Washindi wa mashindano mbalimbali yaliyoandaliwa na Shirika la Posta Tanzania katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Umoja wa Posta Duniani wanatarajiwa kupokea zawadi zao kutoka kwa mgeni rasmi wakati wa maadhimisho hayo.
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 6 Oktoba, 2022 na Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano na Mambo ya Posta Kimataifa Ndg. Elia Madulesi, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya Shirika la Posta Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Maadhimisho hayo yenye kauli mbiu ya “Posta Kwa Kila Mtu” yanatarajiwa kufanyika tarehe 9 Oktoba, 2022 katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), huku Mgeni Rasmi akitarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnaye.
Aidha, Ndg. Elia ameeleza kuwa Washindi watakaopewa zawadi na Mgeni Rasmi ni pamoja washindi wa Uandishi wa barua kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari wenye umri usiozidi miaka 18, Uandishi wa Insha kwa Wanamichezo na Jamii, Uandishi wa Makala kwa Wanahabari, Wabunifu wa Mfumo Tehama katika mawasiliano ya Posta na Ubunifu wa Video inayotumia vibonzo (Moving graphic).
Vilevile Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano na Mambo ya Posta Kimataifa ameongeza kuwa maadhimisho hayo yataenda sambamba na uzinduzi rasmi wa Stempu ya pamoja yenye historia kati ya Tanzania na Oman ikiwa ni muendelezo wa ushirikiano uliopo kati ya nchi hizo mbili hususani katika masuala ya Posta.
Maadhimisho ya Siku ya Posta yanaambatana na Matukio mbalimbali ikiwemo Warsha ya watoa huduma “Postal Courier Services” itakayofanyika ukumbi wa mamlaka ya Mawasiliano TCRA, Kongamano la Biashara Mtandao na Anwani za Makazi itakayofanyika tarehe 8 Oktoba,2022, katika Ukumbi wa JNICC
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...