MICHUANO YA KOMBE LA UHAI (UHAI CUP)
Michuano ya kuwania Kombe la Uhai (Uhai Cup 2011) inayoshirikisha timu za pili (U20) za klabu zote 14 za Ligi Kuu ya Vodacom inatarajia kuanza Novemba 12 mwaka huu katika Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam.
Timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boyz) itashiriki michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Said Salim Bakhresa ikiwa timu mwalikwa.
Bingwa wa michuano hiyo atapata sh. milioni 1.5, mshindi wa pili sh. milioni moja wakati wa tatu atapata sh. 500,000. Mbali ya fedha hizo, bingwa atapata medali za dhahabu, makamu bingwa medali za fedha na mshindi wa tatu medali za shaba.
Mchezaji bora atapata sh. 400,000, mfungaji bora (sh. 300,000), kipa bora (sh. 300,000) na timu yenye nidhamu itapata sh. 300,000. Kila timu inayoshiriki itapatiwa sh. milioni moja kwa ajili ya maandalizi.
Mdhamini pia atagharamia nauli za kuja Dar es Salaam na kurudi kwa timu ambazo zinatoka mikoani. Michuano hiyo itachezeshwa na waamuzi vijana kama ilivyokuwa msimu uliopita.
Pia mradi wa Campaign Against Malaria nao utasaidia kwa kutoa jezi kwa timu zote zinazoshiriki michuano hiyo.
Kesho (Novemba 5 mwaka huu) saa 4 asubuhi kutakuwa na mkutano kati ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na klabu zenye timu shiriki na baadaye kufanyika upangaji ratiba.
STARS KUTEMBELEA MAKUMBUSHO YA TAIFA
Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) ambayo hivi sasa iko kambini kujiandaa kwa mechi dhidi ya Chad, kesho (Novemba 5 mwaka huu) saa 5 asubuhi itatembelea Makumbusho ya Taifa.
Ziara yao ni ya kawaida, lakini pia kutakuwa na onyesho la Historia ya Soka Tanzania.
Wachezaji ambao tayari wapo kambini hoteli ya New Africa ni Juma Kaseja, Godfrey Taita, Shabani Nditi, Hussein Javu, Juma Jabu, Ramadhan Chombo, Shomari Kapombe, Nurdin Bakari, Nadir Haroub, Juma Nyoso, Erasto Nyoni, Mrisho Ngasa, Mwadini Ally na Aggrey Morris.
Idrisa Rajab wa Sofapaka ya Kenya tayari naye yuko kambini wakati wachezaji wengine kutoka nje wanatarajia kuwasili leo usiku. Wachezaji wa mwisho kutoka nje tunawatarajia kesho.
MORO UTD, SIMBA ZAINGIZA MIL 5.7
Mechi namba 86 ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Moro United na Simba iliyochezwa Novemba 2 mwaka huu Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam imeingiza sh. 5,764,000.
Watazamaji waliokata tiketi kushuhudia mechi hiyo walikuwa 1,688 ambapo kiingilio kilikuwa sh. 10,000 kwa VIP na sh. 3,000 kwa majukwaa mengine. Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo ni asilimia 18 iliyolipwa ni sh. 879,254.
Gharama za awali kabla ya mchezo; kila klabu ilipata sh. 118,160 wakati Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) kilipata sh. 101,280 kutoka mfuko wa jichangie ambayo ni sh. 200 kwa kila tiketi.
Nauli ya ndani kwa waamuzi, kamishna na mtathimini wa waamuzi ni sh. 90,000. Posho ya kujikimu kwa kamishna ni sh. 40,000. Gharama ya tiketi ni sh. 1,230,000 wakati usafi na ulinzi ni sh. 500,000.
Baada ya gharama hizo za awali kila klabu ilipata sh. 907,424, gharama za mchezo sh. 302,475, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu- FDF (sh. 151,237), Uwanja sh. 302,475, DRFA (sh. 120,990) na Baraza la Michezo la Taifa- BMT (sh. 30,247).
Powered by Sorecson : Creation de site internet
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...