Na Mwandishi Wetu
SHIRIKISHO la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) wamepata udhamini wa vifaa mbalimbali vya michezo vyenye thamani ya shilingi milioni 5.5 kutoka kwa Mkurugenzi wa Smart Sport Bw. George Wakuganda, ambaye ni mfanyabiashara wa vifaa vya michezo wa jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu wa SHIMIWI, Bw. Alex Temba amesema wadhamini hao wametoa jezi, mipira na vikombe kwa ajili ya washindi wa michezo ya mpira wa miguu na netiboli.

Bw. Temba amesema vifaa hivyo vitakuwa msaada mkubwa kwa Shirikisho zimeongeza thamani zaidi kwa kuwa sasa washindi wa michezo ya mpira wa miguu na netiboli watapata jezi tofauti na awali walikuwa wakipata vikombe pekee.

“Kamati ya Utendaji ilipokea ombi la kuja kujitangaza kwenye kikao chetu cha maandalizi ya michezo kule Mwanza na kamati iliomba waidhamini michezo kwa kutoa chochote, basi ametimiza na tumepokea vikombe 20, jezi jozi sita za michezo ya soka na netiboli na mipira ambayo itatumika kwenye mashindano yetu ya mwaka huu 2025 itakayoanza tarehe 1 hadi 16 Septemba huko jijini Mwanza,”

Bw. Wakuganda amesema nia na madhumuni ni kutengeneza mahusiano mazuri na watumishi wa umma, tofauti na sasa mojawapo ya lengo la michezo hii ni kujenga mahusiano baina ya watumishi wenyewe kwa wenyewe.

“Sisi tumeona mashindano ya SHIMIWI yanavipaji vikubwa huenda wengine hawajaviona ila sisi tumeviona, ndio maana tumevutiwa na kutoa msaada kwa kuanzia kwenye michezo hii mikubwa,” amesema Bw. Wakuganda.
NA. MWANDISHI WETU – TANGA

SERIKALI imewataka wakulima wa mwani nchini kutumia mbinu bora na za kisasa za kilimo ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo na kuongeza ushindani katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Hayo, yamebainishwa na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu, Dkt. James Kilabuko wakati akifunga mafunzo ya kujenga uwezo kwa vikundi vinavyojihusisha na kilimo cha mwani yaliyofanyika Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga kwa muda wa siku kumi na mbili kuanzia tarehe 04 hadi 15 Agosti,2025.

“Mafunzo mliyojifunza ya kilimo bora cha mwani yatawasaidia kuongeza kiwango cha uzalishaji na ubora wa mwani katika soko la ndani na nje ya nchi,” alisema na kuongeza kuwa, “Mafunzo ya uongezaji thamani, matumizi bora ya kemikali mnazotumia kutengeneza bidhaa mbalimbali zitokanazo na mwani, vifungashio vya bidhaa, zitazoweza kuwatambulisha na kuzitangaza bidhaa zenu ndani na hata nje ya nchi, upatikanaji wa masoko ya mwani” Alisema Dkt. Kilabuko.

Pia Dkt. Kilabuko alisema lengo la kuandaa mafunzo hayo ni kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wakulima wa mwani ili kuongezea mnyororo wa thamani wa zao hilo nchini.

Vilevile, aliwataka wakulima hao kujipangia utaratibu wa kufikisha maarifa waliyoyapata kwa wanakikundi wengine ambao hawakupata fursa ya kupata mafunzo hayo kwa kufanya mazoezi katika vikundi vyao hususani mafunzo ya wokozi na huduma ya kwanza majini.

“Mazingira ya kazi zenu ni katika maji, hivyo suala mlilojifunza la namna ya kujiokoa shambani ni muhimu sana, elimu hiyo itawasaidia katika kuokoa maisha yako binafsi pamoja na jirani yako pindi anapopata changamoto akiwa katika shughuli za kilimo shambani” Alisema na kuongeza kuwa,” “kile mlichojifunza muwafikishie na wenzenu ili kuwa na uwelewa wa pamoja katika kuboresha maslahi ya pamoja ya vikundi vyenu”.

Awali akitoa neno la utangulizi kuhusu mafunzo haya Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Kanali Selestine Masalamado amesema Kuwa mafunzo haya yaliyofanyika wilayani Mkinga ni awamu ya pili ya sehemu ya utekelezaji wa mwongozo wa kukabiliana na vitendo vya kihalifu katika bahari na maziwa makuu kwa lengo la kuimarisha ulinzi na usalama katika maeneo hayo uliozinduliwa Februari 2023 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa.

“Sehemu ya kwanza ulitekelezwa katika Wilaya tatu ikiwa ni pamoja na Mafia, Pangani na Bagamoyo ambazo shughuli zake kuu za kiuchumi zinategemea mazao ya bahari kwa kutoa mafunzo kwa vikundi na vyama vya ushirika, ujenzi wa vichanja vya kukaushia dagaa, na ununuzi wa boti moja ya kisasa kwa ajili ya doria baharini,”. Alisema Kanali Masalamado.

Aliongezea kuwa Kutokana na Mafanikio Makubwa wa awamu ya kwanza wa mradi wa kuimarisha ulinzi na usalama , Serikali ya Japan na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) wameendelea kuunga mkono juhudi za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha usalama majini kwa kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa boti mbili za doria, ujenzi wa makaushio ya mwani na mashine ya kusaga mwani, pamoja na kutoa mafunzo elekezi kwa vikundi 26 vya wakulima wa mwani katika Wilaya ya Mkinga.

Naye, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga Bw. Rashid Karim Gembe amepongeza uwepo wa mafunzo na kutoa shukrani za dhati kwa wafadhili pamoja na waratibu wa mafunzo hayo yatakayo leta mapinduzi ya mnyororo wa thamani wa zao la mwani na kuwakomboa kiuchumi wakulima wa mwani, hivyo ameahidi kuendelea kuwashika mkono wakulima wa mwani kwa kuwahakikishia ushirikiano utakao wawezesha kuyafikia malengo kupitia zao hilo.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Shirika la Maendelo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bw. Saimon Nkonoki amesema kuwa, awamu ya pili ya sehemu ya mradi ambao umeanza kwa mafunzo wilayani Mkinga umepokelewa vizuri kwa muitikio na ushirikiano mkubwa ikiwa ni ishara ya utayari wa Serikali katika kuwahudumia wananchi wake.

“Tunaahidi kuendeleza ushirikiano huu kwa wadau mbali mbali wa maendeleo hapa nchini, huku tukitoa rai kwa vikundi vilivyonufaika na mafunzo haya kuyaishi kwa vitendo hasa yale ya vitendo tunaamini yatawasaidia sana”. Alisema Bw. Nkonoki

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo haya wameshukuru mafunzo yaliyotolewa kwao huku wakieleza namna yatavyowasaidia wakulima wa zao la mwani kwa ujumla na kueleza yatawafaa wao na jamii nzima.

Akiongea kwa niaba ya washiriki wenzake Bi. Aisha Jumbe amesema, “tunaamini zao hili tunaenda kulipa heshima kwa kupitia mafunzo haya, ambapo tutakuwa na mbinu mpya za huduma za kifedha, kujua soko na mahitaji ya soko, uandaaji wa fedha na utunzaji wa fedha na hii itatusaidia katika hatua zote za kilimo hadi kufikia matokeo ya mwisho kwa watumiaji wa bidhaa zetu ikiwemo; sabuni za kuogea, kufua, kusafisha maliwato, dawa kwa magonjwa mbalimbali na nyingine nyingi;”.

Mafunzo hayo ya kuvijengea uwezo wa kilimo bora, usimamizi wa vikundi, usimamizi wa fedha,utunzaji kumbukumbu, kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao pamoja na masoko ya zao la mwani kwa vikundi vya wanawake na vijana vya wakulima wa zao la mwani wa Wilaya ya Mkinga, Mkoani Tanga, yameratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini kwa ufadhili wa Serikali ya Japan pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).








 

Na Munir Shemweta, WANMM MBARALI

Baadhi ya wananchi katika halmashauri ya wilaya ya Mbarali mkoa wa Mbeya wameipa pongezi wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuandaa Klinik ya Maalum ya Ardhi kwa ajili ya kuongeza kasi ya umlikishaji ardhi katika maeneo yao.

Klinik Maalum ya Ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Mbarali imeanza tarehe 6 Agosti 2025 na inatarajiwa kumalizika tarehe 18 Agosti 2025 na inahusisha viwanja 30,700 vilivyopangwa na kupimwa kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Usalama wa Milki (LTIP). Mradi huo ulifanyika katika Kata ya Rujewa, Ubaruku, Lugelele, Mabadaga, Igulusi, Kongoromswiswi na Madibira.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti tarehe 14 Agosti 2025 wakati wa Klinik Maalum ya ardhi ilinayofanyika kijiji cha Ubaruku wilayani Mbarali, wananchi hao wamesema uamuzi wa wizara ya ardhi kuandaa klinik hiyo ya ardhi umewarahisishia kupata hati milki za maeneo bila ya usumbufu.

‘’Hili walilofanya wizara kuandaa klinik Maalum ya Ardhi katika eneo hili la Mbarali kwa kweli limetufurahisiha sana kwa kuwa tumepata hati hap hapa, tumesubiri kwa muda mrefu kupata hati na hatimaye kilio chetu kimesikilizwa’’ amesema Juma Omar mkazi wa Ubaruku.

Kwa mujibu wa wakazi hao wa Ubaruku, maeneo yao waliwekewa mawe kwa muda mrefu lakini umilikishaji haukufanyika kwa wakati jambo lililowafanya wananchi kuwa na mashaka juu ya zoezi la umilikishaji.

Wamesema kuwa, iwapo kasi ya umilikishaji inayofanyika hasa kwenye maeneo yaliyoainishwa basi wananchi wa maeneo husika wataweza kunufaika na umiliki wa ardhi yao kwa kupatiwa hati milki inayoweza kutumika kwa shughuli mbalimbali ikiwemo kukopea katika taasisi za fedha.

Sheikh Haroun Mkanyanga, mkazi wa Igawa mbali na kuipongeza wizara ya Ardhi kwa kuandaa Klinik Maalum amewataka wananchi wa Mbarali kuchangamkia zoezi hilo kwa kuwa limewarahisishia kazi ya kufuata huduma hiyo ya ardhi umbali mrefu.

‘’Niwatake wamiliki wenzangu wa ardhi kujitokeza kwa wingi kupata huduma hii ya ardhi hususan hati milki kwa kuwa ardhi ni kila kitu na unapokuwa na umiliki utaepukana na migogoro ya ardhi kama vile migogoro ya mipaka’’ amesema

Kwa upande wake Mratibu wa Program ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) Elia Kamihanda amewataka wananchi wa Wilaya ya Mbarali kujitokeza kwa wingi kupata huduma kupitia zoezi hilo lililoanza tarehe 6 Agosti 2025 na kuhitimishwa tarehe 18 Agosti 2025 kwa kuwa huduma zimesogezwa karibu na wananchi

‘’Niwaombe ndugu zangu wa Mbarali kuchangamkia zoezi hili kwa kuwa limewasogeza huduma lakini mbali na hapa watalazimika kufuata huduma katika ofisi zetu jambo ninaloona halileti afya wakati huduma kwa sasa zipo hapa’’ amesema Kamihanda.

Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha Klinik Maalum ya Ardhi kwa ajili ya kuongeza kasi ya umilikishaji ardhi kwenye maeneo ambayo mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki (LTIP) umetekelezwa.

Klinik hiyo maalum ya ardhi inafanyika Dar es Salaam katika manispaa ya Ilala, Dodoma eneo la Mpunguzi, Mbeya halmashauri ya Mbarali na mkoa wa Shinyanga katika halmashauri ya Kahama pamoja na Manispaa ya Shinyanga.

Kupitia klinik hiyo huduma mbalimbali zitatolewa kama vile umilikishaji ardhi wa papo kwa hapo kwa wamiliki waliokamilisha taratibu za umiliki, utoaji elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya mfumo wa utoaji huduma za ardhi kidigiti (e-Ardhi) na Usaidizi wa ufunguaji wa akaunti ya Mwananchi kwenye mfumo wa e-Ardhi.

Huduma nyingine ni Uhakiki na utambuzi wa viwanja vya Wananchi Uwandani, Utoaji wa namba ya malipo (control number) za ada mbalimbali za Serikali kwa ajili ya umilikishaji pamoja na Upokeaji, usikilizaji na utatuzi wa migogoro kiutawala.
Mmoja wa mwananchi aliyejitokeza kupata huduma (kulia) akihudumiwa na watumishi wa Wizara ya Ardhi wakati wa Klinik Maalum ya Ardhi katika kijiji cha Ubaruku wilayani Mbarali mkoa wa Mbeya.
Wananchi wakipata huduma wakati wa Klinik Maalum ya Ardhi inayoendelea katika Halmashauri ya wilaya ya Mbarali mkoa wa mbeya.
Wananchi wakisubiri kupatiwa huduma wakati wa Klinik Maalum ya Ardhi inayoendelea katika Halmashauri ya wilaya ya Mbarali mkoa wa mbeya.
Baadhi ya watumishi wa wizara ya ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakitoa huduma wakati wa Klinik Maalum ya Ardhi wilayani Mbarali mkoa wa Mbeya
Mratibu wa Program ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) Elia Kamihanda akizungumza wakati wa ufunguzi wa Klinik Maalum ya Ardhi katika kijiji cha Ubaruku Mbarali Mbeya (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)
 

hh




Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Shirika la WILDAF limeanza kuwanoa wagombea wanawake nchini na kuwapa mikakati ya kampeni ili waweze kushinda kwenye uchaguzi mkuu na kuongeza wanawake viongozi.


Mafunzo hayo yanayofanyika wiki hii, yanawajumuisha wanawake 200 wakiwemo 100 kisiwani Zanzibar na Pemba pamoja na 100 jijini Dar es Salaam.


Mratibu wa WILDAF Wakili Anna Kulaya amesema hayo wakati akitoa maelezo juu ya mafunzo hayo jijini Dar es Salaam ambapo alisema wagombea wanawake wanajengewa uwezo wa namna ya kufanya kampeni, kuongea na hadhira, usalama wao binafsi na usalama wa taarifa na wa kidijitali.


Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo akiwemo mgombea wa tiketi ya CCM kwa nafasi ya Udiwani katika Kata ya Ndugumbi Bi. Amina Zuberi Mtemvu amesema kuwa mafunzo hayo yamewasaidia kujua vitu vinavyotakiwa na visivyotakiwa wakati wa kampeni.


"Mafunzo haya yametujengea kujiamini wakati wa kuomba kura", amesema Mtemvu.


Kwa upande wake, Saida Kupela mgombea udiwani wa kata ya Vingunguti kwa tiketi ya ACT amesema mafunzo hayo yamemsaidia kuwa kiongozi wa mabadiliko anaefikilia mafanikio badala ya kuwa mtawala.


"Mafunzo haya yamenipa ujasiri kwamba ninaweza iwapo nitajiamini," amesema Kupela.


Naye Salma Kalokola mgombea udiwani kwa tiketi ya CUF katika kata ya kivule amewashukuru WILDAF na kusema kuwa mafunzo haya yamemsaidia kujua namna ya kushiriki uchaguzi mkuu kama mwanamke na kuwa jasiri zaidi.


Mwezeshaji katika mafunzo hayo Bi Rose Ngunangwa amewataka wanawake hao kuhakikisha kwamba wanakuwa matarishi wa amani na kutoa matumaini kwa wapiga kura wakati wa kampeni zao ili waweze kupita.


Vilevile, amewaasa wagombea hao kulinda sana taarifa zao za muhimu yakiwemo majina matatu na simu zao ili zisitumike vibaya kuzima ndoto zao za Uongozi.


Mafunzo haya yanafanywa na WILDAF kupitia mradi wa Irish Aid Wanawake Sasa unaofadhiliwa na Serikali ya Ireland ambapo pamoja na mengineyo wagombea wanafundishwa namna ya kukabiliana na ukatili mtandaoni, usalama wa taarifa, usalama wao binafsi na wa kidijitali.


Vilevile mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wagombea namna ya kujenga amani na kutatua migogoro ambapo yamejumisha wagombea kutoka vyama vya CCM, ACT Wazalendo, NCCR Mageuzi CHAUMA na CUF.







Na Mwandishi Wetu,Kigoma

Wananchi katika Manispaa ya Kigoma Ujiji wameanza kunufaika na mradi wa TACTIC unaotekelezwa chini ya Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia.

Akielezea mradi huo unavyotekelezwa katika Manispaa ya Kigoma Ujiji , Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa hiyo Bw. Kisena Mabuba amesema kuwa mradi huo umejikita katika uboreshaji wa miundombinu ambapo kwa Manispaa hiyo kazi zinazofanyika ni pamoja na ujenzi wa mitaro ya maji, ujenzi wa daraja, masoko na barabara.

Aidha, ameongeza kuwa miundombinu hiyo inayojengwa inalenga kukuza uchumi wa wananchi na kuondoa kero za usafiri na usafirishaji huku akibainisha kuwa kipindi cha masika wananchi walikua wanapata shida kwani maji yaliingia katika makazi yao lakini kupitia mradi wa TACTIC tayari mitaro imejengwa na maji yanaelekezwa moja kwa moja ziwani.

"Kupitia mradi huu, tutapata barabara za kiwango cha lami zenye urefu wa kilomita 9.5 ambazo zitaunganisha Kata sita za Manispaa yetu, uwepo wa taa za barabarani pia utapendezesha Mji wetu, “alisema

Kwa upande wake Mhandisi Julius Samwel ambaye ni mratibu wa mradi wa TACTIC ngazi ya Manispaa amesema kuwa miradi yote imeanza na utekelezaji wake upo katika hatua mbalimbali.

Wakiongea kuhusu miradi hiyo wananchi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji wameonesha furaha yao juu ya utatuzi wa kero ya muda mrefu.

Bi. Mariam Athumani ambaye ni Mkazi wa Kigoma Ujiji amesema kuwa kabla ya ujenzi wa mifereji ,maji yaliingia katika makazi na kusababisha kero na uharibifu wa mali lakini kwa sasa yameelekezwa moja kwa moja ziwani.

Akiongea kuhusu ujenzi wa Soko la Mwanga Bw. Hussein Hamis ambaye ni mkazi wa Manispaa ya Kigoma amesema kuwa kukamilika kwa soko hilo kutachochea uchumi wa Mkoa kwani watapata wageni mbalimbali kutoka nchi za jirani zikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi ambao watafika kufanya biashara.

Kuhusu ujenzi wa Soko la samaki Katonga, wafanyabiashara wameipongeza Serikali kuleta mradi huo utakaowawezesha kufanya biashara kwa njia za kisasa na kukuza uchumi .


BONDIA wa ngumi za kulipwa nchini, Hassan Mwakinyo, amesema yupo tayari kupambana na bondia yeyote, mradi maslahi ya pambano yatakuwa mazuri.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam na waandishi wa habari kuelekea pambano lake lijulikanalo kama Dar on Boxing Day litakalofanyika Desemba 26 mwaka huu mkoani Mwanza, Mwakinyo amesema anaamini uwezo wake kwenye mchezo wa ngumi unaweza kumkutanisha na mpinzani wa aina yoyote.

“Nipo tayari kupigana na bondia yoyote, ilimradi nipate maslahi ninayoyahitaji, kwani najua nina uwezo mkubwa kwenye ngumi,” amesema Mwakinyo.

Ameongeza kuwa anaendelea na mazoezi kwa ajili ya kuhakikisha anafanya vizuri katika pambano hilo, huku akibainisha kuwa mpinzani wake atatangazwa baadaye.

Kwa upande wake, Mratibu wa Kampuni ya Peak Time Sport Agency, Bakari Khatibu, amesema lengo la pambano hilo ni kuinua vipaji vya mabondia waliopo katika ukanda wa Ziwa na kuendeleza sifa ya mchezo wa ngumi nchini.

“Lengo la kufanya pambano hilo ni kuinua vipaji vya mabondia waliopo kanda ya Ziwa pamoja na kuendelea kuutangaza mchezo wa ngumi,” amesema Khatibu.

Amesema mpinzani wa Mwakinyo atatangazwa hivi karibuni ili mashabiki na wadau wa ngumi waweze kumfahamu mapema.
Taasisi ya Self Microfinance Fund (Self Fund) imeeleza mikakati ya kuwafikia Watanzania wengi zaidi wenye kipato cha chini wanaojishughulisha na uzalishaji mali ili kuwawezesha kujiongezea kipato na kupunguza umaskini.

Taasisi hiyo ya serikali chini ya Wizara ya Fedha ilianzishwa mwaka 2015, imeeleza pia nia yake ya kusaidia kupunguza changamoto za mikopo inayotolewa kiholela kwenye jamii na mwisho wa siku kuwaumiza watanzania ikiwemo ile maarufu kama ‘Kausha Damu’.

Sambamba na hayo yote imejizatiti kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhakikisha Watanzania asilimia 80 wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034 ambapo imeshakopesha Sh100 milioni tangu Januari hadi sasa sekta ya nishati safi.

Hayo yamesemwa leo Ijumaa Agosti 15, 2025 na Ofisa Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo, Santiel Yona wakati akizungumza na wahariri na wandishi wa vyombo mbalimbali vya habari katika mkutano ulioandaliwa na ofisi ya Msajili wa Hazina.

Aidha, Self Fund imetangaza mpango wa miaka mitano wa kupanua huduma zake kwa wajasiriamali wadogo kote nchini. Lengo lake ni kupunguza umaskini na kukomesha vitendo vya ukopeshaji wa kinyonyaji ambavyo vimewafikisha Watanzania kwenye madeni makubwa.

Aidha, Self Fund inalenga kuongeza mtaji wa mikopo hadi Sh300 bilioni ndani ya miaka mitano ijayo, ikifikia zaidi ya wanufaika 200,000 moja kwa moja. Taasisi pia inapanga kuongeza idadi ya matawi yake kutoka 12 hadi 22 ili kufikia huduma nchi nzima.



Songea, Ruvuma – Agosti 15, 2025

Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi na Ugavi Wilaya ya Songea Raymond Aloyce, ameipongeza Shule ya Awali na Msingi Simagoo kwa mafanikio makubwa katika sekta ya elimu, wakati wa mahafali ya nane ya elimu ya awali na ya nne kwa darasa la saba yaliyofanyika leo Agosti 15.

Akihutubia  mgeni rasmi katika hafla hiyo, Aloyce alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya walimu, wazazi na jamii kwa ujumla katika malezi na maendeleo ya mtoto.

Katika kuunga mkono jitihada hizo Aloyce aliahidi kuchangia vifaa vya michezo kwa shule hiyo ili kusaidia kuimarisha vipaji vya wanafunzi na kukuza nidhamu, afya na mshikamano wao kupitia michezo.

Aidha, alitoa wito kwa wazazi kuhakikisha watoto wanapata elimu katika mazingira bora na salama, huku akiahidi kuendelea kushirikiana na shule hiyo katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Shule ya Simagoo, iliyoanzishwa mwaka 2016 ikiwa na wanafunzi saba tu, sasa ina jumla ya wanafunzi 653 (wavulana 345 na wasichana 368). Mafanikio makubwa yamepatikana, ikiwa ni pamoja na ufaulu wa hali ya juu wa darasa la saba ambao umeiwezesha shule kushika nafasi ya pili kiwilaya, ya sita kimkoa, na ya 249 kitaifa.

Shule hiyo pia imefungua tawi jipya Peramiho, kuongeza idadi ya mabasi ya wanafunzi, na kuimarisha uwezo wa wanafunzi kusoma, kuandika na kuzungumza Kiingereza kwa ufasaha.

Hata hivyo changamoto bado zipo, Shule inakabiliwa na ucheleweshwaji wa ada, uhaba wa kompyuta, ukosefu wa ukumbi wa mikutano, mabwalo ya chakula, na vifaa vya michezo changamoto ambazo Aloyce aliahidi kushughulikia kwa kushirikiana na wadau wa elimu.

Wazazi waliohudhuria walieleza kuridhishwa na maendeleo ya watoto wao, wakibainisha kuwa Simagoo imewasaidia watoto wao kuimarika katika nidhamu, mawasiliano na stadi za maisha.






MKUU wa Wilaya ya Temeke, Sixtus Mapunda, amezielekeza halmashauri za manispaa zote mkoani Dar es Salaam, kuhakikisha zinawatumia kikamilifu wahitimu wa mafunzo ya awali ya Jeshi la Akiba katika utekelezaji wa operesheni mbalimbali.

Ametoa maelekezo hayo leo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, katika hafla ya ufungaji wa Mafunzo ya Awali ya Jeshi la Akiba Kundi la 63/2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Kambi ya Jeshi la Wanamnchi Tanzania ya Twalipo, wilayani Temeke.

“Manispaa zote katika shughuli zao na operesheni zao ziwatumie vijana hawa. Wakurugenzi muwatumie wahitimu hawa haraka kabla hawajarudi mtaani,”amebainisha Mapunda.

Amesema vijana hao wakiachwa mtaani kwa kipindi kirefu bila kutumika watasahau kwa haraka kiapo chao.

“Tuna operesheniu za kukusanya mapato. Tuna maandalizi ya uchaguzi mkuu na kusimamia taratibu mbalimbali katika manispaa zetu. Hawa vijana wako tayari kutumika,”ameeleza Mapunda.

Aidha, ametoa wito kwa wahitimu hao kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29 mwaka huu.

“ Oktoba 29 ni siku ya uchaguzio mkuu. Tujitokeze kwa wingi kupiga kura. Ninawakabidhi jukumu la kwenda kuhamasisha vijana wenzenu kujitokeza kupiga kura,”amesema.

Mapunda aliwataka, aliwataka wahitimu hao kuishi kwa kiapo na kujiepusha kutumia mafunzo waliyopata katika vitendo viovu.

Awali Mshauri wa Jeshi la Akiba Mkoa wa Dar es Salaam, Kanali Emmanuel Kasyupa, alisema mafunzo hayo yalijumuisha vijana kutoka wilaya tano za mkoa huo ambazo ni Ilala, Temeke, Kinondoni, Kigamboni na Ubungo.

“Mafunzo yalianza Aprili nne mwaka huu yakiwa na wanafunzi 414. Wanafunzi 66 walishindwa kuendelea kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za utoro, matatizo ya afya na utovu wa nidhamu,”alieleza Kanali Kasyupa.

Amesema jumla ya wahitimu wote ni 348, wanaume 263 na wasicha 85 ambapo mafunzo hayo yalifanyika kwa wiki 18.

Kanali Kasyupa alibainisha, wakufunzi walitoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi, Uhamiaji, Usalama wa Taifa na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

“Kiapo kimesikika. Mmeahidi kuwa watiifu na waaminifu kwa Amirijeshi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mtakuwa watiifu kwa raia . Usiende kukiweka kiapo hiki katika begi. Ikiwezekana ubandike sebuleni ili mgeni akija atambue unawajibu gani kwa taifa,”ameebainisha.

Amesisitiza wahitimu hao kulinda uhuru na uchumi wan chi kama walivyo apa.

“Askari hawa wamefikia kiwango kinachokubarika katika jeshi la akiba na wapo tayari kutumikia taifa katika kutekeleza majukumu mbalimbali,”alieleza Kanali Kasyupa.

Katika mafunzo yao wahitimu hao walipata masomo mbalimbali kwa nadharia na vitendo, ikiwa ni pamoja na kwata, ukakamavu,mbinu za kivita, ujanja wa porini, usomaji ramani, huduma ya kwanza, zimamoto, uhamiaji, usalama wa taifa, Kuzuia na kupambana na rushwa , silaha ndogondogo, utimamu wa mwilki, uraia, kazi za polisi, uhamdisi wa medani,Sheria za Jeshi la Akiba, na vita vya msituni.

Katika risala yao wahitimu hao waliiomba serikali kuongeza bajeti ya mafunzo ya jeshi la akiba na kuwapa kipaumbele kujiunga na JKT na taasisi zingine za aserikali.









WAANDISHI wa habari mkoani Dar es Salaam wamejengewa uwezo kuhusu namna ya kuripoti Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 kwa kuzingatia usalama wao, usawa wa kijinsia, na sheria mpya za uchaguzi zilizopitishwa mwaka 2024.

Mafunzo hayo ya siku moja, yaliyoandaliwa na Kampuni ya Media Brains kwa udhamini wa Shirika la Konrad Adenauer Stiftung (KAS) kutoka Ujerumani, yalilenga kuwapa wanahabari mbinu sahihi za kutekeleza majukumu yao bila kuvunja sheria na kuepuka upendeleo wa kihabari.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Media Brains, Jesse Kwayu, alisema tafiti zinaonyesha kuwa katika Uchaguzi Mkuu wa 2020, wagombea wanawake walipata nafasi ndogo kwenye vyombo vya habari ikilinganishwa na wanaume, hali inayohitaji kubadilika mwaka huu.

“Tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu, vyombo vya habari vinapaswa kutoa nafasi sawa kwa wagombea wote bila kuonesha upendeleo wa kijinsia,” alisema Kwayu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mwenza wa Media Brains na mwandishi mkongwe, Absalom Kibanda, alisisitiza umuhimu wa wanahabari kusoma kwa makini Sheria ya Vyama vya Siasa, Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2024, pamoja na Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC).


“Sheria hizi zimeanza kutumika kwenye mchakato wa awali wa uchaguzi. Ni muhimu wanahabari wakazifahamu ili kujilinda kisheria na kutekeleza majukumu yao kwa weledi,” alisema Kibanda.

Mkurugenzi wa Media Brains, Neville Meena, aliongeza kuwa uelewa wa sheria utasaidia wanahabari kuepuka makosa, hasa wanapowahoji wagombea na wadau wa uchaguzi.

Mafunzo hayo pia yalihimiza uhakiki wa habari kabla ya kuchapishwa ili kuepuka taharuki na kuchochea chuki katika jamii.



 ).


Top News