Baraza la madiwani halmashauri ya wilaya ya Makete likiendelea.
 Diwani wa kata ya Matamba mh. Asheli Mwalyoyo akichangia hoja
 Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Makete Mh. Daniel Okoka akiongoza kikao hicho
 Mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Josephine Matiro akitoa ufafanuzi kuhusu suala la leseni katika baraza hilo.
 Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Makete ambaye pia ni katibu wa kikao hicho Bw. Iddi Nganya akisoma taarifa ya rasimu ya bajeti ya halmashauri yake kwa mwaka 2014/2015.
 Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Makete Francis Chaula akisikiliza kwa makini hoja za madiwani katika kikao hicho.
Na Edwin Moshi, Makete
Baraza maalum la madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Makete mkoaniNjombe leo Januari 28 limejadili na kupitisha rasimu ya bajeti ya halmashauri hiyo kwa mwaka 2014/2015.
Katika kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Makete madiwani hao wamejadili hoja mbalimbali zilizopo katika rasimu hiyo ikiwemo uboreshaji wa namna ya kuongeza mapato kutoka kwenye vyanzo vyote vilivyoainishwa na halmashauri hiyo.
Baadhi ya hoja zilizochangiwa na madiwani hao ni pamoja na halmashauri kuwa na vyanzo vya kukusanya mapato lakini kumekuwa na tatizo la mapato hayo kutofika kama yalivyokusanywa wakimaanisha kumekuwepo na kukosekana kwa uaminifu kwa baadhi ya watendaji wanaokusanya mapato hayo.
Diwani wa kata ya Matamba (CCM) Mh. Asheri Mwalyoyo ametolea mfano katika kata yake kuwa kumekuwepo na ukusanyaji wa mapato lakini taarifa zinazofika wilayani zinaonesha yamekusanywa mapato kidogo ilihali ana uhakika yamekusanywa mengi.
"Tuchukulie kwenye kata yangu ya Matamba ushuru tu wa pombe kwa vilabu 10 tu ni shilingi 60,000/- kwa mwezi lakini kwenye taarifa huku wilayani inaonesha ushuru wa pombe za kienyeji ni 70,000/- sasa hii inashangaza maana tuna vilabu vingi, hapa ni kukosekana kwa uadilifu wa baadhi ya watendaji wanaokusanya mapato hayo" alisema Mwalyoyo.
Naye diwani wa kata ya Tandala Mh. Egnatio Mtawa ameshangazwa na hatua ya rasimu hiyo kuonesha kutegemea kwa kiasi kikubwa mapato ya pombe na kudai kuwa wahusika wote wakiwemo watendaji na wao kama madiwani walikuwa wavivu wa kufikiri kubuni vyanzo vipya vya kukusanya mapato badala ya kutegemea ushuru wa pombe kwa kiasi kikubwa.
Amesema hii inaashiria wananchi wazidi kunywa pombe kwa wingi ili mapato yapatikane lakini pia njia hiyo itachochea vilabu na baa kufunguliwa mapema tofauti na sheria inavyoruhusu hivyo kupata wingi wa wananchi watakao kuwa wamelewa muda wote hasa muda wa kufanya kazi.
Aidha rasimu hiyo pia imeainisha vyanzo vipya vitakavyosaidia kuongeza mapato ya halmashauri ikiwemo ushuru wa majengo ambapo watu waliokwisha jenga nyumba tayari watakuwa wanalipia ushuru wa jengo kwa mwaka na wale ambao bado wana mpango wa kujenga watalipia kabla ya ujenzi kuanza.
Halmashauri ya wilaya ya Makete ni miongoni mwa wilaya ambayo ina vyanzo vichache vya mapato hali inayosababisha upatikanaji wa mapato yake kuwa mdogo, hivyo inaendelea kubuni vyanzo vipya ili mapato yake yaweze kuongezeka zaidi ya sasa


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...