MAONI NA USHAURI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA,

BIASHARA NA MAZINGIRA KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA


UWEKEZAJI TANZANIA WA MWAKA 2022

__________________________


1.0 UTANGULIZI:

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 99 (5) ya Kanuni za

Kudumu za Bunge, Toleo la Juni, 2020, naomba kuwasilisha Maoni ya

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira,

kuhusu Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022.


Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 97 (1) ya Kanuni za

Kudumu za Bunge, Toleo la Juni, 2020, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya

Viwanda, Biashara na Mazingira, iliupokea Muswada huu Mwezi

Septemba, 2022 baada ya kusomwa Bungeni mara ya kwanza tarehe 23

Septemba, 2022 ili iufanyie kazi, na tarehe 18 Oktoba, 2022, Waziri wa

Uwekezaji, Viwanda na Biashara alifika mbele ya Kamati na kutoa

maelezo kuhusu Malengo na Madhumuni ya Muswada huu.


Mheshimiwa Spika, dhana ya Sheria ya Uwekezaji siyo dhana ngeni

katika mizania ya Sheria na Uwekezaji hapa Tanzania na nchi nyingine.

Nchi nyingi za Afrika kama vile Kenya, Rwanda na Afrika Kusini tayari

wana hii Sheria. Kwa nchi ya Kenya Sheria hii ilitungwa Mwaka 2004 na

inaitwa Investment Promotion Act Na.6 ya Mwaka 2004 ambayo

ilifanyiwa marekebisho mwaka 2021. Kwa nchi ya Rwanda Sheria

ilitungwa mwaka 2021na inaitwa Investment, Promotion and

Facilitation Act Na. 6 ya mwaka 2021.

Kwa nchi ya Afrika Kusini Sheria ilitungwa Mwaka 2015 na inaitwa

Protection of Investment Act, Na. 22 ya Mwaka 2015. Uingereza


2


Sheria hii ilitungwa tarehe 4 Januari, 2022 na inaitwa National Security

and Investment Act ya mwaka 2022.


Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia matakwa ya Kanuni ya 97 (2) ya

Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Juni, 2020, Kamati ilitoa

matangazo katika vyombo vya habari na kuwaalika Wadau mbalimbali ili

waweze kufika mbele ya Kamati na kutoa Maoni yao kuhusu Muswada

huu.

Aidha, Wadau walifika mbele ya Kamati tarehe 19 Oktoba, 2022 na kutoa

maoni yao ambayo yamekuwa na mchango mkubwa katika Uchambuzi

wa Muswada huu.


2.0 MALENGO NA MADHUMUNI YA MUSWADA


Mheshimiwa Spika, Muswada huu unapendekeza kutungwa kwa Sheria

ya Uwekezaji Tanzania Na. 9 ya mwaka 2022. Sheria inayopendekezwa

ina Madhumuni ya kuweka masharti ya Mazingira bora kwa Wawekezaji

Tanzania, kuweka Mfumo wa Kitaasisi kwa ajili ya Uratibu na Usimamizi

wa Uwekezaji nchini na kufuta Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya mwaka

1997.


Mheshimiwa Spika, utafiti unaonesha kuwa nchi nyingi duniani na zile

zinazotuzunguka zimefanya mapitio ya Sheria za Uwekezaji ili kuweka

mazingira bora na shindani kwa Wawekezaji ikiwa ni pamoja na

kuzingatia mabadiliko ya haraka katika Mifumo ya Kiuchumi duniani.

Mapitio hayo yamewezesha kuboresha utoaji wa huduma na uratibu kwa

Wawekezaji. Vile vile mapitio hayo yameimarisha utendaji wa Taasisi

zinazohusika na Uwekezaji katika nchi hizo katika kutoa Huduma Mahala


3


Pamoja kwa Ufanisi (True One Stop Centre) na kuzingatia ushiriki katika

uchumi wa Afrika na dunia kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, kwenye Ilani ya CCM ya mwaka 2020, Sura ya Pili

Ibara ya 22 Ukurasa wa 18-19 (a) - (L) Serikali iliwaahidi Wananchi

kuboresha mazingira ya Uwekezaji. Kwa kutaja mambo machache

Chama kiliahidi: -

(a) Kuandaa na kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa kuendeleza

Uwekezaji na kuvutia Wawekezaji wa ndani na nje kwa kushirikisha

Sekta Binafsi;

(b) Kuimarisha upatikanaji wa Ardhi ya Uwekezaji kwa kuhimiza

Mamlaka za Serikali kujenga maeneo ya Uwekezaji, kulipa fidia na

kuweka miundombinu ya Msingi ili kufanikisha Uwekezaji; na

(c) Kupitia upya taratibu za utoaji vibali vya ujenzi ili kuhakikisha

kwamba vibali hivyo vinatolewa ndani ya siku saba za kazi.

Aidha, kutokana na hamasa ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais

wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutangaza na kufungua mipaka

ya uwekezaji nchini, nidhahiri kwamba Muswada huu unalenga kuweka

Mfumo Madhubuti na Endelevu ambao utaondoa vikwazo na dosari

zilizokuwa kikwazo kwa Wawekezaji nchini na hivyo kuwavutia

Wawekezaji wengi kuja kuwekeza nchini.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu umegawanyika katika Sehemu Kuu

Tano zifuatazo: -


2.1 Sehemu ya Kwanza ya Muswada

Mheshimiwa Spika, Sehemu ya Kwanza ya Muswada inajumuisha

masharti ya utangulizi ikiwa ni pamoja na Jina la Sheria

inayopendekezwa, matumizi na tafsiri ya misamiati na maneno

mbalimbali yaliyotumika katika Muswada unaopendekezwa.


4

2.2 Sehemu ya Pili ya Muswada

Mheshimiwa Spika, Sehemu ya Pili ya Muswada inaweka Mfumo

wa Kitasisi wa Uratibu na Uwezeshaji wa Wawekezaji nchini,

kuendelea kuwepo kwa Kituo cha Uwekezaji Tanzania, kuenedelea

kuwepo kwa Kamati ya Taifa ya Uwekezaji, inaweka masharti

yatakayokiwezesha Kituo kuanzisha Mfumo Unganishi wa

Kielektroniki, Uanzishaji wa Bodi, Muundo na Majukumu yake,

Vyanzo vya fedha vya Kituo na Utaratibu wa utunzaji na ukaguzi

wa hesabu;


2.3 Sehemu ya Tatu ya Muswada

Mheshimiwa Spika, Sehemu ya Tatu ya Muswada inaweka

masharti mbalimbali ya Uwekezaji. Ikiwemo kuzitaka Tasisi za

Serikali kushirikiana na Kituo katika kutoa huduma kwa

Wawekezaji kupitia Kituo cha Huduma za Mahala Pamoja. Aidha,

sehemu hii inaweka utaratibu wa maombi ya cheti cha Vivutio,

muda wa uhai wa cheti hicho na vivutio anavyoweza kupata

Mwekezaji. Vile vile sehemu hii inabainisha kuwa vivutio

vinavyosimamiwa na Sheria nyingine yoyote vitatolewa kwa mujibu

wa taratibu zilizoainishwa katika Sheria hizo;


2.4 Sehemu ya Nne ya Muswada

Mheshimiwa Spika, Sehemu ya Nne ya Muswada inahusu Haki

na Wajibu wa Serikali na Wawekezaji. Serikali inapewa haki ya

kusimamia shughuli za Uwekezaji ili kuhakikisha kuwa

zinaendeshwa kwa kuzingatia Misingi ya Sera na Sheria za nchi.

Kwa upande wa Wawekezaji wanatakiwa kutii Sheria za nchi,

kuendesha shughuli zao kwa namna inayolinda walaji, mazingira


5


na Usawa wa Kijinsia na kutoa taarifa kwa Mamlaka mbalimbali za

Serikali pale zitakapohitajika;


2.5 Sehemu ya Tano ya Muswada

Mheshimiwa Spika, Sehemu ya Tano ya Muswada inaainisha

masharti ya jumla yanayojumuisha makosa mbalimbali

yanayohusiana na masuala ya Uwekezaji na adhabu zake pamoja

na Mamlaka ya Waziri kutunga Kanuni kwa ajili ya utekelezaji bora

wa Sheria inayopendekezwa. Shemu hii pia inafuta Sheria ya

Uwekezaji Tanzania ya mwaka 1997 pamoja na kuweka masharti

ya mpito kwa ajili ya masuala mbalimbali yaliyokuwa

yanasimamiwa na Sheria inayopendekezwa kufutwa. Miongoni

mwa masharti hayo ni kuendelea kutambuliwa kwa vivutio

vilivyotolewa na Mikataba iliyoingiwa na Wawekezaji chini ya

Sheria inayopendekezwa kufutwa.


3.0 UCHAMBUZI WA JUMLA WA MUSWADA

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia Kanuni ya 24 (2) (a), (b), na (d) ya

Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Juni, 2020, Kamati ilifanya

uchambuzi wa kina wa Muswada huu wa Sheria kwa kupitia Vifungu

vyote 37 vya Muswada na kujiridhisha na Malengo na Madhumuni ya

Sheria inayotungwa katika Muswada huu.


Mheshimiwa Spika, Kamati ilipokea maelezo ya Waziri wa Uwekezaji,

Viwanda na Biashara tarehe 18/10/2022 ambaye aliieleza Kamati

kinagaubaga kuhusu Malengo na Madhumuni ya Sheria hii.


Mheshimiwa Spika, ili kukidhi matakwa ya Kanuni ya 97 (2) ya Kanuni


6


za Kudumu za Bunge Toleo la Juni, 2020, tarehe 19 Oktoba, 2022,

Kamati ilikutana na kupokea maoni ya Wadau mbalimbali kutoka katika

Sekta ya Umma, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia na Mitandao ya Kijamii ili

kusikiliza na kupokea maoni yao kwa lengo la kuisaidia Kamati katika

uchambuzi wa kitaalamu wa Muswada huu.


Mheshimiwa Spika, baada ya kupokea maoni mbalimbali ya Wadau

Kamati ilijipa muda wa kupitia na kuchambua maoni ya Wadau kwa kina

ili kujiridhisha na maudhui yake. Maoni ya Wadau kwa kiasi kikubwa

yameisaidia Kamati katika kufanya Uchambuzi wa Muswada na

hatimaye kutoa maoni kwa Serikali.


Mheshimiwa Spika, Tarehe 21/10/2022 Kamati ilikutana na mtoa hoja,

Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara ili kushauriana naye kuhusu

hoja mbalimbali za msingi ambazo Kamati iliziona kutokana na

uchambuzi uliofanyika. Yapo maeneo ambayo Kamati ilikubaliana na

Serikali na Serikali ilikubali kuchukua Mapendekezo ya Kamati. Yapo

pia maeneo ambayo Serikali ilihitaji muda zaidi kwa ajili ya kufanya

majadiliano ya ndani na kuandaa jedwali la marekebisho.


Mheshimiwa Spika, kwa ujumla Wadau waliochangia katika Muswada

huu wamekubaliana na Malengo na Madhumuni ya Muswada na

kuipongeza Serikali kwa hatua hii ya kutunga Sheria ya Uwekezaji

Tanzania.


Mheshimiwa Spika, Baada ya kufanya uchambuzi wa kina wa

Muswada huu kwa kupitia Kifungu kwa Kifungu na baada ya kupokea na

kuchambua Madhumuni na Malengo ya Muswada huu Kamati iliona

kwamba kwa maslahi ya Sekta ya Uwekezaji Tanzania kuna haja ya

kuvifanyia maboresho Vifungu 37 vya Muswada huu kwa kutazama


7


mazingira tuliyonayo hapa Tanzania na kwa kutazama pia Sheria za

namna hii zilivyo katika nchi nyingine (International Comparative

Perspective).


Mheshimiwa Spika, baadhi ya Vifungu vilikuwa na makosa ya Sarufi,

maana na mpangilio, tayari vimeingizwa katika jedwali la marekebisho la

Serikali. Kwa mfano, katika Ibara ya 2 (5) ya Muswada sentensi ‘’Bila

kujali Kifungu cha (1) Kituo kitawasaidia Wawekezaji wote, Kamati

imeshauri isomeke ‘‘Kituo Kitawahudumia’’. Serikali imeyapokea

mapendekezo ya Kamati na kuyajumuisha katika jedwali la

marekebisho.


Mheshimiwa Spika, Vifungu ambavyo vilihitaji kuboreshwa zaidi ni

kama ifuatavyo: - Kifungu cha 1 kuhusu Jina la Sheria, Kifungu cha Pili

kuhusu Matumizi, Kifungu cha 3 kuhusu tafsiri ya neno mtaji, Kifungu

cha 4, kuhusu kuendelea kuwepo kwa Kituo cha Uwekezaji, Kifungu cha

5 kuhusu malengo ya Kituo, Kifungu cha 6 Kuhusu majukumu ya Kituo,

Kifungu cha 9 kuhusu uanzishwaji wa Bodi, Kifungu cha 13 kuhusu

Maafisa na Wafanyakazi wengine wa Kituo, Kifungu cha 14 kuhusu

Ukomo wa Uwajibikaji kwa Wajumbe wa Bodi na Wafanyakazi, Kifungu

cha 18 kuhusu Kituo cha Huduma Mahala Pamoja, Kifungu cha 19

kuhusu Maombi ya Cheti na Usajili, Kifungu cha 20 kuhusu Uhai na

kufutwa kwa cheti cha vivutio, Kifungu cha 21 kuhusu Uratibu wa

uanzishwaji wa Taasisi za kibiashara, Kifungu cha 22 kuhusu Manufaa,

Kifungu cha 23 kuhusu manufaa kwa Uwekezaji wa Kimkakati au

Uwekezaji Maalum wa Kimkakati, Kifungu cha 26 kuhusu Wajibu wa

Mwekezaji, Kifungu cha 27 kuhusu Dhamana dhidi ya kurekebishwa au

kubadilishwa kwa manufaa, Kifungu cha 33 kuhusu Utatuzi wa

migogoro, Kifungu cha 34 kuhusu makosa na adhabu.

Aidha, Kamati inapendekeza kiongezwe Kifungu kimpya cha 38


8


kuhusu namna Sheria itakavyo wasaidia, kuwawezesha na

kuwalinda Wawekezaji Wazawa.


Mheshimiwa Spika, baada ya majadiliano ya kina kati ya Kamati na

Serikali, pande zote mbili zilikubaliana kufanya marekebisho kwa ajili ya

kuboresha Vifungu vyote vilivyokuwa na utata ili viwe bora zaidi.


Mheshimiwa Spika, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba

maoni na mapendekezo ya Kamati katika Muswada huu yamezingatia

Uchambuzi wa Kitaalamu wa Muswada huu uliofanywa na Kamati kwa

kushirikiana na Wadau mbalimbali waliotoa maoni yao kwenye Kamati.


4.0 MAONI NA USHAURI WA KAMATI


Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza awali Kamati ilifanya Uchambuzi

wa Muswada Kifungu kwa Kifungu hatua hiyo iliwezesha kutolewa kwa

Maoni na Ushauri kwa Serikali kuhusu maboresho ya Vifungu vya

Muswada kama ifuatavyo: -

Maoni ya Jumla

Mheshimiwa Spika, Kamati ina maoni na mapendekezo ya jumla

yafuatayo: -

Hadhi ya Kituo cha Uwekezaji ilivyo kwa sasa haiwezeshi Mfumo

madhubuti wa Kitaasisi kwa ajili ya Uratibu na Uwezeshaji wa Uwekezaji

nchini, kwa sababu hiyo, Kamati inapendekeza Kituo cha uwekezaji

kipewe Mamlaka kamili badala ya kuendelea kuwa Wakala wa Serikali,

lengo ni kukipa nguvu ya utekelezaji wa majukumu yake;

Kamati inapendekeza kuwa baada ya Sheria hii kutungwa na Bunge

‘‘itafsiriwe katika Lugha ya Kiingereza ndani ya siku 30. Sababu ni


9


uhalisia wa Uwekezaji ambao kutokana na vivutio katika Muswada huu

Wawekezaji wengi wanatarajiwa kutoka mataifa mbalimbali.

Maoni na Ushauri wa Kamati kuhusu Vifungu vya Muswada

Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 1 kuhusu Jina, Kamati inashauri

Jina la Sheria lisomeke ‘‘Sheria ya kuvutia na kulinda Uwekezaji

Tanzania ya mwaka 2022’’.

Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 3 cha Tafasiri, Kamati inashauri

kuongezeke Maneno ‘‘Ardhi’’ na ‘‘Hakimiliki’’ (Intellectual Property

Right) kwenye tafsiri ya neno ‘‘Mtaji’’.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 4 Kamati inashauri maelezo ya

pembeni yasomeke ‘‘Uwepo wa Kituo na Malengo’’.

Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 5 (1) Kamati inashauri Kifungu

hiki sasa kisomeke 4 (4). Lengo ni kuweka mpangilio mzuri wa Vifungu

vya Muswada.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 5 Kamati inashauri maelezo ya

pembeni yasomeke ‘‘Kamati ya Taifa ya Uwekezaji’’.

Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 5 (2) Kamati inashauri Kifungu

hiki sasa kisomeke 5(1), Kifungu cha 5(4) kisomeke 5(2), Kifungu cha

5(3) kibaki kilivyo na Kifungu cha 5(5) kisomeke 5(4) Lengo ni kuweka

mpangilio mzuri wa Vifungu vya Muswada.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya Uwekezaji

katika Kifungu cha 5 (2), Kamati inashauri kwamba aongezwe ‘‘Waziri


10


mwenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika

Mashariki’’. Sababu ni kwamba Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano

wa Afrika Mashariki ndiye mwenye dhamana ya kusimamia Sera ya

Mambo ya Nje ambayo imejikita kwenye Diplomasia ya Uchumi. Huyu pia

ndiye msimamizi wa Mabalozi walioko nje ya nchi wanaohamasisha na

kuwavutia Wawekezaji wa Nje kuja kuwekeza nchini.


Mheshimiwa Spika, kuhusu neno kitawasidia katika Kifungu cha 6 (1) (f),

Kamati inashauri lisomeke ‘‘kitawahudumia’’ Lengo ni kuleta maana nzuri

ya jukumu la Kituo.


Mheshimimwa Spika, katika Kifungu cha 9 (2) kuhusu Wajumbe wa Bodi

ya Kituo, Kamati inashauri kwamba Uteuzi wa Wajumbe wa Bodi ya

Kituo cha Uwekezaji uzingatie uwiano wa Kijinsia. Lengo ni kuona

kuwa uwakilishi wa Wanaume na Wanawake katika Wajumbe wa Bodi. Hii

itasaidia pia kujenga uwezo wa Wanawake katika nafasi za Uongozi na

Usimamizi bora wa utekelezaji wa Sheria hii kwa jicho la kutazama

makundi yote katika Jamii.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 9 (4) (b) (c) kuhusu muda wa

Wajumbe wa Bodi kushika nafasi zao, Kamati inapendekeza kwamba

muda wa Wajumbe kushika nafasi zao iwe miaka mitatu kwa Makundi

yote isipokuwa Mwenyekiti wa Bodi ibaki miaka Minne. Sababu ni

kuondoa tofauti kati ya Wajumbe kutoka Serikalini na wa Sekta Binafsi.


Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kufuta kwa maelezo ya

Utangulizi Aya ya 13 kwa kufuta maneno ‘‘Sekretarieti’’ badala yake

yatumike maneno ‘‘Maafisa na Wafanyakazi wengine wa Kituo’’ ili

kuendana na maelezo ya Kifungu cha 13 cha Muswada huu.


11


Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kufuta kwa maelezo ya

Utangulizi Aya ya 14 kwa kufuta maneno ‘‘Ukomo wa uwajibikaji’’ na

badala yake yatumike maneno ‘‘Kinga dhidi ya madai kwa Wajumbe wa

Bodi na Wafanyakazi’’ ambapo pia yatatumika kwenye maelezo ya

pembeni ya Kifungu cha 14 cha Muswada.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 18(4) kuhusu muda wa utoaji wa

Leseni, Kamati inapendekeza muda wa Utoaji wa Leseni au Idhini uwe

siku 7 za kazi kama ilivyobainishwa kwenye Ilani ya CCM ya Uchaguzi

Mkuu wa mwaka 2020 Sura ya Pili Ibara ya 22 (L) Ukurasa wa 19 wa Ilani.

Sababu ni kuwavutia Wawekezaji na kuondoa urasimu.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 20 (1) (a) na (b) kuhusu uhai na

kufutwa kwa cheti cha vivutio, Kamati inashauri Muswada utoe tafsiri ya

maana ya vivutio vya kifedha na visivyo vya kifedha ili vijulikane kwa

urahisi na Wawekezaji wa ndani na wa kigeni, Wasomi na wasio wasomi.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 22 (2) (d) na (e) kuhusu

manufaa, Kamati ilitoa maoni kuwa Muswada ufafanue utofauti wa magari

hayo na endapo gari la mwekezaji mwenye cheti cha vivutio lisilotumika

moja kwa moja kwenye mradi na lenye injini isiyozidi uwezo wa cc. 3000

lina sifa ya kupata vivutio. Baada ya kushauriana na Serikali, Serikali

ilikubali kwamba kinachoelezwa kwenye Aya ya (d) tayari kimejumuishwa

katika Aya ya (e), hivyo ilikubali kuondoa Aya (d) ili kuondoa

mkanganyiko kama inavyoonekana kwenye Jedwali la marekebisho ya

Serikali.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 26 kuhusu Wajibu wa

Mwekezaji, Kamati inashauri kiongezwe Kifungu (g) mara baada ya

Kifungu (f) kitakachosomeka (g) ‘‘kutunza taarifa za ukaguzi wa hesabu


12


na fedha za kila mwaka na kuwasilisha taarifa hizo Kituoni’’ na (h)

‘‘kutekeleza Mradi kwa mujibu wa Mpango Kazi uliokubaliwa wakati

wa maombi ya vivutio vya Uwekezaji’’.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 33 (1) kuhusu Utatuzi wa

migogoro, Kamati inashauri kuongeza maneno ‘‘ndani ya siku 60’’

katikati ya neno majadiliano na ili. Sababu ni kuweka ukomo wa muda

wa majadiliano.


Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 34 (1) Kamati inashauri

isomeke faini isiyopungua Milioni Tano na isiyozidi Milioni Kumi au

kifungo kisichopungua miezi sita au kisichozidi mwaka mmoja au

vyote kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, katika Kifungu cha 34 (2), Kamati inashauri

kuongeza maneno ‘‘au mwajiriwa wa Wizara, Idara au Taasisi ya

Umma’’ katikati ya neno Kituo na neno ambaye.


Mheshimiwa Spika, napenda kuliaarifu Bunge lako Tukufu kwamba

Serikali imekubali mapendekezo mengi ya Kamati na kuyaweka katika

jedwali la marekebisho lililowasilishwa katika Bunge hili. Serikali pia

imetoa maelezo ya ziada na ufafanuzi katika maeneo ya Muswada

ambayo Kamati ilihitaji ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, Kamati inaamini kwamba uchambuzi wa Kitaalamu

uliofanywa katika Muswada huu utasaidia kupatikana kwa Sheria bora ya

kusimamia Sekta ya Uwekezaji nchini na kufungua ukurasa mpya kwa

Wawekezaji nchiniTanzania.

Kamati inapendekeza Serikali iongeze Kifungu cha 38 katika Muswada

kitakachoelezea namna ya kuwasaidia, kuwawezesha, na kuwalinda,

Wawekezaji Wazawa.


13


5.0 HITIMISHO

Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru sana wewe kwa kutoa kibali ili

Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira iweze kuufanyia kazi

Muswada huu na kuipa fursa ya kuwasilisha maoni yake mbele ya Bunge

lako Tukufu.


Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru Waziri wa Uwekezaji,

Viwanda na Biashara Mhe. Dkt. Ashantu Kijaji (Mb), pamoja na Naibu

Waziri Mhe. Kigahe Exaud Silaoneka (Mb) kwa ushirikiano wao wakati

wa kuwasilisha maelezo ya Muswada huu na kutolea ufafanuzi wa hoja

mbalimbali zilizoibuliwa na Wajumbe wa Kamati.


Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru kwa dhati Wadau wote

walioshiriki na kutoa maoni yao katika Muswada huu ambayo kwa kiasi

kikubwa yamezingatiwa na Kamati. Naomba kutambua mchango wa

Wadau wafuatao: -


• Baraza la Kilimo Tanzania (ACT);

• Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS);

• Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS);

• Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC);

• Shirikisho la Wafanyabiashara na Wawekezaji Tanzania (Tanzania

Trade and Investment Coalition - TATIC),

• IResolve

• Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (Tanzania Private Sector

Foundation), na;

• Umoja wa Makampuni ya Simu Tanzania (TAMNOA).


14


Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa naomba niwashukuru

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na

Mazingira kwa weledi na umahiri wao waliouonyesha wakati wa

kuchambua Muswada huu na hatimaye kutoa maoni na ushauri wa

msingi wa kuuboresha Muswada huu.


Naomba Majina yao yaingizwe kwenye Kumbukumbu ya Taarifa

Rasmi za Bunge (HANSARD).


1. Mhe. David Mwakiposa Kihenzile, Mb - Mwenyekiti

2. Mhe. Eric James Shigongo, Mb – Makamu Mwenyekiti

3. Mhe. Hawa Chakoma Mchafu, Mb - Mjumbe

4. Mhe. Martha Nehemia Gwau, Mb - Mjumbe

5. Mhe. Daudi Silanga Njalu, Mb - Mjumbe

6. Mhe. Balozi Liberata Mulamula, Mb - Mjumbe

7. Mhe. Usonge Hamad Juma, Mb - Mjumbe

8. Mhe. Cecil David Mwambe, Mb - Mjumbe

9. Mhe. Eng. Ezra John Chiwelesa, Mb – Mjumbe

10. Mhe. Lucy John Sabu, Mb – Mjumbe

11. Mhe. Haji Makame Mlenge, Mb – Mjumbe

12. Mhe. Antipas Zeno Mgungusi, Mb – Mjumbe

13. Mhe. Askofu Josephat M. Gwajima, Mb – Mjumbe

14. Mhe. Daimu Iddi Mpakate, Mb – Mjumbe

15. Mhe. Issa Ally Mchungahela, Mb –Mjumbe

16. Mhe. Boniphace Mwita Getere, Mb -Mjumbe

17. Mhe. Maryam Omar Said, Mb, -Mjumbe

18. Mhe. Deodatus Philip Mwanyika, Mb - Mjumbe

19. Mhe. Zulfa Mmaka Omary, Mb –Mjumbe

20. Mhe. Jumanne Kibera Kishimba, Mb -Mjumbe


15


21. Mhe. Nancy Hassan Nyarusi, Mb – Mjumbe

22. Mhe. Shamsia Azizi Mtamba, Mb – Mjumbe

23. Mhe. Dkt. James Kimea Alfred, Mb - Mjumbe

24. Mhe. Salim Hassan Turky Toufiq, Mb - Mjumbe

25. Mhe. Kavejuru Eliadory Felix, Mb

26. Mhe. Hamis, Mohamed Mwinjuma mb, - Mjumbe


Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa lakini si kwa umuhimu, namshukuru

Katibu wa Bunge Ndg. Nenelwa Mwihambi, ndc, kwa Uongozi thabiti

ambao umerahisisha utendaji kazi wa Kamati. Aidha, namshukuru

Mkurugenzi wa Idara ya Kamati za Bunge Ndg. Athuman Hussein, ndc,

Mkurugenzi Msaidizi Ndg. Michael Chikokoto, ndc, Makatibu wa Kamati

waliofanikisha kazi hii ambao ni Ndg. Angelina Langisi Sanga, na Ndg.

Nyamwanja C. Chilemeji, Wanasheria wa Bunge Ndg. Praisegod Zakaria

Lukio, Ndg. Evelyne Shibandiko, na Ndg. Nesta Kawamala na Msaidizi wa

Kamati Ndg. Modesta Kipiko kwa kuiwezesha Kamati kufanya kazi yake

kwa weledi mkubwa na kuhakikisha taarifa hii inakamlika kwa wakati.


Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.


David M. Kihenzile (Mb),

MWENYEKITI, KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA. 01 Novemba, 2022.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...