katika uzazi, muhimu tu ni kupima na kuhakikisha afya zao.

“Lakini pia katika masuala ya matatizo ya uzazi mara nyingi wanawake ndio hulaumiwa, kitu ambacho sio sahihi. Wazazi wote wawili wanatakiwa kupima afya zao,” alisema Dokta Mamkwe.

Mganga huyo wa mkoa amebainisha pia kwamba, wakati mwingine kushindwa kupata watoto hutokana na tatizo dogo tu linaloweza kutibika ikiwa wahusika wangejenga utamaduni wa kupata ushauri wa kiafya.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...