Balozi Ramadhan M. Mwinyi, Naibu Balozi wa Ubalozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa akisisitiza umuhimu wa kuimarishwa na kujengewa uwezo kwa Idhaa ya Radio ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, ilikuwa ni wakati wa Mkutano wa Kamati ya Nne ya Baraza Kuu la 67 la UM uliokuwa ukijadili ajenda namba 55 kuhusu suala la Habari na Mawasiliano ya Umma ya UM. Idhaa hiyo ya Kiswahili ya UM, inaongozwa na Mtanzania Bi. Flora Nducha. Kazi kubwa iliyofanywa na Ubalozi wa Tanzania wa kukumbushia mara kwa mara kuhusu upungufu wa wafanyakazi katika Idhaa hiyo, imezaa matunda baada ya UM kupitia Idara yake ya Habari na Mawasiliano kuongeza wafanyakazi watatu kati ya watano. Mmoja kati ya wafanyakazi hao wapya ni Mtanzania Bi. Asumpta Masoi aliyekuwa Mwandishi wa Habari Mkuu kutoka Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC)
Na Mwandishi Maalum
Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Tanzania imeelezea kuridhishwa na hatua ya Umoja wa Mataifa kupitia Idara yake ya Habari na Mawasiliano
ya Umma ya kuiimarisha na kuiongezea Uwezo Radio Idhaa ya Kiswahili ya Umoja Huo.
Hayo yameelezwa jana ( jumatano) na Ramadhan Muombwa Mwinyi, Naibu Balozi wa Ubalozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa
Mataifa, wakati alipokuwa akichangia majadiliano
ya Kamati ya Nne ya Baraza Kuu la
67 la Umoja wa Mataifa, kuhusu ajenda namba 55 inayohusu masuala ya Habari na Mawasiliano katika
UM.
Majadiliano ya ajenda hiyo yalitanguliwa
na hotuba ya Rais wa Baraza Kuu la 67 la UM, Bw. Vuk Jeremic
siku ya jumanne. Siku ambayo pia Katibu Mkuu Msaidizi anayesimamia Idara
hiyo
Bw Peter Launsky-Toeffenthal aliwasilisha mbale ya wajumbe wa
Kamati taarifa yake iliyoainisha kazi na
majukumu ambayo yametekelezwa na vitengo
mbalimbali vivilivyo chini yake.
“ Mwenyekiti, ujumbe wangu ungependa kuzungumzia jambo moja
ambalo kwetu lina umuhimu wa aina yake
nalo ni hili la Radio ya Idhaa ya
Kiswahili” akasema Balozi Mwinyi
Na kuongeza. “ Tangu kuanzishwa kwake Idhaa hii tofauti
na Idhaa nyingine imekuwa ikitekeleza majukumu yake katika mazingira
magumu hasa ya upungufu wa wafanyakazi. Lakini
tumefarijika na taarifa za hivi
karibuni kwamba, nafasi tatu kati ya tano zilizotengwa zimekwisha kujazwa.
Nimatumaini yetu kwamba na hizi mbili zilizobaki zitajazwa mapema iwezekanavyo” akasisitiza Balozi.
Aidha Naibu Balozi amesema kwa kuongeza wafanyakazi zaidi, idhaa hiyo
sasa itatekeleza majukumu yake kwa
ufanisi, weledi na kwa ubora wa hali ya
juu. Na hivyo kutimiza vema jukumu lake la msingi ambalo ni kuhabarisha na kuelimisha mamilioni ya watu
wanaofahamu lugha ya kiswahili kuhusu majukumu ya UM.
Halikadharika Balozi
Mwinyi akaeleza kuwa, Tanzania inafarijika pia kwamba baadhi ya machapisho yanayolenga kampeni mbalimbali yamekuwa
yakitafsiriwa katika lugha ya kiswahili.
“ Hatua hii ya
kutafsiri kwa kiswahili baadhi ya machapisho ni kielelezo sahihi cha namna UM
inavyotambua na kuthamini mchango wa
lugha ya Kiswahili. Tunaelewa hali
ngumu ya rasilimali ilivyo kwa UM na Idara hii kwa ujumla, lakini ni imani
yetu tafsiri hizi zitaendelea kufanyika”. Akasihi.
Kwa muda mrefu na kwa nyakati tofauti,Mabalozi wa Tanzania
katika Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana
na maafisa wao wa Kamati ya Nne na ya
Tano wamekuwa mstari wa mbele
kuzungumzia upungufu wa wafanyakazi
katika idhaa hiyo na hivyo kuutaka UM kuitafutia ufumbuzi hali hiyo.
Malalamiko hayo pamoja na yale ya kupandishwa
hadhi Mkuu wa Idhaa hiyo hatimaye yamezaa matunda ambayo yamepelekea kuongezwa
kwa wafanyakazi na Mkuu wake kupandishwa Hadhi.
Kati ya wafanyakazi walioogezwa yupo Bi. Asumpta Masoi aliyekuwa Mwandishi wa Habari Mkuu wa Shirika la Utangazaji la Tanzania ( TBC) ambaye
amejiunga hivi karibuni na hivyo kufanya Idhaa hiyo sasa kuwa na Watanzania wawili. Wafanyakazi wengine ni kutoka Kenya na Uganda.
Ingawa lugha ya
Kiswahili si kati ya lugha rasmi Sita
za UM, lakini miaka kadhaa
iliyopita Umoja huo, uliamua kuazisha Idhaa ya Kiswahili sambamba na Idhaa ya lugha ya Kireno ili kukidhi mahitaji ya
wazungumzaji wa lugha hizo kwa lengo pia
la kufikisha habari zake kwa watu wengi zaidi na wa mataifa mbalimbali.
Lugha rasmi za UM ni Kiingereza,
Kifaransa, Kiarabu, Kirusi, Kichina na kihispania.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...