NA MIZA KONA / HABARI MAELEZO ZANZIBAR

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imeamua kulivunja Shirika la Utalii Zanzibar kutokana na changamoto zinazolikabili Shirika hilo hivi sasa.

Akiwasilisha hotuba ya Makadirio ya Mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2013/2014 huko katika Baraza la Wawakilishi Chukwani,Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Said Ali Mbarouk amesema sababu kubwa ya kuvunjwa shirika hilo ni kushindwa kuhimili ushindani uliopo wa biashara ya sekta hiyo.

Amesema kuwa taratibu za kulivunja rasmi Shirika la Utalii la Zanzibar zinatarajiwa kukamilika katika muda mfupi ujao kuanzia sasa.

Akizungumzia Shirika la Utangazaji Zanzibar(ZBC) amesema linatarajia kuweka vifaa vipya vya Studio pamoja na kununua gari moja ya kurushia matangazo ya moja kwa moja kutoka nje ya studio hasa katika sherehe na maadhimisho ya Kitaifa.

Waziri Said Ali Mbarouk amesema lengo la Wizara ni kusimamia mazingira bora ya kazi ili kuliwezesha Shirika la ZBC kutoa huduma bora na zenye ufanisi.

Akitoa maoni ya Kamati ya Mifugo, Utalii, Uwezeshaji na Habari Mwenyekiti wa kamati hiyo Mlinde Mbarouk Juma wameshauri watendaji wa Shirika la Utangazaji Zanzibar kubadilika kiutendaji. kufanyakazi kwa umakini zaidi na kuacha kufanyakazi kwa mazoea .

“Kwa kuwa uendeshaji wa Mfumo wa Digital unahitaji umakini wa hali ya juu kwa kutokuwa makini tutakuja kulaumiana na kuona ni bora tungelibaki katika mfumo wa analogia”, alisema Mwenyekiti Mlinde.

Aidha ameeleza kuwa Utalii ni chachu ya maendeleo katika nchi jirani, lakini bado Zanzibar haujapewa kipaumbele na kuwekewa mikakati na kuwanufaisha wananchi wengi.

“Kamati inatoa rai kwamba dhana ya Utalii kwa wote itekelezwe kwa vitendo na wala sio maneno pamoja na kuwekwa sera na sheria ambazo zitapunguza gharama kwa wazawa.” Alisisitiza Mlinde.

Wameishauri Wizara kujidhatiti katika kuutangaza Utalii wa Zanzibar kwani kufanya hivyo utaweza kuongeza soko katika mataifa mbali mbali na kuitangaza katika nchi za jirani.

Katika kutekeleza majukumu yake Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo imeomba iidhinishiwe jumla ya shilingi 9,985,000,000 kwa kazi za kawaida na shilingi 510,000,000 kwa kazi za maendeleo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 2 mpaka sasa

  1. AnonymousJuly 23, 2013

    Shirika la Utalii la Zanzibar limefanyiwa ufisadi kwa miaka mingi. Shirika linamiliki Mahoteli makubwa Zanzibar kama Bwawani, Afrika House, Zanzibar Hotel itakuwaje yashindwe na vihoteli mbuzi? Disco kila weekend linajaa, pesa zimekwenda wapi? Tupeni ukweli!!!

    ReplyDelete
  2. AnonymousJuly 24, 2013

    Tatizo kubwa la shirika la utalii Zanzibar ni kutokusikiliza ushauri,
    Nilikuwa mmoja wa watafiti sekta ya utalii mwishoni mwa miaka 80s,na tuliishauri SMZ kuwa wangarifu na makini katika kufungua milango kwa wawekezaji wa sekta ya utalii,pia tuliwashauri wajipange na kujiandaa vema.
    Jibu la mmoja wa maofisa wa juu wizarani alitujibu kuwa cha msingi kwa SMZ ni pesa za nje.
    Sasa leo wanavuna walichopanda.
    Mdau
    Ughaibuni

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...