MECHI ZA YANGA, SIMBA ZAINGIZA MIL 182/-
Mechi
za Yanga na Simba za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) zilizochezwa wikiendi
iliyopita jijini Dar es Salaam zimeingiza jumla ya sh. 182,103,000.
Yanga
katika mechi yake dhidi ya Ruvu Shooting iliyochezwa Jumamosi (Septemba
28 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuibuka na ushindi wa
bao 1-0 imeingiza sh. 94,202,000.
Watazamaji
16,492 walikata tiketi kushuhudia pambano hilo ambapo kila klabu
ilipata mgawo wa sh. 22,630,921.58. Viingilio katika mechi hiyo vilikuwa
sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000, na Kodi ya Ongezeko la
Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 14,369,796.61.
Mgawo
mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 11,507,248.26,
tiketi sh. 3,117,215, gharama za mechi sh. 6,904,348.96, Kamati ya Ligi
sh. 6,904,348.96, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh.
3,452,174.48 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA)
sh. 2,685,024.59.
Nayo
Simba ambayo iliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya JKT Ruvu katika
mechi iliyochezwa Jumapili (Septemba 29 mwaka huu) katika Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 87,901,000.
Watazamaji waliokata tiketi kushuhudia pambano hilo namba 41 walikuwa 15,780. Viingilio
katika mechi hiyo vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh.
20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 21,051,025.92 wakati Kodi ya
Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 13,408,627.12.
Mgawo
mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 10,703,911.48,
tiketi sh. 3,132,963, gharama za mechi sh. 6,422,346.89, Kamati ya Ligi
sh. 6,422,346.89, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh.
3,211,173.44, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh.
1,248,789.67 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) sh.
1,248,789.67.
Wakati huo huo, mechi ya ligi hiyo kati ya Mbeya City na Coastal Union iliyochezwa
Jumamosi (Septemba 28 mwaka huu) Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini
Mbeya imeingiza sh. 16,959,000 huku kila klabu ikipata sh. 4,035,229.
Mgawo
wa mechi hiyo ulikuwa ifuatavyo; Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) sh.
2,586,966, uwanja sh. 2,051,811.57, tiketi sh. 696,290, gharama za mechi
sh. 1,231,086, Kamati ya Ligi sh. 1,231,086, Mfuko wa Maendeleo ya
Mpira wa Miguu (FDF) sh. 615,543, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mbeya
(MREFA) sh. 478,756.
MICHUANO YA CHALENJI KUANZA NOV 27
Michuano
ya Kombe la Chalenji inayoandaliwa na Baraza la Vyama vya Mpira wa
Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) inafanyika Kenya kuanzia Novemba
27 hadi Desemba 12 mwaka huu.
Nchi
wanachama ambazo zinataka kushiriki zinatakiwa kuthibitisha ushiriki
wao kwa Sekretarieti ya CECAFA kabla ya Oktoba 20 mwaka huu. Wanachama
wa CECAFA ni Burundi, Djibouti, Eritrea, Ethiopia, Kenya, Rwanda,
Somalia, Sudan, Sudan Kusini, Tanzania, Uganda na Zanzibar.
Michuano
hiyo itatanguliwa na Mkutano Mkuu wa CECAFA utakaofanyika Novemba 26
mwaka huu ambao pamoja na mambo mengine utakuwa na ajenda ya uchaguzi.
Uchaguzi huo ni kwa ajili ya kujaza nafasi nne za wajumbe wa Kamati ya
Utendaji.
Wajumbe
wanaomaliza muda wao ni Sahilu Gebremarian wa Ethiopia ambaye pia ni
Makamu Mwenyekiti wa CECAFA, Abdigaani Saed Arab (Somalia), Tariq Atta
(Sudan) na Raoul Gisanura (Rwanda).
Majina
ya wagombea yanatakiwa kuwa yamewasilishwa katika Sekretarieti ya
CECAFA kabla ya Oktoba 20 mwaka huu, na yakiwa yamethibitishwa na vyama
vyao vya mpira wa miguu.
SUALA LA PAPIC, YANGA LASUBIRI UAMUZI WA FIFA
Shirikisho
la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limewasilisha rasmi suala la
madai ya aliyekuwa Kocha wa Yanga, Kostadin Papic dhidi ya klabu hiyo
katika Kamati ya Hadhi ya Wachezaji.
FIFA
imesema imepeleka rasmi suala hilo katika kamati yake hiyo baada ya
kupokea vielelezo vya Papic anayedai kuidai Yanga dola 10,000 za
Marekani pamoja na vile vya Yanga inayodai kumlipa kocha huyo fedha zote
alizokuwa akiidai klabu hiyo.
Kwa
taratibu za FIFA, hivi sasa haitapokea vielelezo vingine kutoka pande
hizo mbili, na badala yake Kamati hiyo inayoongozwa na Theo Zwanziger
kutoka Ujerumani itafanya uamuzi na kuziarifu pande husika. Zwanziger
kitaaluma ni mwanasheria.
Papic
aliyeinoa Yanga kwa vipindi viwili tofauti aliwasilisha malalamiko yake
FIFA akidai hadi mkataba wake unamalizika klabu hiyo ilikuwa haijamlipa
dola 10,000 za Marekani.
LIPULI, MAJIMAJI KUUMANA WAMBI FDL.
Mechi
ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kati ya Lipuli ya Iringa na Majimaji ya
Songea sasa itachezwa kesho (Oktoba 2 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Wambi
uliopo Mafinga badala ya Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa.
Mabadiliko
hayo yamefanyika kutokana na Serikali kuutumia Uwanja wa Kumbukumbu ya
Samora kwa ajili ya shughuli za mbio za Mwenge.
Mechi
nyingine ya FDL kesho itakuwa kati ya Tessema FC ya Dar es Salaam na
Ndanda FC ya Mtwara, na itafanyika kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume
jijini Dar es Salaam.
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...