Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Serikali imesema imejipanga kuhakikisha kuwa majadiliano ya ushirikiano kwa manufaa ya wote (Smart Partnership Dialogue) yanafanikiwa, yanakuwa endelevu na manufaa kwa nchi kwa muda mrefu ujao.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alipokua akiongea na waandishi wa habari kuhusiana na matayarisho ya mikutano ya kitaifa na ule wa kimataifa kuhusiana na majadiliano hayo hapa nchini.

“Tunafanya mambo mengi kuhakikisha majadiliano haya yanafanikiwa,” alisema balozi Sefue jijini Dar es Salaam hivi karibuni wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya mikutano hiyo miwili muhimu.

Alisema serikali inashirikiana kwa karibu sana na nchi zote ambazo zimewahi kuwa mwenyeji wa majadiliano haya kupata uzoefu wao na kuyazingatia katika maandalizi hayo pamoja na kuwa mahusiano ya karibu na Sekretarieti ambayo iko mjini London.

“Tunashirikiana na wataalamu mbalimbali wa ndani na nje ya nchi katika eneo ambalo Mhe. Rais amelichagua kuwa mada kuu ya majadiliano haya ambalo ni namna ya kutumia teknolojia kufikia maendeleo ya kiuchumi na kijamii,” alisema.

Alifafanua kwamba kama nchi, Tanzania imejipanga kuhakikisha kuwa majadiliano haya yanafanikiwa na yanakua ya manufaa.

Haya ni majadiliano yanayolenga kutoa fursa kwa jamii kukaa pamoja na kuzungumzia maswala mbalimbali ya maendeleo.

Kwa hapa Tanzania, chombo kitakachosimamia na kuratibu majadiliano haya kitaifa ni Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) wakati Wizara ya Mambo ya Nje ina jukumu la kuratibu mkutano wa kimataifa kuhusu majadiliano hayo hapa nchini mwezi Mei, 2013.

Mchakato wa majadiliano haya ulishazinduliwa na Rais Jakaya Kikwete tangu Mei, 2012.

Akizungumzia jukumu hilo la TNBC, Balozi Sefue ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati ya utendaji ya baraza hilo alisema chombo hicho kina uzoefu wa kukutanisha makundi mbalimbali, kujadiliana kwa uwazi na kukubaliana jinsi ya kuendesha mambo katika nchi kwa faida ya serikali na wafanyabiashara.

“Katika utaratibu huu wa majadiliano kwa manufaa ya wote tunahusisha makundi mengi zaidi na hivyo baraza litatumia uzoefu wake kuratibu majadiliano hayo kitaifa,” alisema.

Majadiliano ya kimataifa yanasimamiwa na Wizara ya Mambo ya Nje.

Mkutano wa mwezi Mei, 2013 ni mwendelezo wa mikutano kama hii ambayo imeanza kiasi cha miaka kumi na tano iliyopita na ikianzishwa na Jumuia ya Madola kupitia taasisi yake inayoitwa Commonwealth Partnership for Technology Management na kwa ushiriki mkubwa wa aliyekuwa waziri Mkuu wa Malaysia, Dkt. Mahathir Mohamad.

Tayari TNBC imeshaanza kuendesha semina za uhamasishaji zenye lengo la kutoa ufahamu kuhusu majadliliano ya kitaifa kabla ya yale ya kimataifa.

Kitaifa, majadiliano haya yatahusisha makundi mbalimbali yakihusisha serikali, wanasiasa, wafanyabiashara, wasomi,wafanyakazi, vijana, wasanii na wakulima ambao watakaa pamoja na kujadili maswala mbalimbali yanayohusu biashara na maendeleo.

Makundi haya yatapata fursa hiyo kupitia mabaraza ya mikoa na yale ya wilaya ya TNBC ambako madajiliano hayo yatafanyika kuanzia huko hadi ngazi za kitaifa kabla ya majadiliano ya kimataifa mwezi Mei.

Makundi yote yatapata fursa ya kujadili na kutoa mapendekezo yao.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. majadiliano ya wana-Mtwara na serikali kuu DSM kuhusu gesi kuchochea viwanda mkoani Lindi na Mtwara lini?

    Majadiliano ya serikali na wananchi wa sehemu zenye migodi na serikali kuu DSM lini?

    Mdau
    Mikindani

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...