


TAASISI za sekta binafsi zimetakiwa kushirikiana kwa karibu na Asasi za Kiraia (AZAKI,) katika kuleta maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla na hiyo ni kutokana na jitihada zinazofanywa na Asasi hizo kwa kuwafikia wananchi, kufahamu mahitaji yao na kuyapatia ufumbuzi.
Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Abdulmajid Nsekela wakati akifungua wiki ya AZAKI inayotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 24 hadi 28 Oktoba mwaka huu kwa kauli mbiu ya ‘Maendeleo ya Watu, Habari Fanikiwa za Watu’ jijini Arusha.
Nsekela amesema, matokeo chanya yanayotokana kupitia wiki ya AZAKI yanaonekana dhahiri tangu kuanzishwa kwake mwaka 2018 ikiwemo kuongezeka kwa umoja na mshikamano miongoni mwa wadau.
‘’Suluhisho ya changamoto zinazoikumba jamii yetu inahitaji ushirikiano baina ya wadau yakiwemo mashirika, taasisi, sekta binafsi, Asasi za kiraia na Serikali kwa ujumla, ushirikiano na AZAKI na sekta binafsi ni hafifu tukishirikiana tutafika mbali zaidi katika kujenga uchumi wa jamii na Taifa kwa ujumla.’’ Amesema.
Aidha amesema, Ushirikiano baina ya AZAKI na sekta binafsi utasaidia kutatua changamoto kwa kiasi kikubwa pamoja na kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Pia amewataka washiriki hao kuainisha njia mpya za kuwafikia wananchi na maendeleo kwa kuzingatia ushirikiano baina ya AZAKI hizo na sekta binafsi hasa katika uwekezaji.
‘’Tujadili uwekezaji wa manufaa ya kiuchumi na kuwapa watanzania utulivu wa kiuchumi kwa kutoa wigo kwa ushirikiano baina ya sekta binafsi na AZAKI katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na sekta nyingine za uwekezaji.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kituo cha Haki za Binadamu (LHRC,) Anna Henga amesema kusanyiko hilo la wana AZAKI tangu kuanza kwakwe 2018 limekuwa na malengo ya kufikia maendeleo endelevu pamoja na kubadili mtazamo wa wananchi na kutambua mchango wa Asasi za kiraia.
Aidha amesema ni muhimu sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika wiki hiyo muhimu hasa katika kupanua wigo wa kuwafikia wananchi, kutambua changamto za na kuzipatia suluhu na kuishukuru Benki ya CRDB kwa kuonesha ushirikiano tangu kuanzishwa kwa kusanyiko la Asasi za kiraia mwaka 2018.
Amesema, wiki ya AZAKI kwa mwaka 2022 itakuwa tofauti na licha ya kueleza mafanikio na maendeleo yaliyofikiwa wana AZAKI watatawanyika katika maeneo mbalimbali, kukutana na wananchi na kueleza huduma ambazo AZAKI zinatoa kwa wananchi.
‘’Tutaadhimisha wiki hii kwa namna ya tofauti, licha ya kueleza mafanikio na maendeleo tutawafikia wananchi katika mikoa ya Arusha, Manyara, Arumeru, Loliondo na maeneo mengine na kutoa huduma za afya, ushauri nasihi na kuwasiliana nao moja kwa moja na kuwaeleza huduma ambazo AZAKI mbalimbali zinatoa kwa jamii..Niwaombe wana AZAKI, sekta binafsi pamoja na Serikali za mitaa kushiriki wiki hii kwa ukamilifu.’’ Amesema.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Foundation for Civil Society (FCS,) Francis Kiwanga amesema katika wiki hiyo ya AZAKI wanataraji matokeo chanya hasa katika kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali, sekta binafsi na Asasi za kiraia katika ujenzi wa Taifa na ushiriki wa wananchi katika kuleta maendeleo.







Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...